Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Stella Ikupa Alex

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. STELLA I. ALEX: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Naomba nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa ajili ya uzima na uhai ambao anaendelea kunipatia kila siku.

Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii kumtakia heri Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mpendwa wetu mama Samia Suluhu Hassan.

Mheshimiwa Spika, niendelee kumuombea kwa Mwenyezi Mungu siha njema, hekima na maarifa ya kuendelea kuliongoza Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, naomba niipongeze Serikali kwenye maeneo mengi, kwenye eneo la watu wenye ulemavu kwa yale ambayo yamekwisha kufanyika na yale ambayo yanaendelea kufayika. Kwanza, naomba nianze na eneo la kamati za watu wenye ulemavu. Serikali imekimbizana na kuhakikisha kwamba kamati za watu wenye ulemavu zinaundwa kwenye maeneo mengi ya nchi yetu lakini bado kuna maeneo ambayo kamati hizi hazijaundwa. Niishauri Serikali ihakikishe kwamba zoezi hili la uundwaji wa kamati za watu wenye ulemavu linakamilika nchi nzima. Pia kwa yale maeneo ambayo tayari kamati hizi zimekwisha kuundwa basi Serikali iziwezeshe ili ziweze kufanya kazi kwa mujibu wa sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kamati hizi ni muhimu sana. Mambo mengi ambayo yanaendelea huko chini ambayo hayagunduliki kwenye eneo la watu wenye ulemavu yatakuwa solved kama hizi kamati zitaanza kufanya kazi kama ambavyo zilikuwa zimetarajiwa na sheria. Kwa hiyo, Serikali kupitia TAMISEMI iweze kuliona hili na kutenga fedha ili kamati hizi ziweze kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niipongeze Serikali na kuishukuru sana na watu wenye ulemavu wamenituma niliseme hilo kwa kuweza kusikia kilio chao na hatimaye kuweza kufanya marekebisho ya kanuni za mikopo ya halmashauri zetu. Takumbukwa kwamba katika Bunge la Kumi na Moja, Waheshimiwa Wabunge pia waliweza kuishauri sana Serikali kwamba ione namna ya kufanya marekebisho ili basi mtu mwenye ulemavu mmoja mmoja aweze kupata mkopo. Suala hili Serikali yetu sikivu imekwisha kulifanyia kazi. Kuna swali ambalo nilileta lakini sasa sioni hata umuhimu tena wa swali hili kuweza kujibiwa ndani ya Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Spika, naomba kuishauri Serikali kwamba iendelee kuzihimiza halmashauri zetu kutenga fedha lakini pia kununua mafuta ya watu wenye ualbino na hatimaye kuyasambaza kama ambavyo maelekezo yamekuwa yakitolewa mara kwa mara. Zipo halmashauri ambazo zinatenga fedha lakini kutenga tu haitoshi. Mtu anaishia kutenga, ukifuatilia kweli fedha imetengwa, lakini mwisho wa siku fedha zile hazikuwahi kufanya kazi ambayo ilikusudiwa. Pia kuna maeneo mengine unakuta mafuta yananunuliwa lakini hayawafikii walengwa. Kwa hiyo, niombe Serikali iweke mkazo mkubwa kwenye eneo hili la mafuta kwa watu wenye ualbino.

Mheshimiwa Spika, nimekuwa nikisema na naomba nirudie tena; vifaa hivi visaidizi kwa sisi watu wenye ulemavu ni kama chakula. Kama vile ambavyo binadamu wa kawaida anahitaji kula, vivyo hivyo mtu mwenye ulemavu hivi vifaa kwake inakuwa ni kama chakula ambacho akikikosa kwa kweli inakuwa inamhatarishia maisha yake. Nimeshuhudia mimi mwenyewe kwa macho yangu kwa sababu nimekuwa kwenye eneo hili kwa muda mrefu; watu wenye ualbino wanateseka na kansa za ngozi. Hata kama itatokea mtu ukaona picha yenyewe kwa kweli sijui unaweza ukafanyaje lakini ni muhimu sana haya mafuta yakawafikia wenzetu.

Mheshimiwa Spika, pia elimu kubwa iendelee kutolewa kwa watu wenye ualbino ili iwasaidie na/ama iwawezeshe ni jinsi gani pia wanaweza wakajikinga na hizi kansa za ngozi. Kwa sababu unakuta mtu mwingine mafuta amepaka ndiyo lakini nguo aliyoivaa inamhatarishia maisha kwa sababu anakuwa anajiachilia kwenye mionzi ya jua.

Mheshimiwa Spika, naomba niiombe Serikali kwenye eneo la ajira na hasa TAMISEMI, zile ajira zikiwa zinatangazwa basi itolewe angalau hata idadi fulani maalum kwa watu wenye ulemavu. Kwa mfano, sasa hivi kuna ajira 6,000, hata zikatengwa nafasi 300 ama 200 kwamba hizi ni kwa ajili ya watu wenye ulemavu, kama hawatapatikana basi zitaendelea kuchukuliwa na watu wengine.

Mheshimiwa Spika, kwa harakaharaka naomba nizungumzie suala la miundombinu kwenye shule zetu na hasa vyoo. Vyoo vimekuwa ni tatizo kubwa sana, watoto wenye ulemavu wanapata shida, kwa hiyo, Serikali iendelee kuweka nguvu kubwa na kutenga fedha kuhakikisha kwamba angalau basi katika kila shule kunakuwa na tundu moja ambalo litamuwezesha mwanafunzi mwenye ulemavu kuweza kulitumia.

Mheshimiwa Spika, pongezi zangu zienda kwa Serikali, kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri katika aya ya 73, 74 mpaka 75 imeonesha ufaulu wa watoto wenye ulemavu. Pia kuna ongezeko la uandikishwaji na fedha ambazo zimeweza kununua vifaa visaidizi ambazo ni takribani shilingi bilioni tatu.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema haya machache, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)