Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Madini

Hon. Nicodemas Henry Maganga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Madini

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia Bajeti ya Madini. Naomba nianze kwa kumpongeza Waziri wa Madini kaka yangu Dotto Biteko, kutoka bilioni 168 mpaka bilioni 528 makusanyo hongera sana kaka. Pamoja na kumpongeza naomba niweke changamoto, lazima tufikirie kwamba ni kwa nini mwanzoni tulikuwa tunakusanya pesa kidogo na sasa hivi tunakusanya bilioni 528, ni jambo la kufikiria. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa watu wetu kuna malalamiko makubwa, hasa wachimbaji wadogo. Mimi natokea Jimbo la wachimbaji, Mbogwe. Juzi nimefanya mikutano mitatu kwenye Jimbo langu malalamiko ni makubwa sana. Naomba niishauri Serikali, Mama Samia, Rais wetu, najua maeneo yote yenye uzalishaji wa madini, migogoro ni mahali pake na mimi kwangu nikiri wazi kabisa kuna mgogoro ambao ni mkubwa sana ambao unaninyima sana raha ni wa pale Mbogwe Nyakafuru. Kuna kikundi kinaitwa Isanjabadugu, nashukuru kaka yangu Mheshimiwa Dotto ameniahidi baada ya Mei Mosi tutaenda kutatua huo mgogoro. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wale wananchi wana haki, kama nilivyoeleza kwenye mkutano wa tarehe 27 Februari, kwa Mheshimiwa Rais, Marehemu Magufuli, wale wananchi mashamba yale ni ya kwao, lakini mzungu aliingia kwa kutafiti ikabidi sasa, baadhi ya watendaji wa Serikali wachache waingilie kati, zikafunguliwa kesi mahakamani. Uzuri wananchi wangu wameshinda zile kesi na wana nakala za hukumu, wanatakiwa wakabidhiwe mashamba yao ili waendelee kupokea ile asilimia 10. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, namwomba kaka yangu Mheshimiwa Dotto anisaidie sana kwenye Jimbo langu la Mbogwe, maana wananchi wale machozi yao yatatufata siku tukifa, maana wanalia mpaka sasa hivi hawapati chochote wakati mashamba ni ya kwao.

Mheshimiwa Spika, vile vile, nimpongeze Mheshimiwa Rais kwenye upande wa TRA aliishauri vizuri sana, lakini sekta nyingine ambayo ni ngumu ni hii ya madini. Nilikuwa mfanyabiashara wa madini sasa hivi nimeacha kabisa. Nilichukua mkopo hapa milioni kama 500 na sheria za madini ni mbaya sana, yaani pesa yako ukiichukua tu ukanunua makinikia, wanatoza tozo yaani bila kuangalia mtaji kwamba, umeingiza pesa kiasi gani, wao wanaangalia kulipa tu kodi, ndio maana makusanyo yamepanda namna hii. (Makofi/ Kicheko)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba tuangalie vizuri huku tukiangalia na wananchi wetu. Kwenye Hotuba yake Mheshimiwa Waziri amesema atawasaidia wachimbaji wadogo na naomba ufafanuzi pale, atawasaidia kwa kuwapa pesa ama kuwapunguzia changamoto zilizoko vijijini? Maana kuna Kamati ya Ulinzi na Usalama pale unapochimba tu duara ukapata mifuko kwa mfano, kumi, ile Kamati ya Ulinzi na Usalama inachukua mifuko miwili halafu watu wanajiita sijui nani nani? Serikali ya Kijiji, mifuko miwili, ukiangalia mtu huyu anayepewa leseni naye anachukua mifuko mitano, kwa hiyo, mchimbaji anakutwa anabaki na mifuko 10, malalamiko ni makubwa sana kwa wachimbaji wadogo. Migodi ya Nyakafuru, Mwakitorio, Geita na Mabomba, ukikaa na wachimbaji wanailalamikia sana Serikali kwa hizi tuzo. Kwa hiyo, Waziri pamoja na Mheshimiwa Rais wafanye juu chini kuhakikisha kwamba, wananchi hawa wanyonge, maana sera ya Chama cha Mapinduzi tulikuwa tukinadi majukwaani kwamba tutawajali sana wanyonge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wanyonge hawana haki kwenye Taifa hili hawa wachimbaji wadogo. Sana sana labda, naona yanasaidiwa mashirika yale makubwa STAMICO pamoja na mashirika mengine yaliyoyoendelea na wazungu. Hata hivyo, hotuba ya Mheshimiwa Rais ilizungumza kwamba, hata sisi Wabunge tuwe mabilionea, kwa hiyo, hatuwezi kuwa mabilionea hata siku moja, kama umeingiza pesa milioni 100 hujapata hata faida, lakini ukikutana na Afisa Madini unaambiwa ulipe milioni saba hujapata hata faida. Mimi ni mfanyabiashara na nina watumishi wazuri tu tunafanya hesabu wakati ule tunapoenda kulipa mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukiingia Wizara ya Madini hicho hakipo. Wanaangalia tu umeuza shilingi ngapi wanatoa lolaite (loyalty), wanatoa service levy, pamoja na michakato mingine ambayo haieleweki, haina vichwa wala miguu. Kwa hiyo, tunaweza tukajisifu sana kwamba tumekusanya sana…

SPIKA: Sasa wewe mtani mbona sasa unaongea Kisukuma kwenye mchango wako? (Makofi/Kicheko)

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante mimi si nilikuambia ni Msukuma. (Makofi/Kicheko)

SPIKA: Sasa hiyo lolaite ndio nini hiyo? (Makofi/ Kicheko)

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Spika, nini? lolaite? (Makofi/Kicheko)

SPIKA: Haya Mheshimiwa, endelea kuchangia. (Kicheko)

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Spika, bado dakika tatu.

Mheshimiwa Spika, namwomba Mheshimiwa Waziri pamoja na kwamba tunaiingizia Serikali pato kubwa na sisi tuangalie wale tunaotoka kwenye maeneo ya hii migodi inayoingiza. Maana hatuna barabara, hatuna afya, yaani wananchi wetu wana shida. Huwezi ukalinganisha na kwamba tumeingiza kwenye pato la Taifa bilioni 528, wakati hatuna chochote tunachopata katika pato la Taifa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimwombe Mheshimiwa Rais pamoja na wahusika wote watuangalie kwa macho mawili, hii migodi inayotoa dhahabu kwa wingi Geita, hasa Mkoa wa Geita na Shinyanga… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)