Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia kwenye

hii hoja ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi. Nianze kwa kumpongeza Waziri na timu yake yote, Naibu Waziri na Watendaji katika Wizara hii kwa kazi nzuri na muhimu wanayoifanya.

Mheshimiwa Spika, Wizara hii ya Mambo ya Ndani ya Nchi ni nyeti na ukiangalia maslahi ya watenda kazi katika Wizara hii yanasikitisha na kutia huruma. Kwa mfano, katika Wilaya yangu ya Longido sisi ni wilaya ambayo karibu ina miaka 25 sasa tangu ianzishwe lakini hakuna Kituo cha Polisi cha Wilaya, kuna kituo kidogo kilichojengwa tangu enzi ya ukoloni na nyumba za maaskari pale ukiziangilia zinatia huruma. Naomba katika bajeti hii Waziri hebu aangalie kule Longido atatusaidiaje.

Mheshimiwa Spika, lakini pia ukienda Kwamwanga kuna Kituo cha Polisi ambacho zamani kilikuwa barabarani, barabara ya lami ikafika pale kutoka Rombo, wananchi wakajiongeza wakajenga kituo kingine pembezoni, imebakia finishing tu. Waziri aliyepita nilishamuomba angetuchangia tu kama milioni 20 tunafanya finishing nzuri.

Mheshimiwa Spika, pia maaskari pale wanalala nje, ukiona nyumba wanazolala zinatia huruma. Naomba sana pia katika bajeti hii hebu muangalie hali ya usalama katika Wilaya ya Longido inayopakana na nchi ya jirani yenye kilometa zaidi ya 350.

Mheshimiwa Spika, lakini pia tulishahamisha wananchi kwa sababu alisema kwenye hotuba yake kwamba na sisi tunaweza tukachangia ili tupate vituo vingine zaidi vya polisi, tumefanya hivyo. Kule Mndala tumeanzisha kituo, Serikali haiweki hata mkono. Tarafa ya Kitumbene yenye vijiji zaidi ya 19 tulishapendekeza tuwe na kituo lakini hamna juhudi yoyote ya Serikali katika kuhakikisha kwamba tuna vituo hivyo vya polisi.

Mheshimiwa Spika, naomba suala hili la miundombinu ya polisi kuwafanya wafanye kazi katika mazingira rafiki na makazi yao lizingatiwe sana nchi nzima lakini katika Wilaya yangu ya Longido basi nilisemee maana ndiyo nyumbani kwamba kwa kweli hali ni mbaya, hata ya magari ni mbaya. Kila wakati mimi kama Mbunge ndiyo nachangia tairi, matengenezo ya gari na unakuta kuna magari mengine yamekaa juu ya mawe kwa sababu hamna bajeti inayotolewa kutoka Wizarani kusaidia uendeshaji wa operesheni za polisi katika wilaya yangu. Hata Zimamoto lakini ni jina tu, hawana hata gari ya kukimbia kwenye matukio yakitokea kwenda kushuhudia licha ya gari ya kuzima moto unapotokea mahali popote. Naomba haya masuala yazingatiwe.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu dakika ni chache naomba nijielekeze kwenye suala la wafungwa na mahabusu. Tunashida kubwa sana na sijui Wizara ya Mambo ya Ndani itatusaidiaje. Kuna kikosi kinachodhibiti ujangili wa nyara za Serikali kinachofanya kazi katika wilaya hizi zenye wanyamapori, kuna vitendo viovu vinafanyika. Naomba tu nimjulishe Waziri na ajue namna ya kufanya kwa sababu ndiyo wanaolinda mali na raia wa nchi yetu kwamba watuhumiwa wanapokamatwa kuna mazingira ya rushwa na kuna mahabusu wanaokaa magerezani mpaka miaka mitano hawahukumiwi.

Mheshimiwa Spika, naomba nitoe mfano, kuna mtu anaitwa Taraiya Paulo alikamatwa kwa sababu tu kwenye simu yake alikutwa amefanya mawaliano na mtu ambaye anafanya biashara ya ujangili lakini alikuwa anamfuata kwa deni lake la mbuzi aliyomuuzia. Akakaa mahabusu miaka mitatu, ametoka juzi tu ndiyo anaeleza kwamba yeye alikamatwa kwa sababu simu yake imekutwa na mawasiliano ya mtuhumiwa.

Mheshimiwa Spika, kuna mwingine anaitwa Luka Olokwen, yeye alikamatwa na mguu wa swala ambaye ameliwa na chui akabakiza, kwa sababu sisi jamii ya kifugaji hatuli nyama pori akabeba ule mguu ampelekee mbwa wake nyumbani, akakamatwa akaambiwa usipotoa milioni tano hatukuachii. Familia ikauza tena walewale ng’ombe aliokuwa anachunga akalipiwa milioni tano baada ya mwaka mmoja amekuja amechukuliwa juzi amefungwa miaka 20, kwa sababu tu alikutwa na mguu wa swala aliyeliwa na mnyama pori. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna mwingine anaitwa Daniel Saitot, yeye alikamatwa tangu tarehe 1/9/2018. Kesi yake haijasikilizwa mpaka leo, alikutwa sijui ana ngozi ya chui. Hiyo ni kusema kwamba hebu Wizara hii ya Mambo ya Ndani iangalie mazingira ya kusaidia raia wa Tanzania wasio na hatia wanaopewa kesi mbalimbali za uhujumu uchumi. Sambamba na hilo, mimi naomba hizi kesi za uhujumu uchumi ziwekwe kwa category, ziwekwe ambazo zinadhaminika watu wadhaminiwe waendelee na kesi zao wakiwa majumbani ili kupunguza msongamano katika magereza yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la mwisho, kuna hili suala la uhamiaji, kipengele kinachotukera kidogo sisi watu wa mipakani ni ile hati ya kusafiria ya Single Entry Permit. Mtu ana shida kubwa labda anamuuguza mgonjwa yupo Nairobi anahitaji kwenda kila wiki anadaiwa akate hiyo permit kila wiki. Naomba passport za muda mrefu zitengenezwe na kuwa zinapatikana pale pale mpakani kuwaondolea raia wetu adha ya kulazimika kununua passport mpya ya muda wa dharura kila wakati wanapohitaji kusafiri.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)