Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. Samweli Xaday Hhayuma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Awali ya yote, nichukue nafasi hii, kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa kuaminiwa. Pia niipongeze wizara nzima kwa kazi nzuri inayofanyika.

Mheshimiwa Spika, niongelee maeneo mawili, eneo la kwanza ni eneo la Vitambulisho vya Taifa. Hili suala limesemwa sana jimboni kwangu, wazee wananiuliza hivi tumechukuliwa alama za vidole, ilikuwa ni maonyesho tu, hivi vitambulisho mbona haviji? Kweli hivyo vitambulisho ni muhimu sana kwa ajili ya watu kufanya shughuli zao na kwa ajili ya kujitambulisha katika maeneo mbalimbali. Ukienda kwa watendaji kuomba barua, siku hizi katika maeneo mengine hizo barua za watendaji hazitambuliki, vitambulisho vile ni muhimu kwa watu kupata huduma na kufanya shughuli za kimaendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nijielekeze upande wa huduma hasa za Jeshi la Polisi. Nawapongeza kwa kazi nzuri inayofanyika, kazi ya kuhakikisha kwamba usalama na ulinzi wa raia na mali zao. Vijana wetu wanajituma sana na sisi ambao tunafanya siasa huwa tunatembea usiku na njiani tunaona jinsi wanavyopigwa na baridi, wanavumilia. Ninachoomba, ili wafanye kazi kwa moyo Wabunge wenzangu wamesema sana, tuangalie maslahi yao, wawe na furaha na kazi wanayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tukiangalia kwenye maslahi hasa na kwenye vifaa ambavyo wanavitumia kwa ajili ya kutenda kazi; magari na service za magari, kwa sababu wakati mwingine wanakuwa watumwa kwa viongozi wengine, Polisi katika Halmalshari hawana mafuta wanakwenda kuomba kwa Mkurugenzi. Wakati mwingine wana kazi ya kwenda kufanya au kwenda kukamata, mhalifu, yule aliyelalamika analazimika kuombwa mafuta. Sasa hapo haki inakuwa ngumu kutendeka. Naomba tuwatendee haki tuwape vitendea kazi ili wafanye kazi zao vizuri.

Mheshimiwa Spika, eneo linguine ni eneo la ulinzi shirikishi, Polisi Jamii. Hii inakwenda wakati mwingine inafifia, naomba eneo hilo tulikazie ili angalau sasa wananchi wakishiriki usalama unakuwa mzuri zaidi. Namie niombe ulinzi shirikishi au Polisi Jamii itanuliwe kidogo ifike kwenye upande wa kutekeleza Sheria hizi za Usalama Barabarani hasa inayowagusa vijana wetu wa bodaboda, ambao wengi wao wanaendesha vyombo vile bila mafunzo yaliyokamilika. Kumekuwa na utamaduni sasa kwa sababu anajua kabisa ana makosa, akisimamishwa hasimami anakimbia. Sasa Polisi wanachukua hatua za ziada za namna ya kuhakikisha wanaweza kuwakamata, wakati mwingine wanawachapa fimbo. Sasa ukifanya hivyo maana yake unahatarisha maisha ya yule anayeendesha, lakini na watumiaji wengine wa barabara.

Mheshimiwa Spika, ili kupunguza ajali ambazo zinaweza kuzuilika, naomba katika eneo hili, polisi jamii tuwatengenezee utaratibu mzuri, kwa sababu wana vikundi vyao vile vikundi tuviimarishe ili washirikiane vizuri na Jeshi la Polisi. Kwenye jimbo langu ukienda kimya kimya kama hawajui gari vijana wanaanza kukimbia, maana yake kidogo kuna ile sintofahamu, hilo eneo tukikaa nao, tukalirekebisha angalau tutawasaidia hao vijana kufanya shughuli zao kwa kufuata taratibu na sheria za nchi. Badala ya kuweka nguvu nyingi katika kuwakamata, wakiwa na vitambulisho vya uraia wanafahamika wote wanatoka maeneo gani, wana-register nzuri kwenye eneo lile, inakuwa rahisi kumfuata hata baada ya kuwa umeshajua kuwa kuna kijana huyo amekimbia. Unamfuta kwenye eneo ambalo anaishi hakuna sababu ya kukimbizana.

Mheshimiwa Spika, tuliongea sana na eneo pia la faini wanayopigwa vijana wa bodaboda, pikipiki zile sio zao, kwa siku mapato labda shilingi elfu nane, lakini akipatikana na kosa elfu thelathini. Anaanza kukimbizana na ndugu zake, hii kweli inawaumiza vijana, hatuwajengei uwezo wa kujikwamua kiuchumi. Tutafute namna ya kuwawezesha ili watekeleze sheria na wafanye shughuli zao vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niishie hapa kwa sababu najua kuna limitation ya muda, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)