Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Madini

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Madini

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa hii fursa ya kuchangia Wizara ya Madini ambayo ni Wizara muhimu sana kwenye Uchumi wa Tanzania. Nianze kwanza kwa kumpongeza Waziri na timu yake, kwa kweli wamefanya kazi nzuri sana na kazi imeonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia hata kwenye taarifa yake, pato letu mchango wa madini ulianzia 4%, 2014, lakini kwa sasa hivi unaelekea kwenye 6% na nina imani kabisa kuwa katika hiyo appetite yao ya kufikia asilimia 10 itawezekana kabisa. Kwa hiyo, namshukuru sana tena sana Mheshimiwa Waziri kwa kazi yako nzuri na Wizara kwa jinsi mnavyofanya kazi vizuri, coordination imekuwa ni nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, madini kwa kiasi kikubwa duniani kote yanaweza kutumika kama rasilimali kwenye viwanda. Nasi Tanzania tumebahatika kupata madini mengi ambayo yanaweza kutumika viwandani. Kipindi hiki wakati uchumi wa dunia unayumba yumba sisi Tanzania tuna fursa ambazo zipo kupitia madini kama ilivyokuwa kwenye kilimo ambayo tunaweza kutumia madini yetu kupata hizo fursa za kuanzisha viwanda vingi kama hivi vilivyoanzishwa vya dhahabu ambavyo vimeanza kufanya kazi nzuri sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nilikuwa napendekeza na nimekuwa nikipendekeza mara nyingi, tuna madini ambayo ni adimu sana duniani na ni adimu sana Afrika. Tuna mgodi wa madini Panda Hill Songwe Wilaya ya Mbeya. Huu mgodi utazalisha Niobium na huu mgodi kuna fursa ya kuanzisha kiwanda ambacho kitakuwa ni cha kipekee cha kwanza Afrika nzima; na cha nne duniani. Kuna uwekezaji wa kutoka nje wa dola zisizo pungua milioni 200, vile vile kitazalisha kwa mwaka Dola zisizopungua milioni 200 na Serikali itapata mapato yasiyopungua Dola milioni 50 kwa mwaka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ukiangalia kwa haraka haraka inawezekana hizi projections zikaonekana kama ni za ajabu, lakini hiyo ndiyo hali halisi. Kwa sababu kazi zote zimefanyika za namna gani waweze kuendesha huo mgodi na hicho kiwanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ushauri wangu kwa Mheshimiwa Waziri na Serikali, hivi viwanda vya aina hii tungevipa kipaumbele hasa katika kipindi hiki ambacho tunahitaji sana pesa za kigeni hasa katika hiki kipindi ambacho tunahitaji ajira. Kwa sababu hiki kiwanda wakati wa ujenzi kitazalisha ajira zisizopungua 2,000, lakini mbele ya safari kitakuwa na ajira za kudumu siyo chini ya 600. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli wakati mwingine tunakuwa tunalala na fursa tulizonazo na hili ndiyo tatizo ambalo tunakuwa nalo. Kwa sababu kama hiki kiwanda kikiwepo cha kwanza Afrika ina maana madini ya namna hiyo yanayozalishwa nchi nyingine duniani, siyo Afrika peke yake yataletwa Tanzania kama rasilimali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, haya madini ya Niobium, hiyo product watakayozalisha inaitwa ferroniobium, ambayo ndiyo sasa hivi inatumika kutengeneza vyuma ambavyo vitasaidia kwenye ujenzi wa reli na madaraja kwa vile ndiyo vyuma vya kisasa ambavyo ni vyepesi na vinatumika hata kwenye madaraja ya kwenye maji na hata baharini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba labda kwa kipekee Wizara ya Madini pamoja na Wizara ya Uwekezaji na Viwanda wangejaribu kuliangalia kwa pamoja na nina imani Mheshimiwa Waziri yupo vizuri sana katika kusimamia sheria na mikakati yake ya kulinda rasilimali za Taifa Letu. Nina imani kwa kuzingatia hayo, tukiangalia vile vile katika win win situation tutaona namna gani nchi yetu inaongeza mapato kupitia haya madini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli Mheshimiwa Waziri yeye mwenyewe ni shuhuda, alishafika kwenye huo mgodi, aliutembelea na wawekezaji wamekuja mara nyingi kuonana nao. Nafikiri katika hatua tuliyofikia leo, anaweza kuangalia ni namna gani nchi yetu inaweza kuongeza pato la Taifa na vile vile fedha za kigeni ili tuweze kuimarisha uchumi wetu na ili tufikie lengo letu la pato la Taifa ambalo linachangiwa na madini kufikia asilimia kumi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja, nashukuru sana. (Makofi)