Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Francis Kumba Ndulane

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia kwenye bajeti ya Wizara ya Utumishi na Utawala Bora.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ningependa kujikita kwa kuanzia kwenye maeneo mawili; eneo la upungufu wa watumishi pamoja na eneo la madeni, lakini kama muda utaniruhusu nitaongeza mambo mengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto ya upungufu wa watumishi imekuwa ni changamoto kubwa na ambayo imekuwepo Serikalini kwa muda mrefu sana. Mimi nimefanya kazi kama mtumishi wa umma kwa zaidi ya miaka 20 kabla sijawa Mbunge wa Jimbo la Kilwa Kaskazini. Miaka yote ambayo nimehudumu kama Mkaguzi wa Ndani wa Halmashauri, kama Mhasibu TANROADS, kama Mkurugenzi katika Halmashauri, changamoto ya upungufu wa watumishi na madeni kwa watumishi imekuwa ni changamoto kubwa ambayo imesababisha kuwepo kwa hoja za CAG ambazo zimeshindikana kufungwa kwa sababu changamoto zimekuwa zikiendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna baadhi ya Halmashauri katika nchi yetu na idara mbalimbali za Serikali zimekuwa na upungufu mkubwa wa watumishi kiasi kwamba baadhi ya majukumu yamekuwa yakishindwa kufanyika. Na niseme tu kwamba unapokuwa na upungufu mkubwa wa watumishi ni sawasawa na timu ya mpira ambayo inatakiwa kucheza wachezaji kumi na moja halafu unakuwa na wachezaji pungufu, hatutarajii timu ya namna hiyo iweze kushinda, ili timu iweze kushinda inatakiwa iwe na wachezaji kumi na moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niseme tu kwamba kumekuwa na hii changamoto hata katika Wilaya yangu ya Kilwa kumekuwa na changamoto hii kubwa, kuna baadhi ya zahanati zina watumishi mmoja-mmoja. Unaweza ukaona wale watumishi mmoja-mmoja wanaofanya kazi katika zahanati wanawezaje kufanya kazi wakati wanahitaji kuwa likizo, wakati fulani wanaumwa na kadhalika, lakini kuna zahanati moja kule katika Kata ya Kinjumbi, Kijiji cha Miyumbu ilikaa miaka tisa ikiwa inasubiri watumishi kwa sababu watumishi wachache. Mwaka jana ndio angalau tulipata mtumishi mmoja, lakini kuna zahanati katika Kijiji cha Bugo, Kata ya Chumo ina miaka zaidi ya mitano sasa hivi haijafunguliwa kwa sababu watumishi ni wachache, lakini leo tunacho Kituo cha Afya tunatarajia kukifungua hivi karibuni pale Somanga, tunafikiria, tunaumiza vichwa kwamba hali itakuwaje?

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ningeomba Serikali katika hili jambo, Wizara yetu ya Utumishi ilitilie maanani sambamba na suala la madeni ambalo nalo limekuwa ni shida. Madeni yamekuwa yakihakikiwa; katika utumishi wangu wa umma wa zaidi ya miaka 20 kila mwaka tumekuwa tukihakiki madeni; tunahakiki, tunahakiki, taarifa zinakuja watumishi kutoka Wizarani, Wizara za Kisekta zimekuwa zikija kuhakiki madeni, lakini mwisho wa siku madeni yanakuwa hayalipwi inavyotakiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika,kwa hiyo, kuna utitiri mkubwa, kuna kiasi kikubwa cha madeni kwa watumishi wetu kiasi kwamba inapunguza morali ya kufanya kazi kwa watumishi wetu, kwa hiyo, ningeomba hilo nalo lishughulikiwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vilevile nikirudi kwenye suala la watumishi katika Jimbo langu la Kilwa Kaskazini kuna shule shikizi saba. Katika zile shule shikizi zote zinahudumiwa na walimu wa kujitolea ambao wanalipwa viposho vidogo sana na wananchi baada ya kuwa wanachangia. Kwa hiyo, niseme kwamba, kwa kweli haya matatizo mawili ni matatizo makubwa hili la upungufu wa watumishi na madeni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu kwa Serikali kupitia Wizara ya Utumishi na Utawala Bora, niiombe iandae mpango kazi maalum ili ndani ya miaka minne ijayo wakati tunakwenda kwenye uchaguzi wa mwaka 2025 basi tuhakikishe hii changamoto imekwisha ili tuzipunguzie Halmashauri zetu na idara zetu hii hoja ambayo inaweza ikafungwa, lakini vilevile tuweze kuwasaidia wananchi wetu wapate huduma inayotakiwa katika maeneo mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo ningependa kulichangia ni suala la michezo ya watumishi. Miaka mitano iliyopita kulikuwa na Sera ya Michezo, kulikuwa na Mashindano ya SHIMIWI kwa watumishi wa sekta ya umma, lakini kule kwenye Serikali za Mitaa pia kulikuwa na michezo inafanyika kwa watumishi ili kujenga afya bora, lakini vilevile kupambana na maradhi kama ya UKIMWI na changamoto nyingine za kiafya, lakini hata kwenye mashirika ya umma pia walikuwa na michezo yao wanafanya, lakini ndani ya miaka mitano iliyopita michezo hiyo tumekuwa hatuioni na niseme tu kwamba, nafahamu Waziri, Mheshimiwa Mchengerwa, ni mwanamichezo nimuombe kwa interest aliyonayo kwenye michezo, lakini vilevile katika kuboresha afya za watumishi wetu basi tuweze kurejesha ile michezo katika taasisi za umma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho, kuna Mbunge mwenzangu amezungumza muda mfupi uliopita, kulikuwa na Wakurugenzi saba, RAS mmoja, pamoja na ma-DAS watatu walishiriki kwenye uchaguzi wa kura ya maoni mwaka 2010, lakini kwa masikitiko makubwa wale Wakurugenzi waliondolewa kwenye payroll ya Serikali na hatimaye mpaka leo hii hawajarudishwa, lakini nafahamu kwamba, wapo watumishi wengine wengi maelfu kwa maelfu walishiriki kwenye ule uchaguzi wa kura za maoni, walipotoka kwenye ule uchaguzi baada ya kuwa hawakupata nafasi ya kuendelea na uchaguzi uliofanyika tarehe 28 Oktoba, 2020 walirudishwa kazini baada ya kutoa taarifa kwamba, wametoka na hawakuvuka kwenye kura za maoni.

Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe Wizara iwasaidie wale watumishi kumi na moja, RAS mmoja, ma-DED saba, pamoja na ma-DAS watatu ili waweze kuridishwa kazini na wapate haki zao za msingi. Ahsante. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)