Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira

Hon. Abdulhafar Idrissa Juma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mtoni

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira

MHE. ABDUL-HAFAR IDRISSA JUMA: Mheshimiwa Spika, naendelea kukushukuru na kumshukuru Mwenyezi Mungu kama desturi yangu kutokana na neema hii ya uhai na afya ambayo mara nyingi tunaendelea kupewa.

Mheshimiwa Spika, naomba nichangie haraka haraka katika hotuba hii ya bajeti kuhusiana na masuala haya ya utatuzi wa masuala ya Muungano. Niipongeze sana Ofisi ya Makamu wa Rais kwa namna ambavyo imeendelea kupambana na masuala ya Muungano na wakafanikiwa kutatua baadhi ya changamoto za Muungano hasa hizi tano ambazo zimesemwa katika bajeti. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nigusie hasa hii kuhusu gharama za kushusha mizigo bandarini. Muungano huu pamoja na faida zake kama walivyotangulia kusema wachangiaji wenzangu; changamoto zitakazokuja kujitokeza kwa umri wake ni namna ambavyo wananchi wa upande mmoja wanafaidi fursa za upande mwingine kwa usawa ama katika nafasi ya kupeana favour kwa sababu ni Muungano. Zanzibar ina watu wasiozidi 1,600,000 kwa makadirio; lakini Dar es Salaam tu peke yake ambayo ndiyo geti kubwa la watu kutoka Tanzania Zanzibar kuingia Tanzania Bara ina watu takribani 5,000,000 kuelekea 6,000,000.

Kwa hiyo, utaona namna gani potentiality ya soko la kibiashara ilivyo kwa upande wa Zanzibar na Tanzania Bara, hasa kupitia geti la Dar es Salaam. Nipongeze sana kwa hatua hii, lakini iendelezwe haraka ika-reflect kwa wananchi wetu kama walivyosema wenzangu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, utatuzi huu unaweza ukaleta ufumbuzi wa kurahisisha biashara lakini Muungano huu ni wa watu. Mimi nakuthibitishia sijafanya utafiti lakini ni uhakika zaidi ya asilimia 70 ya familia za wananchi Zanzibar tuna Ndugu zetu upande wa Tanzania Bara moja kwa moja. Mimi binafsi yangu, baba na mama yangu wanaishi Tanzania Bara, kwa hiyo, kuna mambo mengi sana nayahitaji katika kuunganisha. Kwa hiyo, wakati wakitatua masuala ya kibiashara na watatue masuala ya kiubinadamu moja kwa moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, haifurahishi hata kidogo mtu anatoka Zanzibar, amebeba sukari kilo tano tu kwa ajili ya kumpelekea mzazi wake au jamaa yake Tanzania Bara akifika pale bandarini anasumbuliwa. Sasa wakifanya utatuzi katika jambo hili isemwe wazi; Wizara ya Muungano ikaweke bango pale bandari ya Zanzibar, iweke bango pale bandari ya Dar es Salaam waseme sukari mwisho kilo moja ama usibebe kabisa ishia hukohuko; TV usibebe kabisa, ukibeba fuata tararibu hizi za kibiashara. Kwa hiyo, ningetamani waseme pamoja na kuwapongeza kwa haya waliyoyafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nizungumzie suala la TASAF. Zanzibar ina Shehia 338; mpaka sasa Shehia 204 ndizo ambazo zinapata ruzuku ile kwa watu wa kaya maskini. Natambua katika bajeti hii ilivyosomwa kuna mnyanyuko wa Shehia, miongoni mwa Shehia zitakazonufaika ambazo zilikuwa hazipati ni zile zilizopo katika Jimbo langu la Mtoni. Jimbo langu lina Shehia tano, Shehia tatu zilikuwa zinapata msaada wa kaya maskini; Shehia ya Sharif Musa na Shehia ya Kwagoa zilikuwa hazipati. Natambua katika bajeti hii Shehia hizo mbili zimekwenda kuonekana lakini natambua pia si Shehia zote 338 za Zanzibar zitakwenda kumulikwa na mradi wa TASAF katika awamu inayoendelea. Naomba sana Serikali yetu hii, iendelee kutunisha na kutafuta uwezo wa mfuko wa TASAF ili Shehia zote 338 katika Visiwa vya Unguja na Pemba vinufaike na mradi huu wa kunyanyua na kuziwezesha kaya maskini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wabunge tulipewa semina kama ambavyo Mheshimiwa Waziri amesema kuhusiana na Mfuko wa Jimbo kwa kule Zanzibar; natamani semina hiyo hiyo pia wakapewe wale wasimamizi wa fedha zetu kwa upande wa Zanzibar. Tujue, sisi tumeambiwa mipaka yetu ya fedha hizi na wale wakaambiwe kwamba mipaka ya fedha hizi za Mfuko wa Bunge la Jamhuri ya Muungano ni huu ili tukienda kuongoza vile vikao vya matumizi wasije wakaona labda tunawaingilia katika baadhi ya mambo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kumalizia, napongeza sana jitihada zinazochukuliwa katika kutoa elimu, lakini pia mfanye tathmini ya elimu mnayoitoa kuhusu Muungano; je, inakidhi mahitaji ya kisasa ya mabadiliko ya teknolojia? Mnaweza mkatoa elimu lakini bado ikawa haiwafikii watu wengi kwa sababu bado tunanung’unika sana kuhusu Muungano kuliko neema zake.

Mheshimiwa Spika, naomba nielezee Kiti chako na Bunge hili raha za Muungano, mimi ni mmoja wa wanufaika maana mke wangu ni Mchaga wa Rombo. Muungano una mambo mengi mazuri. Kama elimu inatolewa, taarifa zinakwenda, sasa fanyeni evaluation namna mnavyopeleka elimu na mabadiliko ya teknolojia. Ningetamani kila tunapopita tuone tunazungumzia raha za Muungano. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, unaona changamoto zinazojitokeza visiwa kuanza kuliwa, hatutegemei visiwa vyetu vije vifutike, lakini kama mabadiliko ya tabianchi ulimwenguni yakiendelea ni lazima athari ya kupotea visiwa itatokea, tutakwenda wapi? Tuyaseme haya wazi sasa kama Muungano unatupa fursa ya kutembea, unatupa fursa ya kujenga na kujianda kama yale tunayotaka kuyazuia yakishindikana tuweze kuishi upande huu bila bughudha yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa fursa hii, naipongeza Wizara hii lakini naendelea tu kuishajihisha, Shehia 338, tuko katika Shehia 204 sasa mmeongeza Jimbo la Mtoni, mkimaliza Shehia 2 sina kesi nanyi lakini Zanzibar zitimie Shehia zote 338; Zanzibar tuendelee kula raha na kufaidi Muungano. Ahsante sana. (Makofi)