Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Mwantumu Mzamili Zodo

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba nikushukuru kwa kupata nafasi ya kuchangia kwenye Wizara hii muhimu ya Elimu. Naomba nianzie kwenye sensa ya watu na makazi ya mwaka 2002. Kwa mujibu wa matokeo ya sensa ya watu na makazi ya mwaka 2002, tulikuwa tupo watu milioni 34 Tanzania. Lakini baada ya miaka kumi sensa ya 2012 tulitoka milioni 34 mpaka milioni 45. Ni nini tafsiri yake. Tafsiri yake ni kuwa kila mwaka kutoka 2002 mpaka 2012 tulikuwa tunaongeza kwa wastani wa watu milioni moja kila mwaka. Kwa maana hiyo pia kila mwaka tuna wajibu wa kuongeza madawati, madarasa, Walimu, vifaa mashuleni kwa sababu idadi ya watu haishuki bali inaongezeka na itaendelea kuongezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tukiangalia kwenye ajira za Serikali. Serikali imeajiri watu 480,000 tu mpaka sasa. Kutoka kwenye watu milioni 45 ni sawa na asilimia moja, lakini wengine wameajiriwa kwenye sekta binafsi na wengine wamejiajiri kwenye kilimo na biashara nyingine kama ujasiriamali na vitu vingine kama hivyo. Sasa tukiangalia takwimu hizo, ipo haja sasa ya kufanya maboresho makubwa kwenye mtaala, kwa sababu ni kiwango kidogo sana kinaajiriwa, asilimia 99 ya watu wanatakiwa wajiajiri wenyewe ndio tafsiri yake. Kwa maana hiyo sasa tunatakiwa tuboreshe mitaala na tuongeze yale masomo ambayo mwanzo tulikuwa tumeyafuta. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, zamani wakati mimi nasoma, kulikuwa na masomo ya sayansikimu, kulikuwa na masomo kama sayansi kilimo, kulikuwa kuna masomo kama maarifa ya nyumbani. Masomo yale yalikuwa yanafundisha vitu mbalimbali, mkiwa kule shuleni mnafundishwa kilimo, upishi, mnapika keki na nini, lakini sasa hivi tunawekeza fedha nyingi sana kwenye elimu bure, tukishamaliza hapo mwanafunzi anamaliza darasa la saba, anakwenda kutoa 350,000 tena kufundishwa kupika keki. Sasa sijui tunamsaidiaje? Tumewekeza fedha nyingi kwenye kumsomesha, halafu bado akatafute tena ujuzi mdogo tu wa kupika keki kwa 350,000. Anakwenda kujifundisha ushonaji ambao mwanzo yalikuwepo hayo masomo, lakini sasa anakwenda kujifundisha kwa 200,000, anakwenda kujifundisha ujasiriamali kwa 500,000.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo Serikali ya Tanzania inawekeza fedha nyingi sana kwenye elimu bure. Kama tunawekeza fedha nyingi kwenye elimu bure, ipo haja ya kufanya maboresho kwenye mtaala wetu umwezeshe mwanafunzi baada ya elimu kujitegemea, lakini sasa wanafunzi hawa pia bado ni ngumu sana kujitegemea moja kwa moja kwa sababu; elimu ya msingi umri wa mwanafunzi kuanza shule ni miaka saba na miaka sita. Mwanafunzi anamaliza elimu ya msingi akiwa na miaka aidha 12 au 13, ni uongo hata kama tutampa hizi stadi mwanafunzi wa miaka kumi mbili atakayemaliza darasa la saba na mfumo ukamuacha akawa amefeli yupo nyumbani, bado hawezi kufanya chochote huyu bado ni mtoto mdogo mnoo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo sasa, niishauri Serikali elimu msingi iwe ni kuanzia darasa la kwanza mpaka kidato cha nne, angalau sasa huyu mwanafunzi wa darasa la kwanza mpaka kidato cha nne; tukimpa sasa hizo skills anaweza baada ya hapo akitoka akaenda kukaanga chips, anaweza akawa bodaboda, anaweza akaenda kwenye ufugaji, anaweza kwenda kwenye kilimo, lakini sio mwanafunzi wa miaka 12 au 13 ambaye mfumo umemwacha, hataweza kufanya chochote. Matokeo yeke ndio hizo ajira za watoto wanachukuliwa kwenda kufanya kazi za ndani, kuuza karanga, tunaona watoto wengi stendi, majumbani, wapo watoto wadogo sana wamemaliza darasa la saba hawakupata bahati ya kuendelea, aidha anafanya kazi za ndani au anauza karanga stendi au anauza mayai ni watoto wadogo mno. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo sasa, naona ipo haja ya kufanya maboresho kwenye mtaala, lakini pia kuangalia elimu msingi iwe ni kuanzia shule ya msingi mpaka form four, angalau mtoto huyu atamaliza form four akiwa aidha na miaka 16 au 17 angalau tutakuwa tumemvuta…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)