Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Maftaha Abdallah Nachuma

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Mtwara Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. MAFTAHA A. NACHUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii ya kuweza kuchangia hoja iliyopo Mezani leo hii ya Viwanda, Uwekezaji na Biashara.
Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijaanza kusema lolote, naomba nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunibariki kuwa na afya njema. Kwa kuwa katika kuchangia Wizara hizi, hii ni mara yangu ya kwanza nitumie fursa hii pia kuwashukuru wananchi wangu wa Jimbo la Mtwara Mjini na niwaeleze kwamba naendelea kupambana vizuri na nitawawakilisha vyema kwa kipindi chote cha miaka mitano. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna hotuba hii ambayo imetolewa na Mheshimiwa Waziri wa Viwanda na Biashara, nianze tu kwa kusema kwamba mkakati wa Wizara hii wa kuhakikisha kwamba nchi ya Tanzania inakuwa ni nchi yenye uchumi wa viwanda kupitia bajeti yake hii, kimkakati ni jambo zuri sana. Wenzetu nchi nyingi duniani, ukisoma historia, nchi za Ulaya ziliweza kuendelea kwa kiasi kikubwa kupitia sekta hii ya viwanda. Tangu karne ya 15 kule nchi zote za Ulaya ziliweza kufanya mapinduzi ya viwanda na kuweza kuondoa umaskini na hata kuitawala dunia kwa kutegemea sekta hii ya viwanda.
Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu ya Tanzania, baada ya uhuru, Mwalimu Julis K. Nyerere alijitahidi kwa kiasi kikubwa sana, aliweza kuanzisha viwanda vingi sana. Wakati huo ikumbukwe kwamba tulikuwa katika mfumo wa ujamaa na kujitegemea, uchumi wetu ulitegemea kwa kiasi kikubwa sekta hii ya viwanda, lakini kwa bahati mbaya kabisa, Serikali ya Chama cha Mapinduzi mwaka 1995-1996 iliweza kuingia katika mfumo wa uwekezaji, mfumo ambao haukufuata kanuni, sheria na taratibu za kiuwekezaji na hatimaye zaidi ya viwanda 446 viliweza kuuawa kwa kupewa wawekezaji ambao hawana sifa ya kuwekeza Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumze tu angalau kwa kifupi sababu zilizopelekea kuuawa kwa viwanda ikiwa ni kwamba tuliwapa wawekezaji ambao they were not credible buyers katika nchi yetu ya Tanzania, walikuwa hawana uwezo na ujuzi. Jambo lingine lilikuwa ni mazingira yenyewe ambayo tuliyatengeneza hayakuwa rafiki kwa kuweza kuuza viwanda vyetu. Mwisho wa siku leo hii tunasema tunahitaji kufufua uchumi wa viwanda, wakati hatuna utaratibu, hatuna mkakati wowote ili Taifa kama Taifa liweze kuwekeza katika sekta hii ya viwanda kwa kuwapata wawekezaji ambao tunasema ni credible buyers. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Waziri wa Viwanda, Uwekezaji na Biashara amewasilisha bajeti yake hapa lakini nimepitia hii bajeti takribani kitabu chote hiki sijaona hata sehemu moja ambapo ameeleza ni utaratibu gani ambao utatumika katika kuhakikisha kwamba uwekezaji wa ndani ya nchi unakuwa ni uwekezaji wenye tija. Ameeleza tu kwamba tutahakikisha kwamba wawekezaji wa ndani na viwanda vidogo wanapewa kipaumbele lakini sijaona utaratibu wowote ambao wameuweka.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, nizungumzie suala zima hili la mashirika ya umma na hasa mashirika ya hifadhi za jamii. Kuna mashirika ambayo yana mkakati wa kuwekeza ndani ya nchi lakini katika uwekezaji wao wanatumia mamilioni ya fedha kinyume na utaratibu. Wizara kama Wizara sijaona mkakati wowote ambao wameueleza ni namna gani watadhibiti mashirika haya kutumia fedha za umma hovyo hovyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, Shirika la GEPF wakati tunapitia mpango wao ule wa uwekezaji katika Kamati ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma unaweza ukashangaa kuona kwamba wameweka mkakati wamenunua viwanja kwa mfano kule Mtwara wamenunua square meter moja kwa shilingi laki moja na elfu arobaini na nne na something, ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kiwanja hiki sijui wamenunua mbinguni au wamenunua wapi, ni uwekezaji ambao hauna tija. Nazungumzia suala hili la uwekezaji kwamba lazima kama Wizara wahakikishe kwamba wanaweka mechanism iliyokuwa bora kabisa ili waweze kuhimiza uwekezaji wenye tija na Taifa letu liweze kuwa na manufaa.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia pia kuna kiwanja kimenunuliwa Mwanza ambapo GEPF wanaenda kujenga shopping mall lakini ukiangalia square meter moja wamenunua shilingi laki moja na elfu kumi na tano kana kwamba hicho kiwanja kina dhahabu. Hapa nazungumzia suala zima la uwekezaji wenye tija kwa sababu Wizara hii kazi yake ni kuhakikisha kwamba inachochea Watanzania na mashirika ya ndani ya nchi yaweze kuwekeza uwekezaji wenye tija na siyo uwekezaji wa kifisadi.
