Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. George Boniface Simbachawene

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibakwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba nianze kwa kuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote kwa michango yao mizuri waliyochangia na kusema ukweli michango pamoja na kwamba ni siku moja lakini michango ni mingi mno. Umetuendesha vizuri na tumepata wachangiaji 25 waliopata kusema. Lakini pia tumepata wachangiaji wengi walioweka kwa maandishi. Niseme tu kwa kweli michango yote tunaithamini na tutaichukua yote kwa ajili ya kuifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini nafahamu pia wako ambao hawakusema lakini pia hawakuandika ila kwa namna moja ama nyingine tumekuwa tukikutana wakieleza yao. Nataka niseme tu wote michango yenu tutaitumia katika kuhakikisha kwamba tunaboresga utendaji kazi na kuleta mabadiliko katika Wizara hii ya Mambo ya Ndani.

Mheshimiwa Spika, nianze na mchangiaji wa kwanza ambaye ni Kamati yenyewe ya Nje, Ulinzi na Usalama. Michango na maoni yote ya Kamati ya Nje, Ulinzi na Usalama kamati inayoongozwa na Mheshimiwa Zungu, yote kabisa tunaichukua kama ilivyo na sisi kwetu ni suala la kuifanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, Kamati hii ina watu wenye weledi, tunafanya nao kazi kwa karibu na tukijifungia kule tunafundana kweli kweli. Ndiyo maana mengi hapa hayajasemwa lakini hata ambayo hayakuja hapa sisi tunayafahamu na tunayafanyia kazi kwa kadri walivyotuelekeza. Kwa hiyo, nawashukuru sana Wajumbe wa Kamati wote kabisa na hotuba yenu yote sisi tumeichukua na tutaifanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, sio rahisi sana kujibu hoja zote zilizosemwa hapa kwa maandishi na wale waliosema na kwa hivyo nitajaribu kusema baadhi ya zile ambazo kwa mujibu wa uzito wake basi zinapaswa kutolewa majibu hapa.

Mheshimiwa Spika, zimezungumzwa changamoto za vyombo vyote, Polisi, Magereza, Uhamiaji, Zimamoto, juu ya changamoto ya vitendeakazi, changamoto ya makazi ya askari, ofisi zenyewe (vituo) au makambi ya magereza. Yamezungumzwa hapa masuala ya maslahi ya watumishi, upungufu wa watumishi kwa maana ya askari. Yote haya ukiyaangalia kwa namna yalivyo, ni suala la fedha. Kama bajeti ikiruhusu tunaweza tukamaliza matatizo haya yote na tufahamu kuwa nchi yetu hii ni kubwa, Wilaya nyingi bado hazina huduma muhimu, hatuna vituo vya polisi, hatuna makambi kwa ajili ya magereza na nchi inapanuka na kila siku tunaanzisha maeneo ya utawala mapya.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niseme changamoto hii tunaichukua kama Serikali na kadri bajeti zinavyokwenda tutakuwa tunapungua changamoto na mtaona hata katika kitabu chetu cha hotuba ya Wizara ya Mambo ya Ndani tumeweka fedha nyingi sana kwenye development sasa. Kubwa ni kwamba fedha hizo zipatikane na tuweze kutekeleza miradi hiyo, inayoendelea na ile ambayo itatekelezwa kwa fedha hizi ambazo tunaziomba safari hii.

