Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Kilumbe Shabani Ng'enda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kigoma Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii. Nami naungana na Wabunge wenzangu waliotangulia kuonesha imani yetu kubwa sana kwa viongozi wa Wizara hii ya TAMISEMI, Waziri, Naibu Mawaziri pamoja na Makatibu Wakuu na wasaidizi wote. Tuna matumaini makubwa sana katika utendaji wao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kabla sijazungumza mambo ya kijimbo, nilitaka nizungumze haya ya kisera kidogo na hasa ni utaratibu wa kupeleka fedha za maendeleo katika halmashauri zetu. Tulipokuwa kwenye vikao vya RCC tumekutana na tatizo kubwa sana na tatizo lenyewe ni utaratibu mpya nafikiri uliotolewa na Hazina wa kutaka fedha za maendeleo zitolewe baada ya kuwa kandarasi za kazi zinazotaka kufanyika katika mpango kazi zimetangazwa na wataalamu wameandikia na kwenda Hazina. Sasa utaratibu huu umechelewesha sana miradi mingi ya maendeleo kutekelezwa.

Mheshimiwa Spika, mwaka wa fedha wa 2019/2020 katika Mkoa wa Kigoma ni asilimia 78 tu ya fedha za maendeleo ndiyo zilizopelekwa lakini mwaka huu ndiyo hatari zaidi maana mpaka tunakwenda kumaliza robo ya tatu ya mwaka ni asilimia 23.3 ya fedha zote za maendeleo ndiyo zimeletwa. Tatizo kubwa limetokea wapi? Ni uhaba wa wataalamu hasa wahandisi ambao wanashughulika na kuchakata miradi hii ili ipelekwe Hazina kwa ajili ya kuombewa fedha.

Kwa hiyo, labda kama tunaona kuna ugumu wa kuwapata hawa wataalamu kwa wakati kwenye halmashauri zetu na kwenye Sekretarieti ya Mkoa basi turudi kwenye utaratibu wa zamani ambapo pesa zilikuwa zinatolewa Hazina kupelekwa mikoani na kwenye halmashauri kwa kuzingatia mpango kazi. Kama mpango umeshatoka na kasma imeshapitishwa na Bunge, pesa zipelekwe mchakato wa miradi ufanyike huko kuliko huu utaratibu wa sasa unachelewesha sana fedha kufika kwenye maeneo yale. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo napenda nilizungumze, mimi natoka Manispaa ya Kigoma Ujiji. Sisi ambao tunatoka katika miji tuna maeneo yetu ya mapato na wale wanaotoka katika vijiji wana masuala ya mazao, mifugo na kadhalika, wanakuwa na maeneo mapana ya mapato. Moja ya eneo kubwa tunalolitegemea katika mapato kwenye halmshauri zetu ni masoko. Nimeona Serikali imefanya kazi nzuri katika baadhi ya maeneo ya kujenga masoko ya kisasa lakini Manispaa ya Kigoma Ujiji bado eneo lake la kukusanya mapato hili la masoko halijaboreshwa.

Mheshimiwa Spika, tungeomba Wizara ya TAMISEMI waone uwezekano wa kusaidia ili tuweze kupata masoko yaliyopangiliwa na yaliyokaa kisasa na ambayo ni rahisi kudhibiti mapato yake. Nasema hili hasa ukizingatia kwamba Manispaa ile iko mpakani, meli zinakuja pale za kutoka Kongo, Burundi, waone hata nchi yetu unajua wengine hawajui Dar- Es-Salaam hawajui Dodoma, akifika pale akiona soko la hovyo anasema hivi Tanzania tunavyowaona walivyo soko lao ndiyo hili? Wenyewe wanasema ndiyo soko la Tanzania. Sasa mnatupa kazi ya kuanza kujieleza aah, kuna Kariakoo, kuna wapi, wenyewe hawajui. Kwa hiyo, tunaomba mtusaidie sana katika suala la kupata soko la kisasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Manispaa ya Kigoma Ujiji ni miongoni mwa Halmshauri ambazo hazina hospitali ya wilaya na mpaka sasa tunatumia hospitali ya Shirika la Dini la Babtist. Kwa sababu Serikali ni moja nilitaka niseme hili kwamba tumekwishakubaliana kule na sasa hivi tumepata eneo la kujenga hospitali ya rufaa ya mkoa, najua hii iko Wizara ya Afya, lakini ni kwamba hospitali hii ikipatikana hospitali ambayo inatumika sasa kama hospitali ya rufaa ya mkoa inaweza ikawa hospitali ya wilaya ikasimamiwa na Halmashauri ya Manispaa ya Kigoma Ujiji. Kwa hiyo, niombe tu Wizara hizi zinaweza zikafika mahali zikafanya mashauriano ya kusaidia kuharakisha ujenzi wa hospitali ya rufaa ya mkoa ili hospitali iliyokuwa inatumika kama hospitali ya rufaa ya mkoa ya Maweni iweze sasa kubaki kama Hospitali ya Halmashauri ya Manispaa ya Kigoma Ujiji.

Mheshimiwa Spika, nimalizie mchango wangu kwa kuzungumzia suala la upandishaji wa vyeo watumishi. Katika Manispaa ya Kigoma Ujiji lipo tatizo kubwa sana, Watendaji wa Kata na Mitaa walioajiriwa Julai 2005 sasa wana takribani miaka 16 hawajapandishwa vyeo. Naomba mlitazame suala hili.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)