Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Esther Edwin Maleko

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. ESTHER E. MALLEKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kunipa fursa hii ya kuchangia kwenye Wizara hii ya Elimu. Kwanza nianze kwa kutoa pongezi nyingi sana kwa utekelezaji wa elimu bila malipo kwa sababu kwa sasa wanafunzi ambao wanahitimu wameongezeka na wataendelea kuongezeka kwa kasi kubwa. Sasa ni vyema basi Serikali ijipange ni namna gani basi itaweza kukabili mahitaji haya makubwa ya miundombinu ambayo tayari imeanza kuelemewa. Wizara imeomba kuidhinishiwa kiasi cha shilingi trilioni 1.384 ambazo zina ongezeko la shilingi bilioni 42.4 ikilinganishwa na bajeti ya mwaka 2020/2021, nawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kati ya fedha hizo matumizi ya kawaida ni bilioni 480.5 ambayo ni sawasawa na asilimia 34.7 na maendeleo ni bilioni 903.9 ambayo ni sawasawa na asilimia 65.3 tunawapongeza sana kwa uwiano huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo kati ya fedha hizo fedha za maendeleo ni bilioni 403, lakini bilioni 500 zinakwenda kwenye mikopo ya elimu ya juu. Sidhani kama ni sahihi fedha za mafunzo au training kuitwa fedha za maendeleo maana matumizi yake ni ya kawaida na matumizi ya fedha za maendeleo hayawezi kwenda kuwekwa kwenye fedha ambazo tunasema zinapelekwa kwenye mikopo ya elimu ya juu. Kwenye mafungu mengine ya fedha za kugharamia mafunzo ziko recurrent, ndio maana fedha zisipotolewa zote kinacho-suffer ni ile miradi ya maendeleo.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano, katika mwaka huu mpaka Machi, 2021 miradi sita tu kati ya miradi 33 ya mikakati ya maendeleo ndio imepata fedha, lakini hii mingine mpaka sasa haijapata. Miradi hiyo ni EP4R na Equip T haijapata chochote mpaka sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu, ni vyema basi zile fedha za mikopo ya elimu ya juu zipewe fungu lake tofauti ya kujitegemea ili zile fedha za miradi zisiweze kuguswa na ziende kwenye ile miradi, ili iweze kutekelezeka.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo linguine, TAMISEMI tunaomba waboreshe ushirikiano kati yao na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ili waweze kushirikiana vyema kutoa huduma hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine, sina uhakika sana kama Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia wanajua mahitaji makubwa ambayo yanatokana na kuanzisha utekelezaji huu wa elimu bila malipo. Kwa sababu katika kipindi hiki cha miaka minne tutakuwa tunahitaji madawati 41,333; tutakuwa tunahitaji matundu ya vyoo 75,300; vitabu 18,000,825; na walimu 41,833; na fedha za ruzuku ya wanafunzi bilioni 1,882,000,500; ambayo hiyo ni sawa na trilioni 1.476 ili kuweza kukamilisha shughuli hii ya wanafunzi watakaoongezeka katika kipindi hicho cha miaka minne. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tunaomba ushirikiano bora kati ya TAMISEMI, watakaowasaidia kufuatilia miradi inayotekelezwa kwenye wilaya mbalimbali mfano VETA na vyuo vikuu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kufikia hapo, huo ndio mchango wangu. Naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Ahsante. (Makofi)