Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Abdallah Dadi Chikota

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nanyamba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami nichangie hoja iliyopo Mezani. Niungane na wenzangu waliopita kuchangia kuwapongeza viongozi wa Wizara hii tukianza na Waziri wa Elimu, mwalimu wangu, Mheshimiwa Profesa Ndalichako; Naibu wake, Mheshimiwa QS Omari Kipanga; na Katibu Mkuu, kaka yangu, Dkt. Akwilapo; na wasaidizi wake kwa jinsi wanavyochapa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tukiangalia hotuba hii unajua kabisa imeandaliwa na walimu, ina maelezo machache na takwimu nyingi na inajieleza wazi nini kimefanywa ndani ya mwaka mmoja na miaka mitano iliyopita.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile hotuba hii imekuja na majibu ya kilio cha Watanzania kuhusu sekta ya elimu. Ukisoma ukurasa wa 69 utakuta dhamira ya Wizara kwamba sasa inakusudia kufanya mapitio makubwa, siyo mtaala tu, wataanza kupitia Sera ya Elimu ya Mwaka 2014. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ndugu zangu, tusianze kudai mtaala, tuanze na mabadiliko ya sera. Tukibadilisha sera na vitu vingine vitabadilika. Kwa hiyo, hongereni sana Wizara ya Elimu, mmesema mtabadilisha sera, mnapitia Sera ya Elimu ya 2014 lakini siyo hivyo tu, mtapitia na Sheria yetu ya Elimu, ile Sheria Na. 25 ya Mwaka 1978 pamoja na mabadiliko ambayo yamefanywa. Hapo kwa kweli mnakuja vizuri, kwa sababu lazima tufanye mabadiliko ya jumla na siyo vipande vipande.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa muda wa miaka mitano tumeona Wizara hii ikifanya kazi kubwa ya ukarabati katika miundombinu ya shule. Mkoani Mtwara tumeshuhudia, siyo ukarabati wa Chuo cha Elimu Kitangali, ni ujenzi mpya kwa sababu majengo yote yamewekwa chini na tukaanza na ujenzi mpya, hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitachangia maeneo matatu. Sehemu ya kwanza, pamoja na mambo mazuri ambayo yamefanywa, nami nitilie mkazo kwenye mabadiliko haya ya mtaala. Ni kweli kwamba sasa hivi kilio kikubwa cha wanajamii ni kwamba wahitimu katika mfumo wetu wa elimu wanashindwa kukidhi haja ya mahitaji ya kule wanakokwenda.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba sasa hii dhamira ya mabadiliko ya mtaala yafanywe kiukweli kwa sababu hayo ndiyo mahitaji ya sasa. Ukiangalia sababu za kubadilika kwa mitaala, mojawapo ni mahitaji ya kwenye jamii, ambayo ni haya yanayojitokeza sasa hivi. Kwa hiyo, tufanye mabadiliko ya kweli.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba wakati shughuli hii itakapofanyika basi tuwe na ushirikishaji mkubwa wa makundi yote. Tuanze kuwashirikisha wanajamii, tushirikishe walimu kama watekelezaji wa mtaala, wanafunzi wenyewe washirikishwe, siyo hivyo tu, na taasisi mbalimbali ambazo zinahusika na masuala ya elimu, nao washirikishwe. Hili suala la mabadiliko ya mtaala lisiwe suala la watu wa Wizara ya Elimu tu, iwe ni jamii kwa upana wake na taasisi mbalimbali. Siyo hivyo tu, na wadau mbalimbali ambao wanahusika kwenye sekta ya elimu nao washirikishwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukishabadilisha mtaala, siyo kwamba tumefanikiwa, kuna kazi kubwa sana inabidi ifanyike. Tuna kawaida ya kubadilisha mtaala bila kuangalia tunakwendaje katika kuutekeleza huo mtaala. Kwa hiyo, tukishabadilisha ule mtaala mpya tuandae mazingira ya vyuo vyetu na shule zetu kutekeleza mtaala mpya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwanafunzi au mwanachuo akishaenda kwenye hivyo vyuo vyetu, akute kuna facilities za kutosha kujifunza maarifa mapya ambayo yapo kwenye mtaala mpya. Tukiacha hata shule au taasisi zetu kama ilivyo, tutakuwa na mtaala mpya ambao utashindwa kutekelezeka.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile tunahitaji maandalizi makubwa ya walimu na wakufunzi wetu ili waweze kutekeleza mtaala mpya, kwa sababu hawa ndio watakaokwenda kuutekeleza mtaala. Wasipoandaliwa, kuna kawaida ya kufanya mabadiliko ya mtaala tukaishia kwenye watu wa Wizara au kazi ya kanda tu, tufike mpaka kwa mwalimu wa darasa naye ashirikishwe aweze kutekeleza mtaala mpya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie mchango wangu wa pili kuhusu muundo mpya wa Wizara ya Elimu, hususan nafasi ya Kamishna wa Elimu. Ukisoma Sera ya Elimu na Sheria ya Elimu, Kamishna wa Elimu ana majukumu mazito sana, lakini kwa muundo wa Wizara ya Elimu uliopo, kamishna unampa kusimamia maeneo mawili tu; Elimu ya Msingi kwa maana ya primary na secondary na elimu maalum. Kamishna wa Elimu hagusi elimu ya juu na elimu ya ufundi. Hapa kuna changamoto. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Kamishna wa Ardhi anasimamia ardhi yote, hasimamii ardhi ya mjini tu na kuacha vijijini; na Kamishna wa Kodi anasimamia kodi zote. Kwa nini Kamishna wa Elimu, asimamie elimu ya msingi tu na elimu maalum; elimu ya vyuo vikuu hashughulikii na elimu ya ufundi hashughulikii? Tumpe mamlaka Kamishna wetu wa Elimu. Kama hoja ni sifa, kitu ambacho sioni kama ni sifa, kwa sababu Kamishna wa sasa wa Elimu ni Doctor, ana sifa na ninamfahamu, ni mcha Mungu, ni mwadilifu na mchapa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ili kamishna wetu awe na majukumu kama yanavyotajwa kwenye Sera ya Elimu na Sheria ya Elimu, asimamie sekta zote; ahusike kwenye elimu ya msingi, elimu ya sekondari, elimu ya juu na elimu ya ufundi. Haiwezekani kama mtaaluma mkuu akajifunga katika maeneo machache tu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba Wizara ya Elimu na Wizara ya Utumishi mlishughulikie hili, turudishe muundo wa zamani ambapo Kamishna wa Elimu, kwa tafsiri nyingine Chief Education Officer basi awe Msimamizi Mkuu wa Sekta ya Elimu na siyo ilivyo sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. (Makofi)