Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Luhaga Joelson Mpina

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisesa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi uliyonipa. Kwa sababu ya changamoto ya muda, niende moja kwa moja kwamba kuna baadhi ya Halmashauri zetu ambazo zina wazabuni na wakandarasi ambao walishatoa huduma muda mrefu, mpaka leo hii hawajalipwa fedha zao. Hii ni kutokana na zile Halmashauri kuelemewa na changamoto za kimapato. Kwa hiyo, wameshindwa kuwalipa wakandarasi na wazabuni ambao walishatoa huduma. Matokeo yake wananchi hawa wanateseka sana, wanauza nyumba zao, wanakimbia miji yao, wamefilisika na wana mateso makubwa. Watu walishatujengea shule tayari zinafanya kazi, barabara zinafanya kazi, miradi ya maji inafanya kazi lakini hawajalipwa na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ombi langu, Waziri aratibu madeni yote ya Halmashauri zilizoelemewa kulipa madeni ya wananchi hawa ili wazabuni na wakandarasi wapate haki yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili, tunao Waheshimiwa Madiwani, Waheshimiwa Wenyeviti wa Vijiji na Waheshimiwa Wenyeviti wa Vitongoji. Tunakubaliana sote hapa umuhimu wa hawa viongozi. Hata hivyo, viongozi hawa ambao ni Madiwani wetu ambapo leo tunaidhinisha shilingi trilioni 7.68 waende kuzisimamia, hawalipwi. Malipo ya Waheshimiwa Madiwani ni madogo mno kiasi kwamba hawawezi kuhimili na usimamizi huo wala kukidhi mahitaji ya shughuli zao wanazozifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wenyeviti wetu wa Vitongoji na Vijiji hawalipwi kabisa. Tatizo ni nini? Viongozi hawa wame- sacrifice muda wao wote kwa ajili ya kuitumikia Serikali, wanachangisha michango; tukitaka madarasa, wao ndio wanaochangisha, tukitaka zahanati wao ndio wanaofanya; tukitaka mkutano wa hadhara, wao ndio wanaofanya; kwa nini hawalipwi viongozi hawa? Sababu za kutokulipwa ni nini? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mtendaji wa Kijiji analipwa, Watendaji wengine wote kwenye Kijiji hata 30 wanalipwa, lakini Mwenyekiti wa Kijiji mshahara wake unakosekana. Ni nani huko Serikalini ambaye alishakataa hawa viongozi wasilipwe mishahara yao inayostahili kulingana na kazi wanazozifanya? Nashauri Serikali ifanye maamuzi ya kuwalipa hawa viongozi ili nao waweze kutoa huduma sawasawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la mwisho, tumezungumzia kuhusu kupeleka shilingi trilioni 7.68 kwenye Halmashauri zetu. Kwanza nikubaliane kwamba hizi fedha ni ndogo kulingana na mahitaji tuliyonayo; mahitaji ya barabara, maji, zahanati na huduma mbalimbali kwenye maeneo yetu ya Serikali za Mitaa na kwamba hili ndiyo eneo muhimu sana ambalo wananchi wetu wanapata huduma moja kwa moja.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, tunapeleka fedha katika eneo ambalo tayari lina changamoto nyingi. Kama tulivyoona taarifa ya CAG kwamba, hati safi zinazidi kuporomoka, hati zenye mashaka zinazidi kuporomoka na kwenda kwenye hati mbaya. Maana yake tunapeleka fedha eneo ambalo lina changamoto kubwa sana ya usimamizi.

Mheshimiwa Spika, sasa hizi changamoto kwa nini zimekuwa za kudumu? Nadhani hapa kuna kazi ambayo haijafanyika sawasawa. Hii kazi tukitaka tuifanye sawasawa lazima tuzifanye kikamilifu zile activities zote ambazo zinazohusika ili tuweze kukomesha. Haiwezekani Bunge hili kila likikutana linazungumzia watu kutosimamia fedha vizuri na watu kupata hati chafu.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, leo tunaweza tukazungumza Halmashauri zilizopata hati mbaya na chafu, lakini unakuta watumishi wanaohusika hata na kuandaa hizi hawapo. Unakuta hakuna wahasibu, hakuna wakaguzi, unapataje hati safi katika mazingira haya? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mkaguzi hapa anasema, nafasi 510 zinakaimiwa. Kwa nini nafasi 510 zikaimiwe? Kwa nini tuwe na upungufu mpaka wa watumishi Wakuu wa Idara, Wakurugenzi, Wakuu wa Vitengo; tunakuwaje na upungufu na watu hawa? Kwa nini hizi nafasi zisizibwe mara moja? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, hivi kwa nini tuendelee na utaratibu wa vetting na mambo ya seniority katika kuajiri? Hivi kuna shida gani Wakurugenzi, Wakuu wa Idara na Wakuu wa Vitengo wakapatikana kwa njia ya ushindani tu? Tunavijana wengi competent sasa hivi. Sasa unafanya vetting, miaka mitatu unampata mtu uliyemfanyia vetting miaka mitatu, halafu miezi sita unamtumbua kwa kutokuwa na uwezo. Kwa nini tusifanye ushindani? Wakafanya oral, wakafanya written, tukapata competent? Vijana tunao wa sekta zote, competent kabisa. Kwa nini twende na mambo haya?

Mheshimiwa Spika, nafasi hizi zijazwe na tusikubali kuwa na upungufu mpaka wa watalaamu? Mtu wa kusoma X-Ray ni mmoja, halafu unakuwa upungufu wa huyo huyo, kweli! Meatu pale leo miaka mitatu X-Ray haifanyi kazi. Ipo pale, haifanyi kazi, hakuna mtaalam wa kusoma.

Mheshimiwa Spika, la pili, tunao hawa wakaguzi wetu, hivi tunapate hati chafu? TAMISEMI mnapataje hati chafu wakati una Kitengo cha Ukaguzi ambacho kinatoa taarifa kila robo mwaka? Mnazisimamiaje hizo taarifa? Mnazi- coordinate vipi zile taarifa za ukaguzi mpaka mwingie kwenye hati chafu? Hapa kuna tatizo kubwa la usimamizi.

Mheshimiwa Spika,...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Luhaga.

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana.