Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Madini

Hon. Bupe Nelson Mwakang'ata

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Madini

MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia katika Wizara hii ya Madini. Kwanza kabisa nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kutujalia uzima, sisi sote tukawepo hapa Bungeni tukijadili mambo muhimu.

Mheshimiwa Spika, awali ya yote nichukue nafasi hii kutambua mchango wa Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, lakini nimpongeze Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu, Mama Samia Suluhu kwa kazi kubwa, lakini pia kwa Hotuba yake nzuri iliyowafuta machozi Watanzania kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi hii pia kumpongeza Waziri kijana Mheshimiwa Doto Biteko na Naibu wake, kwa kweli wameitendea haki wizara hii, wameituliza kiasi kikubwa wameweza kuongeza mapato kwenye wizara hii, kwa kweli mnafanya vizuri mheshimiwa Doto Biteko endelea na moyo huo Mwenyezi Mungu aendelee kukupigania. Mnyonge mnyongeni haki yake mpeni Mheshimiwa Doto Biteko amefanya vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Sasa niingie kwenye hoja zangu za msingi kwasababu ya muda. Mkoa wetu wa Rukwa kuna utajiri mkubwa sana, utajiri wa helium. Helium gas inapatikana Rukwa, ipo kwa wingi sana, lakini Serikali haijawa serious sana kwenye jambo hili. Natoa ushauri, kwamba Serikali ihakikishe kwamba sasa inatafuta wawekezaji wakubwa ambao wanajiamini na wako serious kwenye jambo hili. Kwa sababu utajiri tunao mkubwa sana wa hiyo helium ni utajiri kwa Taifa lakini utajiri kwa Mkoa wa Rukwa kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kupata wawekezaji hao, tutaomba sisi kama wawakilishi wa Mkoa wa Rukwa tuweze kupata taarifa kwasababu sasa hivi tumesikia kuna wawekezaji ambao wamepatikana lakini hakuna taarifa ambazo tunazijua, tunazisikia sikia tu tunaomba Serikali sasa iwe inakuwa wazi. Kwanza kabisa iweze kuweka sheria ambayo itawabana wawekezaji wetu waweze kuwasaidia wananchi wa eneo husika. Wawekezaji wakipata fursa kama hizo wamekuwa wakisaidia vitu vidogo vidogo hasa utakuta amesaidia shule, amesaidia zahanati lakini utakuta mradi wenyewe ambao anaoupata pale ni mradi wa fedha nyingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nilikuwa naiomba Serikali iangalie hawa wawekezaji wawe wanasaidia wananchi wa eneo husika kwa kiasi kukubwa sana kulingana na mapato yao ya mradi husika. kwa mfano kama hao wawekezaji watakaokuja kuwekeza kwenye helium tunaomba sana wawaangalie sana wale watu, wananchi wanaokaa kwenye maeneo husika kuwasaidia kwa kuwapa aidha, hizo shule lakini shule za maana, sio inajengwa shule tu ili mradi shule imejengwa lakini shule haina ubora wowote. Lakini pia Serikali iweze kuwapa elimu, elimu wananchi wa eneo husika faida za mradi lakini pia na hasara za mradi huo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia kwenye Mkoa wetu wa Rukwa, kwasababu kuna miradi mikubwa kama hiyo tunaomba basi Serikali ikumbuke kuujenga ule uwanja wa Ndege yaani miundombinu ikae vizuri. Lakini pia barabara, barabara ni changamoto kubwa sana kwenda kufika miradi kama hiyo kwa mfano; mradi huo uko kwenye Ziwa Rukwa. Kule upande wa Ziwa Rukwa barabara ni mbaya sana, sasa tulikuwa tunaomba Serikali iangalie sana miundombinu ya Mkoa wa Rukwa ikiwemo uwanja wa Ndege lakini pia ikiwemo barabara ambazo zinakwenda kwenye mradi huo.

Mheshimiwa Spika, nihame kwenye eneo hilo sasa, niongelee sasa upande wa dhahabu. Kama nilivyompongeza waziri kwamba amefanya vizuri tunaomba sasa kama alivyotoa tamko mama yetu Rais wetu Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan kwamba yale maeneo ya hifadhi waachiwe wananchi waendelee kuchimba lakini kujipatia kipato kwenye maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika ni muhimu sana, Waziri Doto Biteko alifanyie kazi haraka iwezekanavyo suala hili ili sasa waraka utoke wananchi waweze kufaidika na maeneo hayo kwa kupata waraka maana toka alivyotoa tamko hilo mama, wananchi wamekuwa wakiingia kwenye maeneo hayo sasa watumishi wa wizara husika au watumishi wa idara husika wamekuwa wakiwapa adhabu kubwa sana wananchi wanaoingia kwenye hifadhi kujipatia kipato. Kwa hiyo, nilikuwa naishauri sana Serikali ifanye haraka sana kutoa waraka kwenye haya maeneo ya hifadhi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Lakini lingine ni hawa watu wa TRA wana wa-harass sana wachimbaji wadogo wadogo. Mchimbaji akionekana tayari ana vitu vya kuchimbia basi wana mkadiria mapato kwa wingi bila kujali kwamba amepata dhahabu kiasi gani au bila kujali kwamba kiasi alichopeleka pale kwenda kupima kinafanana na hizo tozo ambazo wamamtoa.

Suala lingine ni ucheleweshaji wa leseni, leseni za wachimbaji zinachelewa sana utakuta mchimbaji ameomba sehemu ya kuchimba lakini kupata leseni imekuwa ni changamoto. Lakini hilo pia suala hilo Mheshimiwa Waziri aliangalie sana leseni ziwe zinawahi kutoka mchimbaji mdogo akiomba leseni basi apatiwe kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, suala lingine nilikuwa naomba wale wachimbaji wakubwa ambao wana maeneo makubwa

SPIKA: Malizia Mheshimiwa Bupe Mwakang’ata.

MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Spika, ambao wana maeneo makubwa, kwa kumalizia. Yale maeneo ambayo hawayatumii wawagawie wachimbaji wadogo wadogo kwasababu mchimbaji mkubwa ana eneo kubwa halitumii. Lakini mchimbaji mdogo anahangaika pa kuchimba wakati maeneo yamekaa bure. (Makofi)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Wawe wanachukua wanawagawia wachimbaji wadogo wadogo. Ahsante sana, nakushukuru sana. (Makofi)