Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. George Boniface Simbachawene

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibakwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS (TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nampongeza Waziri wa Elimu kwa kuwasilisha bajeti nzuri, lakini pia kwa kutekeleza majukumu yake vizuri pamoja na watendaji wote wa Wizara hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, nachukua nafasi hii kuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote wa pande zote mbili, kwa michango yao mizuri ambayo kwa hakika inalenga katika kusaidia Taifa hili kwenda vizuri katika suala zima la uhai wa Taifa kwa maana ya elimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, yamesemwa mengi hapa na pengine niseme tu, yote haya sisi kama Wizara ya TAMISEMI ambao ndio wamiliki wa shule za Serikali, maana hapa kulikuwa kuna kuchanganya kidogo mambo na pengine nitumie nafasi hii kueleza kwa uwazi; kwa nini tuligatua shule zile za Serikali kutoka Wizara ya Elimu kuleta TAMISEMI? Msingi wake kwanza ni wa kikatiba, ugatuaji wa madaraka ni wa kikatiba. Ukisoma Ibara ya 145(1) na Ibara ya 146(2) zinaeleza juu ya uanzishwaji wa Mikoa, Wilaya na Halmashauri lakini pia mamlaka hizo zinapewa majukumu ya huduma za jamii, afya, elimu barabara na mambo mengine yote yanayohusiana na jamii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa kulikuwa kuna mjadala mkubwa na ninajua mjadala huu umekuwa ukiendelea hata kwenye ma-corridor ambapo kimsingi mjadala huu unataka kuturudisha tulikotoka; kwa maana ya kwamba Wizara ya Elimu isimamie shule zote, isimamie wanafunzi wote, itunge mitihani, itunge vitabu; yaani ishughulikie ithibati, imiliki shule za Serikali, iangalie shule za binafsi, iangalie vyuo, iangalie Vyuo Vikuu, vyote hivi vinarudisha Wizara ya Elimu. Tunarudi tulikotoka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni vyema tukaangalia kama TAMISEMI imeshindwa, imeshindwa kwa sababu gani? Kwanza nieleze, mgawanyo wa haya majukumu ni upi? Baada ya mafanikio ya MESS I na MESS II, katika elimu ya sekondari mwaka 2008 Serikali ya Awamu ya Nne iliamua kugatua shule hizi kuzipeleka kwenye mamlaka ya Serikali za Mitaa. Majukumu ya TAMISEMI ni yafuatayo katika elimu: kusimamia uendeshaji wa elimu msingi, yaani Elimu ya Awali, Elimu ya Msingi, Elimu ya Sekondari, Elimu Maalum na Elimu ya Watu Wazima.
Pili, kuratibu upelekaji wa rasilimali fedha na ruzuku za uendeshaji kwa kushirikiana na Wizara ya Fedha, lakini tatu kusimamia matumizi ya fedha na ruzuku shuleni, lakini nne, kuimarisha rasilimali watu kwenye ngazi za shule, Halmashauri na Mikoa na tano kusimamia uwajibikaji wa watendaji wote na viongozi wote wa elimu kwenye ngazi za shule na Halmashauri za Mikoa; sita, kusimamia uendeshaji wa michezo katika Shule za Msingi na Sekondari.
