Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Zaytun Seif Swai

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. ZAYTUN S. SWAI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia Wizara hii muhimu ya Elimu. Mchango wangu utajikita hasa kwenye kuishauri Serikali katika mambo kadhaa ambayo yanaweza kuinua ubora wa elimu yetu ili kutoa wahitimu wenye weledi na wenye ujuzi sahihi ambao unahitajika katika soko letu la ajira. Naomba vile vile, niwapongeze Kamati ya Huduma za Jamii kwa maoni yao ambayo yanaonesha dira ya kuinua kiwango cha elimu katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nianze kwa kuongelea suala la mikopo ya elimu ya juu. Naomba kwanza nianze kwa kumshukuru Rais wetu mpendwa Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan, kwa kuweza kufuta ile retention fees ya 6% iliyokuwepo katika mikopo ya elimu ya juu. Tunamshukuru sana mama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile naomba nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Elimu, nimesikiliza hotuba yake leo na ameweza kufuata maoni ya Wabunge wengi na kuifuta ile asilimia 10 ya penalty, tunashukuru sana Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye suala la mikopo bado kama Serikali, inabidi tufanye kazi sana, tuendelee kuondoa vikwazo na changamoto mbalimbali ikiwemo masharti magumu kwa wahitimu wetu wenye kupata mikopo hii ya elimu ya juu. Asilimia 15 ya marejesho ya mikopo hii bado ni kubwa kwa wahitimu wetu. Wahitimu wetu wengi wakiajiriwa wanapata mishahara ya kima cha chini na walio wengi hawazidi shilingi laki tano. Kuwatoza asilimia 15 ya marejesho ya mikopo ya elimu ya juu, bado kuna kodi na pensheni pamoja na tozo nyingine kwa kweli hatuwatendei haki wahitimu wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naishauri Serikali kupitia Bodi ya Mikopo iweze kupunguza asilimia hii hadi kufikia basi angalau asilimia 10 ili tuweze kuwawezesha wahitimu wetu waishi maisha mazuri. Vilevile, tuwape nafasi wale ambao wanaweza kuchangia zaidi ya asilimia 10, basi wapeleke marejesho yao katika Bodi ya Mikopo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tatizo la ajira kwa wahitimu wetu bado ni changamoto. Naishauri Serikali, ili kukabiliana na tatizo hili, basi Serikali ianzishe scheme maalum ya mikopo kwa wahitimu wetu ili basi, wakimaliza pale vyuo vikuu kama hawajapata ajira, waweze kujiajiri wenyewe katika sekta ambazo siyo rasmi. Vile vile, nashauri mikopo hii tuishushe kwenye vyuo vyetu vya kati ikiwemo VETA ili basi wahitimu wetu wa-apply ujuzi wao na kwa kutumia mikopo hii waweze kujiajiri na kujitegemea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nizungumzie suala la TEHAMA. Sasa hivi dunia yote inaelekea kwenye digital economy. Naomba Serikali kupitia Wizara ya Elimu iweze kuwekeza katika masomo ya TEHAMA hususan katika shule za sekondari ili basi, tuweze kuwawezesha vijana wetu kupambana na huu uchumi wa kidijitali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo hii ukitaka kuongeza ukusanyaji wa mapato kidijitali, unahitaji wataalam wazuri wa TEHAMA; ukitaka kupata wataalam wa masoko ya mazao yetu na bidhaa nyingine, tunahitaji wataalam wazuri wa TEHAMA. Kwa hiyo, basi naweka msisitizo katika Wizara hii ya Elimu tuweze kuwekeza kwenye masomo ya TEHAMA ili tuwasaidie vijana wetu wapambane na changamoto za uchumi wa kidijitali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa ujumla, ili kuinua elimu yetu ya msingi na sekondari, nashauri, tuweze kuboresha mazingira mbalimbali ya utoaji wa elimu ikiwemo kuweka miundombinu ambayo ni bora zaidi, ikiwemo nyumba za walimu, madarasa na maabara hususan kwenye shule zile za sayansi. Tukiweka mazingira bora ya kufundishia na vile vile, tukiwapa motisha walimu wetu hususan wale wenye kufundisha vizuri na kufaulusha na wale wenye kufundisha kwenye mazingira magumu labda shule za pembezoni, sasi tutaweza kuinua elimu yetu kwa kiasi kikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata kule Loliondo Ngorongoro, Karatu, Mang’ola, Lokisale, Monduli walimu wetu watapenda kwenda kufundisha wanafunzi wetu na kwa ujumla tutaweza kuinua kiwango chetu cha elimu.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru, naunga mkono hoja. (Makofi)