Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Charles Muguta Kajege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mwibara

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nami naomba niende moja kwa moja kwenye hoja zangu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, nilipata bahati ya kuwa katika Kamati ya Utawala na Serikali za Mitaa tukapitia baadhi ya gharama katika baadhi ya mikoa. Kitu cha kwanza nilichogundua ni kuwa kuna ugawaji wa rasilimali ambao hauendani na hali halisi ya wananchi. Kwa mfano, kuna ujenzi wa Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Kishapu gharama yake itakuwa 1.5 billion, lakini ukiangalia gharama hizi zinazidi mara tatu ujenzi wa vituo vya afya ambavyo vimekubaliwa na Serikali.

Mheshimiwa Spika, nataka nijielekeze katika Jimbo langu la Mwibara kwa sababu muda ni mfupi. Naomba katika Jimbo la Mwibara tupate maji kwa sababu licha ya kuzungukwa na robo tatu ya Ziwa Viktoria lakini maeneo mengi bado hayana maji ya kutosha.

Mheshimiwa Spika, vituo vya afya vilevile ni tatizo kubwa. Katika Kata za Nasimo, Kibara, Chitengule, Igundu, Nampindi, Kwilamba, Namuhula, Butimba na Nyamiholo bado hakuna huduma nzuri za afya. Katika maeneo hayo wananchi wamejitahidi sana kujenga maboma ya zahanati. Serikali iliahidi kwamba ingemalizia, naomba Serikali itekeleze na yenyewe wajibu wake.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ni katika barabara. Barabara nyingi za Mwibara hazipitiki lakini hasa nitazungumzia barabara moja ambayo inatoka katika Kijiji cha Buguma - Chigondo haipitiki kabisa kwa sababu mkondo wa maji umekatisha katikati ya barabara. Kama leo nikiongozana na Waziri wa TAMISEMI akienda kuona jinsi ambavyo wanawake wanavuka pale sidhani kama atafurahi. Kwa hiyo, naomba barabara hii na yenyewe ipewe umuhimu katika kujengwa.

Mheshimiwa Spika, lingine ni elimu. Tuna matatizo ya vyumba vya madarasa, maabara, maktaba na nyumba za walimu. Vilevile maboma mengine ambayo wananchi wamejenga hajayakamilika, naomba Serikali itusaidie.

Mheshimiwa Spika, tatizo lingine ni kivuko kati ya Nasimo na Kisiwa cha Nafuba. Naomba Serikali itufikirie kutusaidia katika eneo hili.

Mheshimiwa Spika, lakini tatizo lingine ni fidia kwa wananchi ambao walipisha mradi wa barabara ya kutoka Bulamba - Kisorya. Hawa nao bado hawajalipwa, naomba vilevile tufikiriwe.

Mheshimiwa Spika, lingine ni wakulima wa pamba. Hawa ni karibu mwaka wa tatu sasa hivi hawajalipwa pesa zao. Nafikiri Wizara husika inaweza kuangalia namna ya kuwasaidia.

Mheshimiwa Spika, katika jimbo langu ajira ziko katika maeneo makubwa mawili, kwanza ni kilimo. Bahati nzuri tunazungukwa na Ziwa Viktoria, naomba tupewe skimu za umwagiliaji maji na vilevile tupate mikopo ya matrekta.

Mheshimiwa Spika, lakini sekta nyingine ni uvuvi. Sasa hivi samaki wamekuwa wajanja huwezi ukawavua kwa kutumia zana za kizamani. Kwa hiyo, naomba Serikali iangalie namna ya kutusaidia kupata zana za kisasa kuliko Maafisa Samaki au Maafisa Uvuvi kuendelea kuwakamata wavuvi wetu kwa kutumia zana za zamani.

Mheshimiwa Spika, kitu kingine naiomba Serikali kuangalia ulipaji wa madeni kwa wale waliotoa huduma Serikalini. Kwa mfano, nina kampuni mbili za jimboni kwangu; moja ni Swahili Ceramics, hawa wanaidai TBA zaidi ya milioni 139 kuanzia mwaka 2017 hawajalipwa, naomba Serikali ichukue hatua. Kampuni nyingine ni Wajenzi Enterprises ambao wanaidai Halmashauri ya Gairo milioni 10.5. Hawa nao wanasumbuliwa, naomba nao waangaliwe.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia halmashauri ya kwetu ambayo ni ya Majimbo mawili ya Mwibara na Bunda Vijijini; ili uweze kwenda katika Jimbo la Bunda Vijijini inabidi uvuke Jimbo la Bunda Mjini. Ushauri wangu naomba Bunda Vijijini na Bunda Mjini wawe katika halmashauri, moja sisi Mwibara tubaki peke yetu.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa muda huu, naomba na mimi niunge mkono hoja hii. (Makofi)