Mheshimiwa Mwenyekiti, majukumu haya ni majukumu ambayo yamekabidhiwa kwa TAMISEMI. Sasa TAMISEMI ni nani? Ni mamlaka za Mikoa, Wilaya na Halmashauri zetu kwamba leo hii Mkurugenzi yule ndio mwajiri wa Walimu wa Sekondari. Ni rahisi sana kwa mfano shule za kwenye Wilaya yako ya Kasulu kwa mfano kuhudumiwa na Mkurugenzi shughuli zao zote. Issue hapa: Je, Mkurugenzi anawahudumia? Kwanini hawahudumii? Ndiyo issue ya kujadili. Anashindwa nini? Hana nini? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo kuhamisha! Mnakumbuka ilivyokuwa maandamano Wizara ya Elimu pale, palikuwa hakuna hata mahali pa kukanyaga, tulikuwa tume-centralize. Ukisoma hata democratic development za aspects mbalimbali za kimaendeleo ya kidunia decentralization ndiyo mfumo wa kidemokrasia. If you centralize, maana yake unataka mtu anayesoma shule ya Kasulu kule, yule Mwalimu Mkuu awe chini ya Katibu Mkuu Wizara ya Elimu Dar es Salaam. Hizo allowance za kumlipa anaposafiri kwenda kucheki kule na kurudi, tutazitoa wapi? Tusirudi kule tulipotoka jamani, kama kuna makosa, tuyajadili hayo. Mimi sisemi kwa sababu nipo leo TAMISEMI, naweza nikatoka kesho, lakini tunataka kurudi kule kwa jazba. Wizara ya Elimu ina majukumu gani? Hebu tuyaangalie. (Makofi)
Kwanza huo udhibiti, hapa yanazungumzwa masuala ya vitabu; huo udhibiti tu peke yake, ni majukumu makubwa kweli kweli! Ithibati peke yake ni majukumu makubwa; Vyuo Vikuu peke yake ni majukumu makubwa; Vyuo vya Elimu hivi vya kati vya Diploma na Certificate ni majukumu makubwa; Vyuo vya VETA ni majukumu makubwa! Leo mnasema na shule turudishe kule. Tunataka kufanya kosa walilolifanya waliopita. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwa sababu wali-centralize na mambo haya yakashindikana na leo tumeongeza shule, tuna shule nyingi, tuna Walimu karibu laki mbili wa Shule za Msingi, tuna Walimu karibu laki moja wa Sekondari. Hawa wote tunataka waende Dar es Salaam. Tuna wanafunzi hawa; hivi inawezekanaje? Hebu tutafute jibu, kwaniini hatutoi huduma nzuri? Tatizo ni kwamba tuliokabidhiwa ambao ni sisi Wabunge, tupo kwenye Halmashauri, ndipo shule zilipo; tuna Wenyeviti wa Halmashauri, ndio wanaowa-controll kwa nidhamu na kila kitu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, je, wanasimamia, rasilimali, zinakwenda? Ndiyo maana Mheshimiwa Rais anasema kama kuna uozo, upo kwenye Halmashauri. Mimi sikatai, ni kweli. Hapa tusaidiane Waheshimiwa Wabunge, hili Taifa ni letu. Tunapofika hatua fulani, lazima tukubaliane wote; na ndio maana nataka nikubaliane na aliyesema hebu siku moja tufungiane kusiwe vyombo vya habari. Nafikiri alisema Mheshimiwa Mbatia, akasema, hebu tuzungumze mambo ambayo tuna maslahi wote ambayo yanafanana. Tukiwa tunazungumza tuna-criticize tu hapa hatuwezi kupata majibu. Kwa mfano, unazungumzia waliosimamia mitihani mwaka 2014/2015 kwamba hawajalipwa baadhi ya fedha zao. Unajua kilichotokea? TAMISEMI wameomba 17.7 billion, Wizara ya Fedha ikatoa 17.7 billion. TAMISEMI wanakwenda kupeleka kwenye Halmashauri zile pesa, wanasema hazitoshi. Wanarudi wanaomba 6.8 billion kwamba hizi hawa wamekosa. Unauliza 6.8, how? Wanasema, kwa sababu hii na hii; hebu leteni mchanganuo. Mchanganuo unakuja, 1.04 billion. Sasa hebu niambie, kwanini Waziri wa Fedha asikatae kutoa fedha, aseme ngoja kwanza? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mimi nasema uozo upo kwenye Halmashauri zetu. Ni lazima wote tujikute tuna majukumu na sisi Waheshimiwa lazima tuhakikishe tunahudhuria vikao vya Halmashauri kwa sababu tumepewa majukumu makubwa. Halmashauri zimepewa majukumu makubwa na ndiyo maana tunawajibika katika hata huu upungufu kwa sababu maamuzi yote tumepewa sisi kule.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, naunga mkono hoja. Ahsante sana.