Mheshimiwa Spika, nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge, changamoto ni nyingi, zote mlizozisema, nyingi zinahitaji fedha. Kama fedha hakuna, hakuna muujiza hapo. Na siwezi kusema kwamba nitafanya kwa sababu ni fedha ndiyo itakayofanya. Kwa hiyo, nawaomba Waheshimiwa Wabunge mtuelewe, kadri Serikali itakavyokuwa inapata fedha tutaendelea kupunguza changamoto mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, tunayo magari takribani 357 ambayo yataingia wakati wowote kwa ajili ya Jeshi la Polisi. Tutajitahidi tugawane kwa kuangalia uzito wa maeneo yetu mbalimbali. Safari hii tutaangalia maeneo ya vijijini zaidi na ya mipakani ambako huko ndiko kuna changamoto nyingi sana. Nimeongea na IGP amesema kweli kabisa this time tutayapeleka magari haya vijijini zaidi kuliko hata mijini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini ukiangalia katika ujenzi wa makazi ya askari katika kila jeshi tumepanga kiwango cha fedha ambazo zitakwenda. Kuna ambao wana shilingi bilioni sita, bilioni tatu, bilioni mbili; zitatusaidia kwa kiasi kikubwa kupunguza changamoto hii ikiwemo na kusaidia miradi inayoendelea sasa. Tumepewa fedha nyingi sana ambazo kusema kweli zitatusaidia sana, Dodoma tu hapa tunajenga nyumba nyingi tu, lakini na mikoa kadhaa tutajenga nyumba nyingi tu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niwaambie Waheshimiwa Wabunge changamoto hizi tunazifahamu kama Serikali na kusema ukweli askari wetu wanaishi katika makazi ambayo hayafai ukilinganisha na mabadiliko ya uchumi na kadiri tunavyokwenda kwenye uchumi wa kati, haiwezekani sekta nyingine zimekuwa sana elimu, afya lakini sekta hii ya ulinzi bado hatujaikuza kulingana na mazingira tunayokwenda nayo. Bado kuna majengo ya kikoloni yanaonekana, lock up za kikoloni, cell za kikoloni, bado tuna kazi kubwa ya kufanya. Mimi niseme natambua sana michango ambayo imetolewa na Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Spika, yako mengine ambayo yamezungumzwa ni very specific. Kuna hili lilizungumza juu ya mafunzo yale ya utayari ya askari polisi. Yale mafunzo siyo mafunzo kama mtu anaenda kusomea kazi mpya. Ni mtu anaenda kufanya mafunzo ya utayari, ukakamavu, sasa ile ni sehemu ya kazi. Hizi Sh.10,000 ambazo wanapewa kila siku kama ration allowance huwa ni kwa ajili ya askari huyo kupata chakula. Kwa hiyo, awe yuko ofisini, barabarani, likizo au ypo kwenye training ya mafunzo hayo ni hela hiyohiyo ndiyo anayotakiwa kula.

Mheshimiwa Spika, ndiyo maana sasa ukisema unamlipa nyingine wakati ana hela ya kula na ameenda kwenye mafunzo ya utayari, jamani, unajua kuna utofauti kati ya vyombo hivi vya kijeshi na civil service ya kawaida. Hawa wanajeshi utayari ni sehemu ya kazi yao, yaani kunyakua, kuruka kichura na kadhalika ni sehemu ya shughuli yao sio mafunzo kama mafunzo mapya. Kwa hiyo, anapokwenda pale anahama na ileile Sh.10,000 yake anaenda kuila akiwa kule kwenye yale mafunzo kwa sababu ukimlipa utakuwa umemlipa double payment na kwa mujibu wa sheria za Serikali ni makosa mtu kumlipa malipo mara mbili kwa ajili ya jambo hilohilo. Kwa hiyo, chakula hicho atakula akiwa nyumbani, kwenye mafunzo au akiwa popote. Hiyo ndiyo PGO inavyosema na ndiyo sheria ya nchi inavyosema. Sasa kama ni suala la huruma ya kwangu mimi Simbachawene ningesema tu kwamba walipwe lakini sasa ni sheria kwamba amepewa ration allowance ataila popote pale atakapokuwa.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ni juu ya kazi ya Jeshi la Polisi na lawama ambazo wamekuwa wakipewa. Nataka niwaambie ndugu zangu, ukiangalia katika takwimu na ukiangalia level ya uhalifu katika nchi yetu tuna nafuu kubwa sana. Leo katika hotuba yangu nimesema makosa ya usalama barabarani yamepungua kwa asilimia 36.4 na makosa ya jinai za kawaida yamepungua kwa asilimia 15.9. Hii maana yake ni kwamba vyombo hivi vinafanya kazi vizuri kwa kushirikiana na wadau wengine. Lawama za mtu mmoja- mmoja kwa tabia yake na hulka yake hizo haziwezi kuepukika zipo katika kila sekta. Hawa askari polisi ni binadamu, ni watoto wetu tuliowalea wenyewe na tunawajua wanavyofanana; tunawajua kwa sababu ni ndugu zetu, kwa hiyo, siyo kosa la mtu mmoja lifanye jeshi zima la polisi likawa halina maana.