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie kidogo suala zima la viwanda. Waziri hapa kazungumzia kwa kiasi kikubwa sana na alikuwa anaruka sana wakati anazungumzia kwamba sasa hivi Taifa letu litajenga viwanda vya kutosha na nchi yetu itaondokana na umaskini kupitia sekta hii ya viwanda. Nizungumza hapa wakati ule tunachangia Mpango wa Serikali kwamba viwanda hivi lazima viwekewe utaratibu maalum wa kuhakikisha kwamba Watanzania walioajiriwa wanafanya kazi kwa tija ili waweze kuondokana na umaskini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tukiangalia Kiwanda cha Dangote, nimekuwa nikilia sana kwenye Bunge lako hili, ambacho kipo Mtwara Mjini pale, kile kiwanda kimewekezwa na wawekezaji kutoka nje, mwekezaji kutoka Nigeria anaitwa Aliko Dangote, lakini mashirika yaliyopo mle ndani ambayo yanaajiri Watanzania ambao ndio leo hii tunawazungumzia hapa kwamba waondokane na umaskini kile kiwanda kinanyanyasa kwa kiasi kikubwa Watanzania waliopo mle ndani. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia hata namna ya upataji wa kazi, wananchi wa Mikoa ya Kusini wa Mtwara na Lindi ili wapate kazi mle ndani lazima watoe rushwa kuanzia shilingi laki tatu na elfu hamsini. Nilizungumza hapa na nilimwomba Mheshimiwa Waziri ahakikishe kwamba anaunda Tume Maalum ije Mtwara ifanye ukaguzi wa haya ninayozungumza na mwisho wa siku waweze kuwachukulia hatua wale watu, lakini kama Waziri anarukaruka na kusema kwamba tunawekeza katika viwanda wakati hivyo viwanda vichache vilivyopo, watu wananyanyaswa, wanapewa mshahara mdogo, wanapewa shilingi elfu sita kwa siku badala ya shilingi elfu kumi na mbili halafu tunasema kwamba tunataka tuondoe umaskini kupitia viwanda! Nimwombe sana Mheshimiwa Waziri ahakikishe kwamba anatembelea kiwanda hiki. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo la ajabu kabisa kwa wananchi wa Mikoa ya Kusini, hiki Kiwanda cha Dangote kimeanza kuzalisha cement, cement inazalishwa kwa wingi sana. Cha ajabu ni kwamba, bei ya cement Mtwara na Lindi ambako ndiko cement yenyewe inatoka ni shilingi elfu kumi na tatu na mia tano ukija Dar es Salaam, cement ile ile inayotoka Mtwara mpaka Dar es Salaam kilomita zaidi ya mia tano inauzwa shilingi elfu kumi na mbili, huku sio kuwadharau wananchi wa Kusini?
Mheshimiwa Naibu Spika, tumekuwa tunazungumza sana kwamba, tumenyanyasika sana Wanakusini lakini tukizungumza mnatupiga mabomu, mnatuletea Wanajeshi. Haiwezekani na haikubaliki hata kidogo na wala haingii akilini kwa watu wenye akili, kiwanda kiko Mtwara, halafu kinazalisha cement, pale pale Mtwara shilingi elfu kumi na tatu na mia tano, ikisafirishwa kwenda Dar es Salaam na maeneo mengine shilingi elfu kumi na mbili na mia tano, huku ni kuwadharau wananchi wa Kusini na wananchi wa Kusini tunasema tutachoka hivi sasa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumze kidogo suala zima la Viwanda vya Korosho. Viwanda vya Korosho kwa mfano pale Mtwara, kulikuwa na kiwanda kidogo kinaitwa Kiwanda cha OLAM, lakini kwa usimamizi mbovu wa Serikali ya Chama cha Mapinduzi kile kiwanda kimeachwa kinahamishwa badala ya kutengeneza mazingira rafiki, hiki kiwanda niseme tu kwamba kilikuwa kinaajri takribani akinamama 6,000 ambao walikuwa wanabangua korosho, lakini hakikutengenezewa mazingira rafiki, kikafanyiwa hujuma, mwisho wa siku yule mwekezaji amekihamisha hiki kiwanda na kukipeleka Mozambique. Halafu tunasema kwamba tunataka tuweke mazingira rafiki!
Mheshimiwa Naibu Spika, kila mmoja anafahamu kwamba kama kweli Serikali ingekuwa makini ikajikita katika kuwekeza na kufungua viwanda vidogo vidogo vya korosho, tunaamini kabisa umaskini ungeweza kuondoka katika Mikoa yetu hii ya Kusini na Tanzania kiujumla. Tunasema tu kwenye makaratasi, mikakati yetu haioneshi kwamba kweli tuna nia ya dhati ya kuhakikisha tunajenga viwanda hivi ili tuweze kuwakomboa wananchi wetu ambao ni maskini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niombe sana, kama kweli tunahitaji kufufua viwanda ili viweze kuleta tija kwa Watanzania, tujenge Viwanda vya Korosho. Korosho yenyewe, kama unavyojua kwamba, kila kitu kinachotoka kwenye korosho ni thamani. Maganda yenyewe ni thamani, mafuta ni thamani, korosho zenyewe ni thamani! Tuhakikishe kwamba tunayenga viwanda vya korosho maeneo ya Kusini na Tanzania kiujumla ili tuweze kuondokana na umaskini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nimalizie kwa kusema kwa mfano tuna madini ya Tanzanite, nilikuwa nafanya utafiti mdogo tu, nilikuwa naingia kwenye maduka kuangalia ni madini gani sasa hivi yana thamani. Ukiingia dukani ukakuta Tanzanite unaona ni miongoni mwa madini ambayo yana thamani kuliko madini mengine sasa hivi. Nashauri tujenge viwanda vya kufanya processing.
MHE. MAFTAHA A. NACHUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.