Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Madini

Hon. Christopher Olonyokie Ole-Sendeka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Simanjiro

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Madini

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi ya kwanza kukushukuru wewe mwenye kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia bajeti hii ya Wizara ya Madini.

Mheshimiwa Spika, niende moja kwa moja kwenye eneo linalonihusu la madini ya vito. Lakini kabla ya kufika huko niseme, waswahili wanasema mnyonge mnyongeni lakini haki yake mpeni, kwa muda mfupi niliokaa kwenye Bunge hili baada ya kurudi juzi Waziri Biteko amefika katika eneo la Mererani kama mara tatu hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na nilimnong’onezea juu ya kero zinazowakabili wachimbani wa madini ya vito aina ya Tanzanite pale Mererani. Kwa wale wasiofahamu wachimbaji wapatao kati ya 8,000 au 10,000 wanaingia na kutoka katika eneo la machimbo ya Mererani; 8000 – 10000 kwa siku. Nilimuomba Mheshimiwa Waziri asaidie kujenga shade ambayo ingeweza kusaidia wachimbaji wale kujikinga wakati wa mvua na wakati wa jua. Mheshimiwa Biteko alichukua uamuzi palepale na kutoa maelekezo na tatizo hilo sasa linakaribia kufika ukingoni maana jengo hilo linajengwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilimuomba Mheshimiwa Waziri aweke utaratibu rafiki unaoweza kuwasaidia wachimbaji wadogo na hasa wale wakipato cha chini kuweza kumudu kuendesha biashara katika eneo la uzio wa Mererani, nilipata majibu positive na alitoa maelekezo ambayo ni rafiki na wachimbaji walimpongeza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilimuomba sana Mheshimiwa Waziri aliondoshe janga lililokuwa mbele yetu kitendo cha… natafuta lugha ya staha; kitendo cha fedheha cha ukaguzi usio na staha, wanaofanyiwa wachimbaji wa madini ya Tanzanite Mererani ambapo watu wapato 20 au 15 wa rika mbalimbali wanapotoka kwenye uchimbaji wakifika kwenye gate kuna vyumba viwili vya ukaguzi, kimoja cha wanawake na kimoja cha wanaume. Wanaume zaidi ya 20 au 15 kwa wakati mwingine; wanawekwa kwenye chumba hicho na kuvuliwa nguo zote, zote; na katika chumba cha wanawake vivyo hivyo, wanaingia kwenye chumba hicho bila kujali rika, bila kujali nini wanavuliwa nguo zao zote na wanaambiwa waruke kichura kidogo kitendo ambacho ni cha aibu. Haitarajiwi kwa Taifa kama letu ambalo linatambua na kuthamini misingi ya utu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini cha kustaajabisha zaidi, Mheshimiwa Waziri alitoa kauli mbele ya wachimbaji wadogo na mbele yangu kwamba jambo hili likome sasa na ukaguzi wa staha ufanyike. Alisema hivyo katika ziara yake ya kwanza, akarudia mbele ya Kamati ya Madini, baada yake siku iliyofuata ikaja Kamati inayoshughulika na masuala ya Ulinzi na Waziri wa Ulinzi ambaye ndiye anayeshughulikia mambo ya ulinzi wa madini pale getini.

Mheshimiwa Spika, ninapata mashaka, kwasababu Serikali haikuongea lugha moja, Wizara hizi mbili hazikuongea lugha moja na juzi tumefanya kikao cha pamoja kati ya Wizara ya Ulinzi, Wizara ya Madini, Wizara ya Fedha, Wizara ya Nishati kwa pamoja kujadili masuala ya Mererani. Kinachoshangaza hata baada ya ombi langu mbele ya Kamati hizo mbili ya Nishati la Kamati ya Ulinzi; hata jana na leo asubuhi ukaguzi unaoendelea ni ule ule, walichotofautisha ni kwamba wamiliki wa migodi na mameneja wa migodi wamepewa mlango wao wa kutokea na kwamba hawavuliwi nguo hao. Lakini wale maelfu wengine waliobaki wanaendelea na kitendo hicho cha fedheha.

Mheshimiwa Spika, waislam wanasema; “ukiliona jambo ovu liondoshe, kama huwezi kuliondosha lishtakie kwa mwenye uwezo kuliondosha na asipoliondosha endelea kulinyooshea kidole mpaka atakapopita mtu wa kuliondosha.” (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hili ni jambo ovu, ni jambo ambao halijarajiwi litendeke hasa na Serikali ya chama changu Serikali ya CCM. Ninataka maelezo ya Mheshimiwa Waziri leo, kauli ya Serikali itolewe na kwasababu kuna kujikanganya kati ya Waziri wa Ulinzi na Waziri wa Madini. Waziri wa Madini yupo clear kwenye jambo hili, Waziri wa Ulinzi anapata kigugumizi, Waziri Mkuu atoe kauli juu ya jambo hili, kama Tanzania tumefika mahali ambapo Watanzania wanavuliwa nguo hadharani na kukaguliwa na watoto ambao wanaweza kuwazaa…

SPIKA: Mheshimiwa Ole-Sendeka nilitaka tu kukuhakikishia kwamba Waziri wa Ulinzi yupo.

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana napokea maelekezo yako mkuu.

Mheshimiwa Spika, ninachotaka ni kwamba atoe kauli yeye vinginevyo ushauri wangu utakuwa ni vizuri kila mtu aonje fedheha hii. Tulikataa wakati wa Azimio la Arusha tukasema tumeonewa kiasi cha kutosha, tumenyonywa kiasi cha kutosha, tumepuuzwa kiasi cha kutosha, unyonge wetu ndio uliotupelekea tuonewe, tunyanyaswe na tupuuzwe, sasa tunataka mapinduzi, mapinduzi yatakayotupelekea tusionewe tena, tusipuuzwe tena, tusinyonywe tena. Azimio la Arusha mwaka 1967 na tukaweka kwenye utangulizi wa Mwongozo wa TANU wa mwaka 1971. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tamko letu ni la mwaka 1967, kama mnadhani kitendo hiki ni kizuri na mnadhani watendewe watu wa Mererani onesheni demo, ninyi ambao mmepewa dhamana Mawaziri na Makatibu Wakuu tafuteni chumba cha wanaume peke yenu, bila kujali….(Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Ole-Sendeka, hiyo hairuhusiwa Bungeni kuwashauri Mawaziri waende wakaruke kichura. Aaah dakika zako zimekwisha Mheshimiwa.