Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Dr. Jasson Samson Rweikiza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukoba Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. JASSON S. RWEIKIZA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili nichangie hoja hii. Kwanza napenda kuwapongeza sana Waziri, Mheshimiwa Ummy Mwalimu na Manaibu wake Mheshimiwa Silinde na Mheshimiwa Festo kwa kazi nzuri ambayo wamekwisha kuifanya hadi sasa ambayo inaonekana.

Mheshimiwa Spika, nipende pia kuipongeza Serikali ya CCM kwa kazi kubwa inayofanyika kwenye maeneo yetu. Kazi zinaonekana, shule zinaonekana hata kama zina matatizo madogo madogo, vituo vya afya kwa maana ya hospitali, zahanati, hospitali za wilaya na vituo vya afya, barabara zinatunzwa, zinarekebishwa, tunasonga mbele.

Mheshimiwa Spika, pamoja na pongezi hizo niseme kwamba tunahitaji kuongeza jitihada na kuboresha miundombinu tuliyonayo. Sasa niongelee jimbo langu, pale kwenye jimbo langu, kuna Kata moja inaitwa Lukoma, haina shule ya sekondari kwa hiyo, wanafunzi kutoka pale Lukoma wanatembea kilomita 19 kwenda shule jirani kutafuta elimu. Nasema jirani kwa sababu ndiyo inayofuata lakini siyo jirani kilomita 19 kwenda tu, kurudi 19, jumla 38 kwa siku moja mtoto mdogo wa form one, wa form three au kidato chochote, anatembea kilomita 19 kwenda, hivyo hivyo kurudi, kwa hiyo kwa siku anatembea kilomita 38 karibu 40, ambayo ni adha kubwa sana.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba hii kata na yenyewe ipatiwe shule, shule tulishajenga tayari pale, tumefika katikati hapo kwenye ukuta, lakini hatuna uwezo wa kumalizia, wananchi wamechanga wameishiwa nguvu, tunaomba Serikali itoe msaada unaotakiwa pale iki shule hii ikamilike na hawa wananchi wapate shule ya kata, kama ilivyo sera ya CCM kila kata iwe na shule ya sekondari.

Mheshimiwa Spika, katika Jimbo zima la Bukoba Vijijini, hatuna shule ya A level, ya form five na form six, sasa hii nayo ingawa ngazi hii ni ya kitaifa, lakini ni vizuri tukawa na shule ya namna hiyo kusudi tuweze kupata huduma inayotokana na shule hiyo. Tuna shule za sekondari za form one hadi form four nyingi zaidi ya 30, lakini hatuna shule ngazi ya form five na form six. Kwa hiyo, wanafunzi wanapomaliza darasa la kumi na mbili hawawezi kusoma pale pale mpaka watafutiwe sehemu nyingine, nje ya mkoa au nje ya jimbo ambayo nayo inakuwa ni adha kubwa kwenda mbali.

Mheshimiwa Spika, nikiwa bado kwenye eneo la shule la elimu, tumejenga shule nyingi kwenye nchi hii, za kata za sekondari na zingine zilikuwepo, nyingi zimekuwa na matatizo kidogo kidogo ambayo yanasababisha huduma isiwe nzuri. Niongele sasa kwenye vyoo, shule nyingi hazina vyoo vizuri au havina vyoo kabisa, wanafunzi wanakwenda maporini hata Walimu na watumishi wengine wanakwenda kwenye maeneo ambayo siyo salama. Pale nina Shule moja inaitwa Kaishozi Sekondari, shule hii ni kubwa ni ya siku nyingi siyo ya kata, iko siku nyingi, lakini haina choo, choo kimeharibika siku nyingi na wanafunzi wanapata tabu sana inapofika kuwa na haja ya kwenda chooni.

Mheshimiwa Spika, nimalizie na suala la TARURA; Wabunge wengi wamezungumzia suala la TARURA, TARURA imekuwa ni mkombozi mkubwa wa barabara za vijijini na mijini zile ambazo siyo za TANROAD, lakini TARURA haina fedha kama walivyosema Wabunge wenzangu, ina fedha kidogo, nafikiri mpaka leo wanapewa asilimia 30 ya Road Fund (Mfuko wa Barabara), TANROADS wanapewa asilimia 70 na TARURA asilimia 30. Sasa fedha hizi ni ndogo sana, TARURA wana kilomita zaidi ya laki moja na kumi ambazo wanazihudumia ambazo kila mwaka zinaongezeka na ni barabara mpya, ndogondogo lakini za muhimu sana.

Mheshimiwa Spika, hizi barabara ni muhimu kwa sababu ndizo zinawapeleka watu mbalimbali mashambani, zinapeleka pembejeo zinazoenda mashambani huko, zinawasaidia wanafunzi kwenda mashuleni, zinawasaidia wananchi kwenda katika vituo vya afya kupata huduma za afya, bila barabara inakuwa ngumu sana. Kwa hiyo, TARURA fedha hazitoshi.

Mheshimiwa Spika, hasahasa niongee Jimbo langu la Bukoba vijijini pale kama ilivyo majimbo mengine ya Kagera tuna mvua nyingi kwa hiyo ikija mvua moja au mbili barabara nyingi zinashindwa kupitika zinakuwa hazipitiki hazifai kabisa. Kwa hiyo, tunaomba kwamba tunapopangiwa hela ya TARURA iwe ndogo iliyopo tunatafuta namna ya kuiongeza hiyo ndogo iliyopo Kagera iangaliwe kwa jicho la pekee kwamba ipewe fedha za kutosha kusudi barabara ziweze kupanuliwa kutengenezwa na madaraja yaweze kufunguliwa nakupitika muda mwingi wa mwaka.

SPIKA: Ahsante sana!

MHE. JASSON S. RWEKIZA: Mheshimiwa Spika, nakushuru sana naunga mkono hoja. (Makofi)