Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Timotheo Paul Mnzava

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Korogwe Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Namshukuru sana Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema aliyetujaalia uzima. Kipekee nampongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa uteuzi wa kuwa Waziri kwenye Wizara hii. Odo Ummy tuna imani kubwa sana nawe, tunaamini kwamba utaifanya kazi yako vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawapongeza Waheshimiwa Manaibu Waziri kwa kuendelea kuaminiwa, lakini pia najua mna timu nzuri sana TAMISEMI. Mmepata Katibu Mkuu mzuri, Profesa Shemdoe, mtu mahiri, mtu makini san ana pia anaye Naibu Katibu Mkuu kama ndugu yangu Ndugu Gerald Mweri, tuna uhakika na kazi wanayoifanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie muda huu kushauri mambo machache kwenye eneo la TAMISEMI. Jambo la kwanza ni upande wa TARURA. Waheshimiwa Wabunge wengi wamezungumza kuhusu TARURA, nami naendelea kusema na tutaendelea kusema kwa sababu ni kitu muhimu sana kwenye maendeleo ya Halmashauri zetu hasa kwa sisi ambao tunatoka maeneo ya vijijini. TARURA inafanya kazi nzuri, lakini lazima tukubaliane kwamba ziko changamoto zinahitaji kufanyiwa kazi ili kazi hii nzuri inayofanywa na TARURA iweze kuwa na matokeo mazuri kwa watu wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto kubwa ya kwanza ni fedha. Tuseme tutakavyosema lakini pesa wanayopewa TARURA ni ndogo, wanahitaji kuongezewa fedha ili waifanye kazi yao vizuri. Jambo hili siyo kwa TAMISEMI tu, ni jambo la Serikali. Tunahitaji Serikali itusikie kwamba tunahitaji kuona TARURA ikiongezewa fedha iweze kufanya kazi zake vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na hoja ya baadhi ya watu wakihoji kwa nini TARURA au barabara zimetolewa Halmashauri na TARURA imesimama yenyewe inajitegemea? Kwa upande wangu, kuirudisha TARURA Halmashauri ni kurudi hatua moja nyuma na wala siwezi kushauri jambo hilo. Ninachokiomba hapa kifanyike kuwe na mahusiano mazuri kati ya Halmashauri ya TARURA.

Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge na Madiwani ndio waliokwenda kuomba kura, ndio tunaojua mahitaji ya wananchi, ndio tunaojua vipaumbele vya watu wetu. Lazima TARURA watushirikishe Halmashauri zetu kwenye kuteua barabara za kufanyia matengenezo. Isiwe hisani kwamba akijisikia aseme, asipojisikia asiseme. Watushirikishe tushauriane ili twende tukaangalie maeneo kulingana na mahitaji na vipaumbele vya watu wetu kwenye Halmashauri zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri kwenye hotuba yako ukurasa wa 118 nimeona unazungumzia mradi wa barabara kwenye maeneo ya uzalishaji hasa kwa maeneo ya kilimo. Umeongelea eneo la kule nyanda za juu kusini peke yake. Yako maeneo mengi ya uzalishaji ambayo yana shida kubwa ya barabara. Katika Mkoa wa Tanga, milima ya Usambara ni maeneo muhimu sana hasa kwa kilimo cha chai. Barabara ni mbovu sana, tunahitaji miradi ya namna hii ifike kwenye maeneo yale pia tuwasaidie wananchi. Tunapoteza chai nyingi sana ya wananchi wetu kwa sababu ya ubovu wa barabara, inachelewa kufika kiwandani, watu wetu wanapata hasara. Tunaomba sana mtusaidie kwenye eneo hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia Mheshimiwa Asenga ameshauri hapa kuhusu vifaa, hata kama siyo kwenye level ya Halmashauri, basi hata kwenye level ya mkoa angalau TARURA kwenye ngazi ya mkoa kuwe na vifaa. Haiwezekani tukipata dharura tuanze kuhangaika kukopa kwa Wakandarasi na mkiwakosa wananchi wapate hasara. Angalau kila mkoa basi kuwe na vifaa, ikitokea dharura wafanye kazi kwa kutumia wataalam tuliokuwanao kwenye TARURA kwa vifaa walivyokuwa navyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2020 Serikali ilitoa maelekezo ya kuhamisha Halmashauri zote ambazo walikuwa wanafanyia kazi kwenye maeneo ambayo ni nje ya maeneo yao ya utawala kwenda kwenye maeneo yao ya utawala. Halmashauri ya Wilaya ya Korogwe ni moja ya Halmashauri ambazo tulihamisha Makao Makuu ya Halmashauri yetu, lakini tuna changamoto kubwa sana ya usafiri kutoka kwenye Tarafa kwenda kwenye Makao Makuu ya Halmashauri mpya tuliyopeleka sasa. Naomba mtusaidie TARURA wawe na programu maalum ya barabara za kuunganisha angalau Tarafa na Makao Makuu hizi mpya za Halmashauri ili wananchi wetu waweze kufika vizuri na kwa urahisi kwenye eneo hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nichangie kwenye upande wa afya. Tunaishukuru Serikali, imefanya kazi nzuri na kazi kubwa sana kwenye Sekta ya Afya. Korogwe tumepata Hospitali ya Wilaya, tumepata Kituo cha Afya cha Mkumbara na sasa tunajenga Kituo cha Afya cha Kerenge, lakini kuna vituo vya afya vikongwe vya muda mrefu. Ninacho Kituo cha Afya kule Korogwe cha Bungu kimejengwa mwaka 1977 mpaka leo hakijawahi kufanyiwa ukarabati, hakina huduma ya upasuaji, kutoka huko kwenda Hospitali ya Wilaya ni zaidi ya kilometa 55. Naomba pamoja na kazi nzuri mnayoifanya tuangalie maeneo haya, tusogeze huduma, tuboreshe vituo hivi vikongwe viweze kufanya kazi yake vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, ziko ahadi za viongozi. Waziri Mkuu alipita Korogwe akaahidi kusaidia ukarabati wa Kituo cha Afya cha Bungu. Aliahidi Kituo kipya cha Afya kule Mashewa, tunaomba ahadi za viongozi zikatekelezwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2020 kwenye bajeti ya TAMISEMI nilisema na mwaka huu narudia tena, hamtutendei haki kwa namna mnavyogawa hizi rasilimali tulizokuwa nazo. Huyu ndugu yangu wa Korogwe Mjini hapa ana vijiji na vitongoji jumla 34, mimi nina vijiji 118; ana shule za Msingi 34, mimi nina shule 138; unaposema kila wilaya au kila jimbo lipewe maboma tisa, hamtutendei haki. Sisi wengine tunaumia, tuna maeneo makubwa. Hata kama ni kigezo cha watu, pia tuna watu wengi. Tumefuatilia kwenye hizo Halmashauri nyingine, hawana watu wengi namna hiyo. Tunaomba mtuangalie sisi ambao tuna maeneo makubwa, tunaumia Zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna uhaba mkubwa sana wa watumishi hasa kwa upande wa Halmashauri za vijijini. Halmashauri za vijijini zimekuwa ni maeneo ya watu kwenda kuanza kazi na kuondoka kwenda kwenye maeneo mengine mazuri wanayoyataka wao. Sekta ya Afya na Sekta ya Elimu tuna upungufu mkubwa sana wa watumishi. Naomba mtusaidie kupunguza tatizo la upungufu wa watumishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nawaomba TAMISEMI na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, hebu tuweke utaratibu mzuri wa mtu kuhama kutoka kwenye Halmashauri moja kwenda kwenye Halmashauri nyingine. Hii tabia kila mtu akitaka kuhama anaandika moja kwa moja, inakuja kutoka Wizarani amehamishwa, mnatuumiza. Tuna shule zina walimu watatu, kuna zahanati ina mtumishi mmoja au wawili, tunawaomba mtusaidie kupunguza changamoto hii ya watumishi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimshauri Mheshimiwa Waziri kwenye eneo la kusimamia mamlaka ya Serikali za Mitaa. Tuna ripoti ya CAG imetoka juzi; moja ya maeneo ambayo hatukufanya vizuri ni kwenye Halmashauri. Namwomba sana dada yangu, hatafanya kazi yake vizuri TAMISEMI kwa kukimbizana kwenye ziara katika kila Halmashauri. Kwa siku uende Halmashauri tatu au nne, hakuna kitakachofanyika kule. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba, imarisheni sekretarieti za mikoa ili ziwasaidie kuzisimamia Halmashauri. Katibu Tawala wa Mkoa ajue ana jukumu la kuisimamia Halmashauri na Mkurugenzi ajue kwamba yeye immediate boss wake ni Katibu Tawala wa Mkoa na Katibu Tawala wa Mkoa ajue kwamba Halmashauri ikiharibu, naye hatabaki salama. Tuna sekta zote, tuna idara zote pale kwenye Sekretarieti ya Mkoa, zinafanya nini? Kwa nini mpaka tusubiri Waziri au Katibu Mkuu aje? Tuimarishe Sekretarieti za Mikoa zikusaidie wewe na Katibu Mkuu kuzisimamia Halmashauri zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kuimarisha Sekretarieti za Mikoa, tunacho kitengo cha ukaguzi wa ndani kwenye Halmashauri zetu. Mimi naomba TAMISEMI mtafakari upya namna ya kufanya kazi na kusimamia hiki kitengo vizuri.

Mambo yote anayoyasema CAG kwenye Taarifa zake siyo mapya. Wakaguzi wa ndani wameshayaibua kwenye Halmashauri zetu, lakini mwisho wa taarifa ya Mkaguzi wa Ndani ni nini? Hatua za taarifa za Mkaguzi wa Ndani zinachukuliwa na nani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, iko haja ya kukiimarisha hiki kitengo sambamba na kuwajengea uwezo Madiwani wetu kwenye Kamati za Fedha na kwenye Mabaraza ya Madiwani kuzifanyia kazi vizuri taarifa za Wakaguzi wa Ndani ili mambo yaweze kwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine niwaombe, tunazo sheria; hebu TAMISEMI fanyeni kazi ya kupitia sheria. Ziko baadhi ya sheria zinatusababishia kupoteza mapato kwenye Halmashauri zetu. Leo tunapozungumza sisi watu wa Korogwe na watu wa kule Nyanda za Juu Kusini, kuna mgogoro mkubwa sana kwenye kupata ushuru wa mazao kwenye zao la chai, lakini shida ni sheria tu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna haja ya kuziangalia sheria, lakini pamoja na sheria hiyo, iko changamoto nyingine kwamba kampuni inafanya kazi kwenye Halmashauri lakini Makao yake Makuu yako kwenye Halmashauri nyingine. Kwa hiyo, kwenye kupata Service Levy tunakuwa na mgogoro mkubwa sana. Tunaomba TAMISEMI mtusaidie kutoa mwongozo wa namna ya kwenda na vitu kama hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi tuna imani na Mheshimiwa Waziri kwamba wataifanya kazi hii vizuri. Tuna imani nanyi kuwa mambo yanakwenda kukaa sawa sawa. Tunachowaomba, tusaidieni kuzisimamia Halmashauri zetu vizuri. Tusaidieni kuwaimarisha TARURA, tusaidieni kuimarisha Idara ya Afya kwenye Halmashauri ndani ya nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru kwa kunipa nafasi, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)