Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Innocent Edward Kalogeris

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. INNOCENT E. KALOGERIS: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia. Niendeleze hapo hapo alipozungumza dada yangu Mheshimiwa Munde Tambwe. Mkoa wa Morogoro tunaomba ukatwe ipatikane mikoa miwili. (Makofi/Kicheko)

MBUNGE FULANI: Ugawanywe.

MHE. INNOCENT E. KALOGERIS: Nimeelekezwa ni ugawanywe.

Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Morogoro ugawanywe ipatikane mikoa miwili ambapo kutakuwa na Wilaya ya Morogoro, Wilaya ya Mvomero, Wilaya ya Gairo na Wilaya ya Kilosa; na kwingine kutakuwa na Wilaya ya Ulanga, Wilaya ya Malinyi na Wilaya ya Kilombero. Tupate mikoa miwili ili kuweza kurahisisha kupata maendeleo katika Mkoa wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii kumpongeza sana dada yangu Mheshimiwa Ummy kwa uteuzi ambao ameupata katika Wizara hii mpya. Ni imani yangu kwamba yeye na wasaidizi wake; Manaibu wake watafanya kazi kubwa kama ile aliyoifanya akiwa Wizara ya Afya wakati wa mapambano ya Corona na tukashinda, naamini kabisa kwamba TAMISEMI atafanya vizuri zaidi. Hizi changamoto zote pamoja na mafanikio yote, lakini changamoto hizi tutakwenda kuzimaliza.

Mheshimiwa Spika, nianze na suala la barabara. Mimi ni Mkandarasi. Katika uhalisia, Wilaya ya Morogoro Halmashauri yetu ina eneo la square mita 11,731, ina barabara zenye urefu wa kilometa 750, ina madaraja makubwa 29, ina ma-box culvert 74, lakini mgao wake tunapata shilingi bilioni 1.1. Ni kwamba kwa namna moja au nyingine, tunatengeneza kilometa moja tu bila kugusa makalavati wala nini kwa shilingi milioni moja.

Mheshimiwa Spika, kama Mkandarasi, barabara ya changarawe ili iweze kupitika ikiwa na madaraja au box culvert, unahitaji kilometa moja kwa shilingi milioni 30. Sasa naomba tu, ndugu yangu Mheshimiwa Zungu amezungumza, Mwenyekiti wangu wa Kamati ya Miundombinu Mheshimiwa Kakoso amezungumza, tuangalie jinsi gani tunaisaidia TARURA. Katika kuisaidia TARURA, naomba, hawa wenzetu wamekokotoa, wamechanganua, ni kwamba kutakuwa na uwezekano wa kila mwaka kupata shilingi milioni 500. Katika hilo suala la Mwenyekiti wangu ndugu yangu Mheshimiwa Kakoso, kila mwaka tutakuwa tunapata shilingi trilioni 2,160. Naomba Serikali ichukue mawazo haya na ikayafanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika shilingi trilioni 2,160 ukizigawa kwa Halmashauri zetu, tutakuwa na uhakika wa kila mwaka kupata kila Halmashauri shilingi bilioni 11. Shilingi bilioni 11 ukipeleka kwenye Halmashauri, ndani ya miaka mitano, tatizo la TARURA litakuwa halipo tena hapa Bungeni. Kwa hiyo, naiomba Serikali tu, mama yangu Mheshimiwa Ummy, Waziri wa Fedha na wengine wote wanaohusika, lisimamieni hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitakupa kichekesho kimoja, lakini siyo kizuri. Juzi mliona katika mitandao, wale watu waliokuwa wanatembea uchi, wametoka jimboni kwangu. Kilichojitokeza, watu huwa wanavua nguo wanapopita kwenye barabara za umande, wanazihifadhi nguo zao. Kwa hiyo, naomba tu, tunadhalilika. Jimbo la Morogoro Kusini eneo kubwa ni milima, kwa hiyo, shida yetu kubwa ni barabara. Tunawaomba mtusaidie katika hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili, kuna suala la maboma, ndani ya Halmashauri yetu tuna maboma 170 yanasubiri kumaliziwa, tunaiomba Serikali sijui dada yangu Mheshimiwa Ummy katika bajeti ya mwaka huu umetutengea kiasi gani? Tunaomba tufanya jambo hilo ili zile nguvu ambazo wananchi wamezitumia zikakamilike na waone faida yake. Tutaendelea kuwahamasisha kufanya mambo mengine, lakini kama haya hatujawakamilishia wataona kama vile tunawapotezea nguvu zao. Kwa hiyo, katika bajeti hii sijui Halmashauri yetu umetutengea kiasi gani, lakini tunaomba maboma yakamilike.

Mheshimiwa Spika, lingine ambalo ningependa kulizungumza ni kwenye masuala ya madeni ya watumishi. Katika Halmashauri yetu watumishi wanadai karibu shilingi bilioni mbili. Watu hawa wanajitoa kwa hali na mali katika kufanya kazi, inapofika mahali hatuwezi kuwapatia fedha ambayo ni stahiki yao, tunakuwa hatuwatendei haki. Nawaomba katika bajeti hii, fedha zitengwe watu wapate haki zao ili waweze kututumikia vizuri vile inavyopasa.

Mheshimiwa Spika, la mwisho, namwomba dada yangu Mheshimiwa Ummy au wasaidizi wake, tukimaliza bajeti twende wote wakaone uhalisia wa Jimbo la Morogoro kusini na Halmshauri ya Morogoro jinsi gani ilivyo ili wakija katika bajeti ijayo wawe na mpango uliokuwa sahihi.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)