Mheshimiwa Spika, hapa nichukue nafasi hii kuwapongeza sana Waheshimiwa Wabunge wote ambao kwa kweli mmesema sana juu ya hali za maisha ya vijana hawa wanaofanya kazi nzuri na kwamba zinatakiwa kuboreshwa pengine tutawatoa kwenye utendaji mbovu, mtu anaingia ana -stress, anakuja pale badala ya kum-arrest mtu vizuri anam-arrest vibaya kwa sababu yuko traumatized kiasi kwamba akili yake haiko vizuri. Kwa hiyo, tushirikiane kwa pamoja na mimi nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa michango yenu.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia kwa mfano, sisi Jeshi letu la Polisi limejitahidi sana kufanya kazi vizuri kwa kushirikiana na majeshi mengine na wadau wengine. Ukiangalia takwimu, kwa mfano, kuna namna ambayo unaweza uka-rate ukaangalia jinai ikoje na makosa yakoje, Kingereza wanasema incarceration rate. Incarceration rate ni pale unapohesabu katika population ya watu laki moja ni watu wangapi wako magerezani au wamezuiwa wanasubiri aidha kesi au wamehukumiwa.

Sasa ukiangalia Marekani incarceration rate ni 727, Kenya 81, Uganda 124, Brazil 193, Tanzania 59. Maana yake katika Watanzania laki moja wanaokuwa wamezuiwa magerezani ni wachache. Hii maana yake ni kwamba vyombo hivi vinafanya kazi nzuri na ndiyo namna pekee ya kuweza kutathmini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niwapongeze na niwashukuru Waheshimiwa Wabunge na nieleze kwamba kwa yale ya marekebisho waliyosema tutaendelea kuchukua hatua kwa wale ambao hawana uadilifu. Mambo yote yanafanyika kwa mujibu wa utaratibu, mtu anapokiuka taratibu kusema kweli tutachukua hatua kali. IGP hapa kila siku lazima kuna watu wanakuja ofisini kwangu kukata rufaa amewafukuza. Ukitaka kuwarudisha anakwambia haiwezekani huyu mimi najua hafai kuwa askari polisi. Ninyi wenyewe Wabunge ndiyo mnaonipigia simu Mheshimiwa Mbunge ndugu yangu amekuwa hivi, amekuwa hivi, huku tunakwenda kwa mujibu wa sheria na hili ni jeshi, huku ni discipline asilimia 100. Kwa hiyo, tutajitahidi na tutachukua hatua kuhakikisha tunakuwa na jeshi lenye weledi lakini lenye nidhamu pia.

Mheshimiwa Spika, limezungumziwa suala la ucheleweshaji wa malipo ya wastaafu na hapa ni kwa majeshi yote. Nataka niwaambie malipo ya wastaafu sasa hayachelewi sana, kama yanachelewa ni pamoja pia na malipo ya wastaafu wengine. Mimi nizungumzie ile ya kufungasha mizigo na kumrudisha askari aliyestaafu kwao; hii ilikuwa ina tatizo kwa muda wa miaka kadhaa, kwa kweli ilikuwa haijalipwa, lakini Mama yetu Mheshimiwa Rais Samia Hassan Suluhu alipoingia tu kama kuna document ya kwanza niliyompelekea ofisini kwake ilikuwa ni kumuomba fedha hizi na sasa ameruhusu na zimeanza kutoka. Uhamiaji wameshapata shilingi milioni 65, Polisi wamepata shilingi bilioni 3 na Magereza wamepata shilingi milioni 812, tumshukuru sana Mheshimiwa Rais. Sasa tutaanza kuwalipa wale wastaafu ambao walikuwa hawajapewa fedha zao kwa ajili ya kufungasha mizigo na kurudi nyumbani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lilizungumzwa jambo ambalo lilikuwa sensitive kidogo kwa sababu ni gender sensitive; suala la taulo za kike kwa askari na kwa wafungwa. Bado jambo hili si la kukurupuka na kulisemea kwa sababu tukisema kwa askari ambao wana mshahara na wana malipo mengine kama hizo allowance, ration allowance na vitu kadhaa, wataibuka na walimu hapa, watasema kwani sisi walimu wa kike hizi taulo na sisi vipi? Kwa hiyo, maeneo mengine na sekta nyingine wataibuka, lakini acha tulichukue kwa sababu ni jambo la gender kwa sababu pia kuna jeshi mojawapo hapahapa nchini linafanya hivyo. Tujiulize wenzetu wamefanyaje, wamechukua wapi, basi tutaelewana na tunaweza tukaja na suluhisho lakini ni muhimu zaidi kwa wafungwa magerezani. Kwa wafungwa magerezani hili nadhani tulichukue tuone namna tunavyoweza kuwashirikisha wadau kuweza kutatua tatizo hili kwa sababu wale hawana alternative means, wamefungiwa mle hawana njia, asiyekuwa na uwezo anafanyaje? Hili tunalichukua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ilizungumzwa juu ya Graduate Sergeant kufanya kozi ya graduate. Sergeant huyu kama ni graduate ukienda moja kwa moja ukawa Inspector umeruka sana. Zamani utaratibu ulikuwa ni huu uliorudi sasa wa kwamba lazima apitie kwenye Sergeant course ndiyo aende kwenye Inspector. Ukimaliza Sergeant course siyo mtu mdogo anaongoza askari 30. Kwa hiyo, mimi niseme tu utaratibu huu mpya acha tuuone unavyokwenda, lakini hata watakaokuwa na diploma wanaweza wakafanya hii Sergeant course kwa sababu majukumu yale hawezi kushindwa kubeba mtu mwenye diploma. Kama anaweza kubeba mwenye degree na mwenye diploma anaweza kubeba.

