Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 –Wizara ya Katiba na Sheria

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 –Wizara ya Katiba na Sheria

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa dakika tano hizi nimalizie mchango kwenye Wizara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, niunge mkono hotuba hii lakini kwa sababu ya muda nijielekeze moja kwa moja kwenye mada. Ni ukweli usiopingika tunalo tatizo la watumishi. Hili ni tatizo la Kitaifa kwamba kila Idara kuna upungufu mkubwa wa watumishi. Sasa leo mimi nitazungumzia Idara ya Mahakama hasa Ofisi ya Mtendaji Mkuu wa Mahakama.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na upungufu mkubwa wa watumishi kwenye Idara hii lakini kuna unyanyasaji mkubwa sana wa watumishi kwenye Idara hii hasa kwenye upandishwaji wa madaraja. Watumishi wengi wa Idara ya Mahakama wanahangaika kutafuta madaraja, hawapandishwi madaraja kwa wakati. Hili nalo limekuwa ni donda kubwa kwenye Ofisi ya Mtendaji Mkuu wa Mahakama.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninao mfano hapa, nina mtumishi aliyeajiriwa tarehe 4 June, 1990 anaitwa Rashid Ally Libago, mtumishi huyu tangu mwaka 1990 mpaka leo nasimama hapa hajawahi kupanda daraja. Sasa hebu chukulia mshahara wa mwaka 1990, huyu anadumu nao mpaka leo atapata mafao ya shilingi ngapi? Jambo hili linasikitisha sana na barua zake ninazo hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, barua ya mwisho ameandika tarehe 12 Mei, 2020 nayo haijapata majibu mpaka leo. Jambo hili ni la kusikitisha sana na barua yake ya uthibitisho ilikuwa ni tarehe 14 Julai, 1999. Mshahara hapa siusemi lakini jamani tufikirie, hawa watumishi wanafanya kazi kwenye mazingira magumu sana sasa inapotokea mtumishi anafuata haki zake, hili suala la kuzungushwazungushwa nalo sio jambo jema. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ni la kisera. Ilani yetu inasema tumekusudia kila Wilaya iwe na Mahakama ya Wilaya; lkila Kata kama sio Tarafa iwe na Mahakama ya Tarafa au Kata. Wilaya ya Liwale ni Wilaya tangu mwaka 1975 lakini mpaka leo hatuna jengo la Mahakama ya Wilaya. Jengo linalotumika sasa ni lile lililokuwa na mkoloni ambalo ndiyo ilikuwa Mahakama ya Mwanzo ya Liwale Mjini.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo masika hii ukienda ofisi ya masijala wamefunika maturubai kwa sababu jengo lile linavuja. Kibaya zaidi au cha kusikitisha zaidi bajeti ya mwaka 2017/2018 niliuliza swali la nyongeza hapa Mahakama ya Wilaya ya Liwale itajengwa lini? Mheshimiwa Waziri alitumia sekunde moja tu kunijibu, Mahakama ya Wilaya ya Liwale tunaijenga mwaka 2018, akafunga kitabu akaenda kukaa leo tunazungumza ni mwaka 2021 haijajengwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ombi langu, tunapouliza maswali hapa na kujibiwa, kama Waziri huna uhakika wa jambo hilo basi jipe muda lakini unapowaambia watu kwamba Mahakama ya Wilaya ya Liwale itajengwa mwaka 2018 watu wanakusikiliza. Mpaka leo mimi wananiuliza, Mheshimiwa Waziri alikudanganya? Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi imeshaanza kusema uongo? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi naiomba sana Serikali tunapojibiwa maswali kwanza ijulikane kwamba sisi tumeagizwa na wananchi na tunachokisema hapa tunasema kwa ajili ya wananchi, tunaomba tujibiwe kama wanavyotaka waajiri wetu. Wilaya ya Liwale ina Kata 21, Mahakama za Mwanzo mbili tu; ya Liwale Mjini na Tarafa ya Makata, tunaiomba Serikali itufikirie. Nililisema hili wakati nachangia hotuba ya Waziri Mkuu. Miongoni mwa majengo niliyoyataja ambayo hayana sura ya kuitwa Ofisi ya Wilaya ya Liwale, hayana sura hiyo ni pamoja na jengo la Mahakama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho nizungumzie suala la Wazee wa Baraza la Mahakama mpaka leo posho yao ni Sh. 5,000 na posho yenyewe haitoki mpaka siku ya hukumu ya kesi. Kuhudhuria kesi hawalipwi, wanalipwa pale kesi inapohukumiwa. Sasa tufikirie hii Sh. 5,000 ni ya mwaka gani na leo tunazungumzia mwaka gani. Hawa watu hawaruhusiwi kukosa, kila kesi ikiitwa wao wanaenda, kesi isipohukumiwa wanatoka kama walivyokuja mpaka hukumu ya hiyo kesi. Kwa shida iliyopo ya kuwa na Mahakimu wachache na vitendea kazi vichache, kesi zetu zinachukua hata miaka minne au mitano, wewe Mzee wa Baraza unasimamia kesi miaka mitano unafukuzia Sh. 5,000. Ombi langu kwa Serikali tufikirie mambo mawili; aidha, kuwaajiri au kuwoangezea hako ka posho. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa nafasi hii. (Makofi)