Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Anthony Peter Mavunde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Dodoma mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. ANTHONY P. MAVUNDE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi. Nami nianze kwanza kuwapongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na Manaibu Mawaziri kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya na ninaamini wataendelea kuifanya katika kuimarisha Ofisi ya Rais, TAMISEMI. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijielekeze katika kuishauri Serikali katika namna bora ya kuendelea kutafuta fedha ya kuifanya TARURA iweze kufanya kazi vizuri. Nakubaliana na michango iliyotolewa na Mheshimiwa Mussa Zungu na Mheshimiwa Moshi Kakoso ya namna bora ya kuweza kupata fedha za kuifanya TARURA ifanye kazi. Kifungu cha 8(1) cha Government Notice No. 211 ya mwaka 2017 ilitengeneza utaratibu wa namna ambavyo TARURA watapata fedha (source of funds).

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijielekeze katika jambo ambalo halijasemwa humu lakini naamini linaweza litakaleta tija. Kabla ya TARURA, Halmashauri za Miji, Manispaa na Wilaya zilikuwa zikitenga bajeti ya barabara kupitia Idara ya Ujenzi. Sioni ni kwa nini zisiendelea kufanya hivyo kwa sababu tunamhudumia Mtanzania mmoja. Kama waliweza kuzitenga hapo awali, kwa nini wasiendelee tena kutenga? Ndiyo maana namwomba Mheshimiwa Waziri waende kulisimamia jambo hili na inawezekana kabisa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais wakati anawaapisha Mawaziri, alisema hili pia. Waende wakafanye coordination nzuri ndani, Halmashauri zitenge fedha, vilevile na fedha ya TARURA itaendelea kutumika. Lengo hapa ni kuhakikisha mfuko huu unaendelea kuwa na fedha za kutosha. Naamini Mheshimiwa Waziri atakuwa ameshakutana na hii nyaraka, ukienda ofisini, uko waraka ambao aliutoa aliyekuwa Katibu Mkuu, Iyombe ya kuzitaka Halmashauri za Majiji, Manispaa na Wilaya kutenga hizi fedha. Mheshimiwa Waziri naomba isiwe hiyari, iwe lazima fedha hizi zikatengwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili ambalo nataka niishauri Serikali ni katika eneo la mapato ya malipo ya mbele kwenye ardhi (premium). Katika miji yetu yote zoezi la upimaji wa viwanja na urasmishaji linaendelea, lakini ndani ya zoezi hilo wananchi huwa wanalipa fedha ya premium ambayo imeelekezwa katika kuboresha huduma za kijamii na hasa miundombinu. Kwa nini fedha hii isitengewe utaratibu mzuri ikaingia TARURA kwa ajili ya kuweza kusaidia kwenye majukumu ya TARURA? Kwa sababu hivi sasa inabaki katika Halmashauri na kupangiwa matumizi mengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, naamini kabisa, kwa sababu katika upimaji wa viwanja vipya inatozwa asilimia 2.5 malipo ya premium na katika urasmishaji ni 1%, hizi ni fedha nyingi sana. Tuna uwezo pia wa kutumia chanzo hiki kwa ajili ya kuifanya TARURA iwe na mfuko ambao utafanya kazi zake vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, bahati nzuri Mheshimiwa Waziri una uwezo wa kukaa na Waziri wa Ardhi mkakubaliana tu, vizuri kabisa namna ya utaratibu huu kwa sababu mwenye mamlaka kwa mujibu wa Kifungu cha 31(1) cha Sheria ya Ardhi ni Waziri wa Ardhi. Mkukubaliane kwa pamoja ukawekwa utaratibu mzuri ili fedha hizi ziingie katika TARURA na wafanye kazi ya kutuhudumia Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo nataka nilichangie hapa, Dodoma hivi sasa ni kati ya majiji ambayo yanakuwa kwa kasi sana. Kwa mtandao wa barabara za lami, Dodoma ndiyo inaongoza kuliko jiji lolote Tanzania nzima kwa kuwa na mtandao mrefu wa barabara za lami. Huu tuliupata kupitia mradi wa TSCP.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna mradi mwingine ambao unakuja, baada ya kuona mafanikio ya TSCP kuna mradi wa TACTIC hatujui umekwamia wapi? Tunaiomba Serikali, wakati Mheshimiwa Waziri anakuja kujibu hoja, atueleza jambo hili kwa sababu lina manufaa makubwa sana. Miradi hii ikitekelezeka, inaboresha miundombinu, inachochea uchumi katika eneo husika, inakuza na ajira.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiliona leo soko la Ndugai, ukiona stendi ya ma-bus pale ni mradi wa TSCP, una mchango mkubwa sana. Kwa hiyo, nitaomba Mheshimiwa Waziri akija atuambie umefikia hatua gani kwa sababu tumesubiri muda mrefu katika jambo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, huu mradi ukikamilika, unakugusa wewe pale kwenye Jiji la Mbeya, unamgusa Naibu Waziri Tanga, unanigusa mimi hapa Jiji la Dodoma, unakwenda Arusha, Mwanza na matokeo yake ni makubwa sana. Pia tuna jambo ambalo linaendelea…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ANTHONY P. MAVUNDE: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)