Mheshimiwa Spika, kwa harakaharaka nizungumzie suala la tozo za zimamoto, ukaguzi wa majanga ya moto na kutoa ithibati. Tozo hii ni kweli imelalamikiwa ni kubwa na Kamati ime-raise concern kubwa sana kwamba ukaguzi ukifanywa gharama zile ni kubwa. Tunafikiri na kwa sababu ni suala la Kanuni zilizo chini ya Waziri tutajaribu kuona, tupitie upya, tutashirikiana na Kamati yenyewe ili tuweze kuja na Kanuni rafiki ili tupanue na wigo wa watu wanaoweza kulipa. Hili hatuwezi kulifanya ndani ya mwaka huu, tulifanye kwa mwaka huu kwa ajili ya mwaka wa fedha unaokuja kwa sababu Kanuni za Fedha zinatukatalia.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine lililozungumzwa ni upekuzi magerezani. Upekuzi huu unafanyika kwa mujibu wa sheria. Kama kuna wanaofanya kinyume na sheria inavyotaka, wanafanya makosa na pale tutakapopata taarifa za malalamiko mahsusi tuna uwezo wa kuchukua hatua kwa wale waliofanya upekuzi huo.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine lililozungumzwa ni suala la Uhamiaji. Uhamiaji na hasa mipakani ambapo wamelalamika sana, niseme tu hata inapozungumzwa habari ya Kitambulisho cha Taifa cha NIDA unaweza ukapata kitambulisho lakini bado ukawa…

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, Waziri anapoongea hapa ni elimu kubwa sana kwenu ambayo itawasaidia hata ninyi kufafanua baadhi ya mambo kwa wananchi. Sasa mtu unakuwa uko hapa hapa unapiga story wakati yanatolewa majibu ambayo ndiyo kero za wananchi, ni vizuri sana mkakaa mkasikiliza. (Makofi)

Mheshimiwa Waziri, endelea.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, wamesema kwamba maeneo ya mipakani kuna ubaguzi, wanahojiwa waseme nne, waimbe wimbo wa Taifa; hizi ni technique tu za kutaka kujua huyu ni nani na huyu ni nani. Kama walivyosema Waheshimiwa Wabunge wa mikoa ya mipakani tunafahamu kwamba wakati mwingine kati ya nchi hii na nchi hii kutofautisha ni kitu kigumu sana, lakini ni kautaratibu tu fulani siyo conclusively kwamba kenyewe anatosha kuweza kumtia mtu hatiani. Kinachofanyika ni zaidi ya hapo, tunataka kujua pia umezaliwa wapi, wazazi wako walikuwa wapi, hayo tumekuwa tukifanya na ndio kazi ya Idara ya Uhamiaji. Tukifanya hivyo tunagundua kabisa, mtu mwingine anakwambia mimi mama yangu alifia hapa lakini tukienda nchi ya pili tunaenda kukuta mpaka mama yake na kwao mpaka tunajua kila kitu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, haya tunayafanya kwa weledi mkubwa na Waheshimiwa Wabunge naomba mtuamini. Kwa sasa tunadhani pengine tukipata vitambulisho hivi vya Taifa ndiyo tumepata uraia wa Tanzania; uraia wa Tanzania una Sheria yake ya Uraia na unamchakato wake. Kitambulisho hiki ni procedure tu ya kuwatambua na vinatolewa hata kwa wakimbizi na wahamiaji wa kazi. Kwa hiyo, ukipata kitambulisho hiki siyo muarobaini kwamba wewe umeshamaliza sasa hutaulizwa, hapana! Utaulizwa na utanyang’anywa hata hicho kitambulisho kama umepewa tukigundua kwamba wewe siyo raia wa Tanzania kwa sababu ziko haki za Mtanzania na ziko pia haki za mtu anayeishi Tanzania ambaye siyo raia wa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, suala la NIDA. Kwa sasa tulikuwa tunamalizia vitambulisho vya first generation kwa maana ya ile backlog ya zamani. Ndiyo maana kasi yetu pamoja na kufunga mashine haijawa kubwa kwa sababu kwa sasa tunazalisha vitambulisho kama 32,000 kwa siku. Lengo letu lilikuwa ni kuzalisha vitambulisho 140,000 kwa siku endapo tungekuwa tunatumia vitambulisho vya second generation. Sasa vile vya first generation bado tulikuwa na backlog ya vitambulisho kama 4,500,000 (raw card) ambazo ni lazima tuzimalize, tusipozimaliza ile ni fedha tutapata hasara. Kwa hiyo, mtaona speed inasuasua lakini badaye tutatoa vitambulisho kwa speed kubwa.

