Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Michael Constantino Mwakamo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibaha Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi ya kuweza kuchangia kwenye Wizara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kama walivyoanza wenzangu kuwapa shukrani Waziri na Naibu Waziri kwa kazi nzuri wanazoendelea nazo hasa kwa kuanzia hotuba ya bajeti ambayo Waziri ameiwasilisha jana na ameonesha ni namna gani amejipanga na namna gani anayajua yaliyo ndani ya masuala ya utumishi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niwashukuru pia Waheshimiwa Wabunge wote kwa namna ambavyo wameona na ameguswa na shida za watumishi na hii inaonesha ni kwa namna gani ndani humu Wabunge tumekuwa wawakilishi wa kweli wa wananchi kwa nafasi zote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa pamoja na michango mingi ambayo wengi wameisema na nisingependa sana niirudie kwa sababu itakuwa ni kula muda na watu wanatakiwa kuchangia, lakini nina maeneo machache ambayo na mimi nataka nianze kuzungumza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza ambalo nataka nilizungumzie ni suala zima la maslahi ya wastaafu na hasa katika masuala mazima ya upatikanaji maslahi yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe niseme kwamba katika nchi hii sasa hivi na hata hususani kwenye jimbo langu kuna watumishi wengi wamestaafu, lakini shida hata kufungishwa mizigo kurudishwa imekuwa mtihani na umekuwa mtihani mkubwa sana na kulifuatilia jambo hili ukipeleka kwenye Ofisi ya Wizara ya Utumishi wanakuambia watumishi wengi wako kwa Mkurugenzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini lazima tukiri, humu ndani wote tumezungumza ni namna gani Halmashauri nyingi zimekuwa na mapato yawe madogo na ni namna gani Halmashauri zimekuwa na mzigo mkubwa wa kuendesha shughuli za Halmashauri. Wanawezaje kuwasafirisha watumishi hawa na kuwarudisha makwao kwa sababu sehemu kubwa ya watumishi kwa sasa hivi kwenye nchi hii wanapatikana kwenye hizi Halmashauri mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ningeiomba Wizara ya Utumishi, jambo hili walitazame kwa kina, walichukue, walifanyie kazi, pamoja na kwamba majukumu hayo wameyaacha kwa Halmashauri, lakini vyema wakalifanyia kazi wakawasaidia wakaja na mpango unaoweza kusaidia kuondoa tatizo hili kwenye watumishi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini sambamba na hilo wapo watumishi wamezungumza akiwepo Mheshimiwa Nape Nnauye alizungumza namna watumishi wanavyopata taabu kwenye maslahi na hasa hasa maslahi yao ya kustaafu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilipata wageni hapa, Naibu Waziri anafahamu, nililazimika kumtafuta anisaidie kujibu hoja zao. Watumishi wale walisahaulika kwenye bajeti, walikuwa wanastahili kupanda vyeo, lakini katika mazingira yasiyoyakueleweka wakasahaulika kupanda vyeo. Kwa bahati mbaya wakapewa wengine barua za kupanda vyeo vyao wale ambao walibahatika, lakini kilichotokea wamekosa mshahara haujabadilika, na wengi wa timu hii wamestaafu, wamekuja kwangu hapa mjini Dodoma, tumekwenda kwa Naibu Waziri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kinachosikitisha kwasababu wameshastaafu hawawezi kurekebishiwa zile haki zao, sasa watu hawa tunawasaidiaje? Na hii Serikali ya Chama cha Mapinduzi ni Serikali ya kushughulikia matatizo na watu waliokuwa na mazingira magumu. Ni kwa namna gani sasa sisi tunaona ni namna gani tunaweza tukawasaidia watu hawa, twende tukawatengeneze utaratibu maalum na ikiwezekana Waziri apite kwenye maeneo hayo, apate hayo makundi ambayo yana matatizo na hatimaye atengeneze mpango maalum uletwe kwenye Serikali tuwasaidie kuwatoa watu wale, kwa sababu hakika kabisa ni watu ambao wameitumikia Taifa hili, ni watu ambao wametengeneza mambo mengi kwenye nchi hii na kwa kweli leo wananyanyasika kupitiliza wakifuatilia madai yao pasipokuwa na mafanikio.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kundi hilo nashukuru leo tumepata taarifa nzuri hapa kwamba kuna shida kwenye mifuko, watumishi wanastaafu, wanakwenda kufuatilia pesa zao kwenye mifuko, inaonekana kuna miaka katikati hapa mwajiri hajapeleka makato, eti analazimishwa mtumishi yule kwamba kwanza akafuatilie makato yake, halafu yaje yajaziwe pale kwenye maeneo ambayo alikuwa hajamaliza halafu ndio aweze kulipwa. Hii kweli jamani lazima tuitazame kwa kina inawatesa watumishi wengi, na hivi tufikirie ingekuwa inatugusa sisi Wabunge tungekuwaje? Hebu tunaomba tufanyie kazi, Waziri amezungumza hapa kwamba lazima watu wale walipwe na ukitazama ndio sheria inavyosema.

Mheshimiwa Naibu Spika, Bunge limepitisha sheria hapa tarehe 20 Oktoba, 2017 ya kuunganisha mifuko, hiyo sheria inasema majukumu ya kufuatilia makato, majukumu ya kupeleka makato kwenye mifuko, ni jambo la mifuko yenyewe na waajiri watajuana wenyewe, huyu mtumishi anatakiwa akistaafu akachukue hela yake aendelee na shughuli yake. Leo anatakiwa afanye kazi ya kufuatilia makato yake…

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mwakamo, kuna Taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Ester Bulaya.

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na mchango wake mzuri, kwa ajili ya rekodi tu nilikuwa nampa taarifa kwamba ile sheria ambayo tuliunganisha ya mifuko haikuwa mwaka 2017 ilikuwa mwaka 2018.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mwakamo unaipokea Taarifa hiyo?

MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niendelee kwa sababu ni suala zima la kurekebisha taarifa wanaorekebisha taarifa watakuwa wamekaa nayo vizuri. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na haya ambayo nimeyazungumza kwenye eneo hili, lipo jambo moja ambalo naomba nilieleze kuna hizi nafasi mbili ambazo wenzangu wamezizungumza vizuri, kuna hawa wanaitwa Watendaji wa Kata, kuna hawa wanaitwa Watendaji wa Vijiji.

Mheshimiwa Waziri mimi nakufahamu, na najua uchapakazi wako, nikuombe sana ndugu yangu hebu kada hii tuiangalie ni kada ambayo wengi wakizungumza hapa hawaizungumzi, lakini ndio wenye kazi ya kusimamia miradi, ndio wanaokusanya mapato kule, lakini ukiziona ofisi zao, ukiona maslahi yao wanayolipwa wao, unashangaa kabisa.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa, kengele imegonga.

MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)