Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Ally Mohamed Kassinge

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii kwanza kukushukuru binafsi kwa kuniona. Pili, kushukuru kwa hotuba nzuri ya Wizara ya Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa ikiwa ni sambamba…

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge tusikilizane, huyu anayeongea ndiye aliyechukua Jimbo la yule Mbunge ambaye alikuwa anajiita Bwege. Sasa mbadala wake ni Mheshimiwa Kassinge, karibu sana hiyo ndiyo bunduki mpya ya CCM. (Makofi)

MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Spika, niendelee kupongeza Ofisi ya Rais, TAMISEMI, kwa mawasilisho ya hotuba ya bajeti, lakini kwa kuaminiwa na mamlaka katika timu zote kuanzia Mheshimiwa Waziri na Wasaidizi wake, lakini pia Katibu Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo langu la kwanza la uchangiaji ni kuishauri Ofisi ya Rais, TAMISEMI kuja na sera ya ugatuaji ili maeneo ya mgawanyo wa madaraka katika maeneo yote ya siasa, utawala, fedha yabainike baina ya Serikali Kuu na Serikali za Mitaa.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, katika eneo la mapato ya halmashauri, kuna eneo la mapato ya ushuru wa mazao produce cess. Ushuru huu umekuwa ukitofautiana kati ya halmashauri moja na halmashauri nyingine. Niishauri Ofisi ya Rais, TAMISEMI iweze ku-harmonies ili ushuru huu uwe sawa na halmashauri zote na kuondoa mgogoro au mgongano ikiwa ni sambamba na kurudisha asilimia tano ya ushuru wa mazao badala ya asilimia tatu ya sasa hivi, kwa sababu utafiti umebainisha kwamba wanaochangia halmashauri katika ushuru huo wa mazao asilimia tatu ni wanunuzi na si wakulima.

Mheshimiwa Spika, pili, kuna eneo hili la property tax ambalo baadhi ya Wabunge hapa wamelizungumzia. Kimsingi hili ni eneo la ushuru au mapato ya Local Authority, lakini hali ilivyo sasa hivi inakusanywa na halmashauri lakini ina hesabika kuwa ni mapato ya Serikali Kuu. Nishauri eneo hili lirudishwe halmashauri na hayo ni mapato ya halmashauri ili zikajenge barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kuna ushuru wa halmashauri wa kimazoea (traditional) wa siku nyingi, ushuru mdogo mdogo wa wajasiriamali, wauza vitumbua, wauza mahindi ya kuchoma na kadhalika.

Lengo la Serikali kutoa vitambulisho kwa wajasiriamali lilikuwa ni lengo zuri na kazi hii inafanywa vizuri na Watendaji wa Halmashauri kukusanya fedha kupitia vitambulisho 20,000 kwa mwaka, lakini mapato yanahesabika si mapato ya halmashari bali ni mapato ya Serikali Kuu, yanakwenda Hazina moja kwa moja. Niishauri Ofisi ya Rais, TAMISEMI na Serikali kwa ujumla, mapato yanayotokana na wajasiriamali wadogo wadogo yarudi halmashauri yakajenge barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kushauri masuala ya kisera sasa nije katika eneo langu la uongozi na uwakilishi kwa maana ya changamoto zilizopo katika Jimbo la Kilwa Kusini, nikianza na eneo la barabara zinazohudumiwa na TARURA. Naomba hapa nitoe takwimu; kuanzia mwaka 2017/2018 – 2019/2020, Halmashauri ya Kilwa imekuwa ikipata fedha za barabara billioni moja plus kidogo hivi, lakini kuanzia 2021 imekuwa ikishuka ni mpaka kufikia Sh.984,000,000 na hali hii imeendelea kushuka mpaka bajeti hii tuliyonayo. Kwa hali halisi ya urefu wa barabara za Kilwa ambazo ni zaidi ya kilomita 1,000, Sh.984,000,000 hazitoshi.

Mheshimiwa Spika, nashauri tuongeze bajeti hii ili ikahudumie barabara zile. Hapa naomba nizungumze barabara mahsusi na naomba hizi zipewe kipaumbele. Barabara ya kutoka Hoteli Tatu - Pande, Hoteli Tatu – Lihimalyao, sisi Wanakilwa hii ni barabara ya kimkakati inaenda kuhudumia wakazi wapatao 30,000 ambao ni wazalishaji wakubwa wa korosho, kwa hiyo itakuwa ni barabara ambayo itajenga uchumi katika eneo hili. Nishauri kupitia Ofisi ya Rais, TAMISEMI, barabara isiingie katika utaratibu wa maintenance, badala yake iingie katika utaratibu wa development na itengewe fedha za kutosha ili ipitike kipindi chote cha mwaka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho Sekta ya Afya. Hospitali yetu ya Wilaya ya Kilwa imechakaa vya kutosha…

SPIKA: Kengele imeshagonga. Ahsante sana Mheshimiwa Kassinge.

MHE. ALLY M. KASSINGE: Kwa hiyo tunaomba hospitali ikarabatiwe, kama si kujenga hospitali mpya.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru na naunga mkono hoja. (Makofi)