Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira

Hon. Khalifa Mohammed Issa

Sex

Male

Party

ACT

Constituent

Mtambwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira

MHE. KHALIFA MOHAMED ISSA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Awali ya yote nimshukuru Allah Subhanallahu Wataallah kwa kutujaalia uzima na afya na kuukabili huu Mwezi Mtukufu wa Ramadhan kwa salama. Inshaallah Mwenyezi Mungu atujaalie tuukamilishe kwa salama.

Mheshimiwa Spika, nataka nijikite katika jambo hili la mazingira kwa maana ni jambo muhimu sana katika uhai wa binadamu. Mazingira yanayotuzunguka yanaakisi uhai wa binadamu na viumbe hai ambao wapo ndani ya ardhi yetu hii tunayoishi. Kuharibika kwa mazingira au kuharibiwa; ni kuharibika kwa maisha ya binadamu na viumbe hai vilivyomo. Mazingira uharibiwa ama kwa makusudi au bila kujua na binadamu wenyewe katika maisha yao ya kila siku ya kutafuta riziki zao. Sasa ni juu ya Serikali kusimamia na kuona kwamba mazingira haya kwa namna yoyote hayawezi kuharibiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikija katika Serikali yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Zanzibar ni sehemu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na inajumuisha Visiwa vya Unguja na Pemba na visiwa vidogo vidogo ambavyo vimezunguka visiwa hivyo. Kwa hivyo, uwepo wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania unategemea pia uwepo wa Visiwa vya Zanzibar.

Mheshimiwa Spika, tumeona mabadiliko ya tabia nchi yameathiri sana na kama nilivyosema mwanzo hata matendo ya binadamu wenyewe ya siku kwa siku yameathiri mazingira yetu hivyo bahari imechukua sehemu kubwa sana. Tumeambiwa katika tafiti nyingi kwamba katika miaka 50 zaidi ya sentimeta 19 – 20 zimekuwa maji ya bahari kwa maana ya kwamba kina cha bahari kimekuja juu. Kwa hiyo, imeathiri visiwa vingi sana vya Zanzibar kwa maana ya Unguja na Pemba kutaka kutoweka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niruhusu nitoe mifano michache kwa Zanzibar ambapo ni ushuhuda wa wazi wa kuondoka kwa visiwa. Kwanza, kuna Kisiwa cha Mtambwemkuu ambacho kimo katika Jimbo langu; Kisiwa kile kinavamiwa kwa kasi sana na maji ya bahari kiasi kutishia watu kutaka kuhama katika maeneo yao. Mfano wa pili; katika Jimbo langu pia kuna sehemu inaitwa Tosawana. Sehemu hii ina mashamba ya mpunga; watu wanajitafutia riziki zao kwa kulima katika maeneo yale, lakini kwa kweli kila baada ya muda maji ya bahari yanavamia mashamba yale ikabidi watu kuhama. Kwa kweli TASAF katika kipindi cha miaka miwili iliyopita walijitahidi kujenga tuta pale lakini kwa sababu lile tuta halikujengwa kitaalam, wala halikusimamiwa baada ya muda mfupi limeyeyuka kwa hivyo bado maji yanaingia kwenye mashamba ya watu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna mfano mwingine katika eneo la Jimbo langu hilo hilo, kuna sehemu tunaambiwa miaka 50 iliyopita au zaidi kidogo ilikuwa ni mashamba watu wanalima mpunga, maji baridi lakini leo huwezi kupita kwa mguu lazima upite kwa kidau. Hii ni kutokana na maji ya bahari kupanda kila kukicha. Kuna mfano kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge, Kisiwa cha Misali; Kisiwa cha Utalii; baada ya muda mfupi kinaweza kupotea kwa sababu ya kuvamiwa na maji. Kuna Kisiwa cha Mnemba pia Kisiwa cha Utaliii, nacho kiko hatarini kukikosa. Jimbo la Mheshimiwa hapa Bandani kuna Shehia ya Mjananza kuna sehemu inaitwa Uvuni kuna wakulima zaidi ya 100; leo wamehama kwa sababu maji ya bahari kuvamia mashamba yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile katika Kisiwa Panza bahari inakaribia shule, kwa hiyo makazi ya watu yako hatarini kuondoka. Mwambeshidi mashamba yamevamiwa na maji, Ukunda Kengeja, Mwambe Shamiani, Nanguji, kote watu wamejitahidi kupanda miti kwa jitihada zao lakini bado kasi ya maji ni kubwa kwa hiyo athari inaweza kutokea wowote.

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa ushauri tu kwa Serikali, kipindi kilichopita tuliomba sana lakini haikuwezekana, naomba tena Waziri na wataalam wake watembelee maeneo haya ili wakague na kuona zile athari ili wajue hatua za kuchukua.

Mheshimiwa Spika, mwisho niseme…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante Mheshimiwa Khalifa.

MHE. KHALIFA MOHAMED ISSA: Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)