Mheshimiwa Spika, mimi nina uhakika kwamba hadi Julai, August, backlog yote iliyokuwepo ya 25,000,000 tutakuwa tumemaliza kabisa. Kwa target ya 25,000,000 tumetoa vitambulisho 7,000,000, tuliokwishawatambua ni 18,000,000. Tuna uhakika kazi ya utambuzi kama imefanyika basi kazi ya kufyatua vitambulisho itafanyika kwa speed.

Mheshimiwa Spika, changamoto ni nyingi, ukitaka kununua wino mchakato wa manunuzi, ukitaka kununua raw card mchakato wa manunuzi, ukitaka kufanya sijui nini mchakato wa manunuzi. Kwa hiyo, michakato hii ya manunuzi ndiyo inayochelewesha mambo kwenda lakini sasa ndiyo sheria za nchi tutafanyaje? Hata hivyo, kwenye eneo hili nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba Julai na Agosti watu wote waliokuwa wamechukuliwa alama za vidole, wametambuliwa watakuwa wamepata vitambulisho vyao.

Mheshimiwa Spika, sasa ilielezwa hapa juu ya kadi mbovu 427,000 zilizokuwa zimeonekana wakati Mkaguzi wa Hesabu za Serikali alipopita kwenye Ofisi za NIDA. Kadi zile zilikuja mwanzo kabisa wakati NIDA haijaanza kuzalisha hata kitambulisho hata hiki kimoja. Walipoangalia specification wakaona haziendani na zilizokuwa zimeagizwa, kwa hiyo, mkandarasi akaambiwa kadi zako hizo hatuzitaki, tunazozitaka sisi ni hizi. Kwa hiyo, ilikuwa ni yeye juu yake kuja kuchukua kadi zake kwa sababu hatuzihitaji pale lakini kwa sababu sasa zimeshafutwa kwa mujibu wa sheria na tumeandikiana tayari hakukuwa na mawasiliano mazuri kati ya Ofisi ya CAG na Ofisi ya NIDA juu ya namna ambavyo zile kadi zilikuwa abandoned pale maana hazina specifications tunazozihitaji. Kwa hiyo, zinatakiwa hata kuteketezwa yaani hazihitajiki. Kwa hiyo, eneo hilo ndivyo ambavyo ninaweza kulisemea.

Mheshimiwa Spika, maeneo mengine ambayo yamesemwa ni yale ya jumla, kama nilivyosema tutajitahidi kuyafanyia kazi na kuhakikisha kwamba yote yaliyosemwa na Waheshimiwa Wabunge tunayazingatia. Vinginevyo nichukue nafasi hii kuwashukuru sana wachangiaji wote, nina vikaratasi hapa vina michango mingi sana lakini niseme tu tutazingatia yale waliyoshauri.

Mheshimiwa Spika, niongelee hili la mradi wa Dar City, zile nyumba za Kunduchi na Msasani ambapo Kamati pia na wenyewe walisema. Tulielewana na Kamati, tunamalizia mchakato wa mwisho ili negotiation kati ya yule mbia na Serikali uweze kumalizika kwa sababu pale ni kwamba mkataba ule unavunjika. Mnapovunja mkataba kunakuwa kuna mambo mengi, investment ile ilikuwa ya miaka 70, investment ile ilikuwa ya hela nyingi kwa hiyo, Wizara ya Fedha na Wizara yangu zinaendelea kushirikiana kuhakikisha kwamba tunamaliza mkataba ule bila Serikali kuingia kwenye kesi mbaya au kuvunja mkataba kwa kukiuka taratibu.

Mheshimiwa Spika, nimalizie kwa kukushukuru sana wewe na Waheshimiwa Wabunge wote. Nimshukuru Naibu Waziri wangu na Maafisa wote wa vikosi vyote ambao wanafanya kazi kwa karibu sana pamoja na mimi.

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja. (Makofi)