Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Aleksia Asia Kamguna

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. ALEKSIA A. KAMGUNA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Kwa heshima na taadhima, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa sisi sote kutuwezesha kuwa salama. Pia nawashukuru Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa kuwasilisha bajeti yao ambayo ni nzuri, inaleta mwelekeo pamoja na changamoto zake, lakini inaleta matumaini katika Taifa letu. Tunasema ahsante.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukweli kwetu tuna matatizo, Mkoa wa Morogoro ni mkoa wenye bahati, tumepata miundombinu ya kimkakati, lakini kuna matatizo mengi katika mkoa huu. Naomba kwa heshima na taadhima nizungumzie huo mkoa. Mkoa wa Morogoro ni mkubwa sana na wote wanakiri ni mkoa wa pili katika nchi yetu, lakini tumepata neema, tuna ardhi nzuri, kadhalika na kadhalika, lakini pamoja na hiyo ardhi nzuri imeguka sasa imekuwa shubiri inatutesa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini nasema hivi? Nichukue mfano wa Wilaya ya Malinyi; wilaya hii iko bondeni, yaani mvua ikinyesha Iringa sisi kwetu ni maji. Ninavyoongea leo hii, siwezi nikatoka hapa Dodoma kwenda kwetu sina kwa kupita, kwa maana wilaya nzima imejaa maji. Kwa kuwa imejaa maji hatuna miundombinu ya barabara, hali ni mbaya, yaani Malinyi waiangalie kwa jicho la huruma, wengine wote wanalilia lami lakini sisi tunalilia kufika kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Malinyi ni wilaya mpya, ni wilaya ambayo imetokana na Wilaya mama ya Ulanga imeanzishwa mwaka 2015, lakini kama nilivyotangulia kusema barabara hatuna, yaani TARURA kama inawezekana, wote wanasema asilimia 40, basi kwetu sisi iwe asilimia 60 kwa ili iweze kuisimamisha Malinyi. Malinyi hatuna madaraja na hatuna hata barabara ya changarawe. Mheshimiwa Waziri na wasaidizi wake, angekuwa amefika Malinyi angenielewa ni nini nazungumza.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi hatuna njia ya kuingia Malinyi; tukifika sehemu moja ambayo inaitwa Misegesi kwenda Malinyi huwezi kufika, kuna hitaji daraja na halipo. Kuna sehemu nyingine ya Malinyi kuelekea Lugala ambako ndiko kuna Hospitali ya Misheni ambayo tunaitegemea, huwezi kufika kwa sababu barabara hakuna. Pia kuna sehemu nyingine ambayo inaitwa Malinyi Lugala ndio huko kwenye Hospitali karibu, lakini huwezi kufika. Sasa huyo mtu wa Malinyi anaishije. Naomba Mheshimiwa Waziri avae viatu vya watu wa Malinyi, kwa kweli Malinyi tuna matatizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wabunge wengi wanasema kwamba wanahitaji TARURA kwa ajili ya barabara na sisi watu wa Malinyi tunasema TARURA ni uhai, kwa maana bila ya TARURA sisi hatuwezi kuishi na kweli maisha yetu ni magumu.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, Malinyi tuna matatizo kwa upande wa afya. Hatuna barabara, hatuna dispensary, hatuna Hospitali ya Wilaya, Hospitali ya Wilaya imejengwa, kuna kipindi walitoa mwongozo kwamba, lazima hospitali zote waanze kutibia wagonjwa wa OPD, ndio hicho kimeanzishwa, lakini kwa ujumla hospitali ya Serikali hakuna. Sasa kama hospitali ya Serikali hakuna, miundombinu ya barabara hakuna, huyu mwanamke ambaye amepewa kazi na Mungu ya uzazi, anawezaje kutoka kwake afike kwenye hospitali na kama atafika kwenye hospitali, kwanza hospitali yenyewe haipo, anaenda wapi? Tunaomba pia Mheshimiwa Waziri kwa upande wa afya atuangalie, hatuna barabara, hatuna hospitali, kama mama inaumiza. Naomba watuangalie Malinyi. Leo sina mengi ya kusema zaidi ya kuomba yaani nimesimama kwa ajili ya kuomba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna sehemu nyingine ya Wilaya ya Ifakara kuna hospitali moja inatiwa Man’gula B. Hapa limejengwa jengo zuri kabisa la Kituo cha Afya katika Mkoa wa Morogoro, lakini hakuna sehemu ya operation. Ni kituo cha afya kikubwa na kizuri na Serikali imetumia pesa nyingi. Sasa tunaweka kile kituo bila sehemu ya wazazi na wazazi wanafariki, tunaomba nalo liangaliwe, bado Morogoro ina changamoto. Morogoro ni kubwa na lazima TAMISEMI waiangalie kwa jicho la pekee wakilinganisha na mikoa mingine, kwa sababu kama ni kubwa ina maana na mahitaji yake yatakuwa makubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakuja upande mwingine wa utawala; hili naomba niwaeleze, sasa hivi naona kuna mikoa mingi au Wilaya nyingi kuna matatizo au ina changamoto, unakuta Mkuu wa Wilaya anagombana na Mkurugenzi, anagombana na Mbunge, sasa kunakuwa tafrani, nafikiri viongozi wenzangu watakubaliana nami kwamba katika wilaya nyingi au halmashauri nyingi hazina amani, kuna vurugu. Kwa nini kuna vurugu? Yawezekana kwa mawazo yangu uteuzi tunaoufanya sasa hivi wa Wakuu wa Wilaya labda turudi nyuma, mwanzo tulikuwa tunawachukua hawa Maafisa Tarafa, wanakuwa na uzoefu, wanakuwa karibu na Wakuu wa Wilaya, ukimteua kuwa Mkuu wa Wilaya anajua zile ethics za uongozi, lakini hawa wa sasa hivi kama wanawatoa tu shuleni, wanawapeleka wanakuwa Wakuu wa Wilaya, matokeo yake kunakuwa conflict of interest, matokeo yake wilaya zinakuwa na vurugu. Hilo nimeliona, naomba tuliangalie kwa umakini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hayo machache, nakushukuru na naunga mkono hoja. (Makofi)