Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Jerry William Silaa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukonga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia bajeti hii ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Nami niungane na wenzangu kumpongeza sana dada yetu Mheshimiwa Ummy Mwalimu na wenzake wote kwa nafasi na fursa waliyoipata kutumikia Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu nitauelekeza kwenye maeneo matatu lakini kwanza ni kwenye Jiji la Dar es Salaam. Jiji la Dar es Salaam lina historia ndefu kuanzia mwaka 1920 lililopata hadhi ya kuwa mji mpaka lilipokuwa Manispaa ya Dar es Salaam mwaka 1949 na lilipopata hadhi ya kuwa Jiji tarehe 10 Desemba 1961. Mafunzo tuliyoyapata kutoka mwaka 1972 mpaka mwaka 1978 kwenye Madaraka Mikoani na mafunzo tuliyoyapata kuanzia mwaka 1996 mpaka 2000 kwenye Tume ya Jiji, naamini tunaweza kuyatumia kwa upana wake katika kuhakikisha tunatengeneza mbinu bora zaidi ya kutengeneza mazingira ya uongozi na utawala kwenye Jiji la Dar es Salaam.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie fursa hii kuishukuru Serikali kwa kuanzisha ama kwa kuipandisha hadhi Manispaa ya Ilala kuwa Jiji la Dar es Salaam. Tunapozungumzia masuala ya majiji, tunazungumzia maisha ya watu na makazi kwa maana ya urbanization, lakini niseme tu kwamba Dar es Salaam kwa kipindi kirefu imekuwa ikiendeshwa bila master plan. Master plan ya mwisho iliandikwa mwaka 1979 na kwa bahati mbaya hizi master plan huwa zinatakiwa kuhuishwa kila baada ya miaka mitano. Hata hivyo, master plan hii ilikuja kutangazwa kwenye Gazeti la Serikali mwaka 1984 miaka mitano muda ambao ulitakiwa master plan hii ihuishwe lakini tokea wakati huo jiji hili limekosa master plan. Naomba nichukue fursa hii kuipongeza Serikali kwamba mwezi Juni, 2020 katika Gazeti la Serikali tumetangaziwa master plan ya Jiji la Dar es Salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunavyozungumzia master plan ya Jiji la Dar es Salaam tunazungumzia Mkoa mzima wa Dar es salaam, lakini tunazungumzia wilaya za jirani ambazo kutokana na ongezeko la makazi, sasa zimeungana na Jiji la Dar es Salaam. Wilaya za Bagamoyo, Kibaha, Kisarawe na Mkuranga, zote sasa zimeungana na Jiji la Dar es Salaam. Sasa tumepata Jiji pale kwenye Manispaa ya Ilala imekuwa Jiji la Dar es Salaa lakini juzi tumeona Manispaa ya Temeke nayo imeomba na ina vigezo vya kuwa jiji naamini Kinondoni nayo itafika wataomba jiji na naamini kuna siku Ubungo nao wataomba jiji, tutakuwa na majiji mengi. Dhana hasa ya kuwa na jiji ni ya kupata mamlaka yenye uwezo wa kusimamia master plan hii ya Jiji la Dar es Salaam.

Mheshimiwa Naibu Spika, yuko Mheshimiwa Mbunge hapa alichangia kwenye mpango wenzetu kwenye majiji mengine wamewahi kutafuta namna bora zaidi ya kuhakikisha majiji haya yanakuwa na miundombinu ya uhakika na uongozi ambao unaweza kusaidia maisha ya wakazi wa jiji lile kuwa maisha yanayoendana na maeneo mengine. Ziko nchi zimetengeneza Wizara za masuala ya jiji, ziko nchi zimetengeneza mamlaka ya kusimamia jiji. Niombe Serikali iiangalie Dar es Salaam na maeneo yanayozunguka maana jiji hili ndiyo linazalisha zaidi ya asilimia 70 ya mapato ya nchi yetu iweze kutengeneza mfumo ambao utasaidia kuboresha makazi ya wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Zungu hapa amesema, leo Dar es Salaam tunavyozungumza mvua zimenyesha, Dar es Salaam haipitiki, maisha ya wananchi yamekuwa ya tabu. Leo mtu kutoka kule Mzinga Magore, Bomba Mbili Majohe, Mpemba Majohe, Mkolemba anatumia zaidi ya shilingi 1,000 kupanda bajaji imfikishe kwenye eneo la kupata usafiri kwenda mjini.

Mheshimiwa Naibu Spika, nami nitaungana na wenzangu kuendelea kuisii Serikali iangalie umuhimu wa Mradi wa Dar es Salaam wa Metropolitan Development Project (DMDP II). Nami niseme tu pamoja na kuungana na wenzangu kwamba tunapozungumza kwenye bajeti ya TAMISEMI, dada yetu Mheshimiwa Ummy Mwalimu ni mchapakazi, hilo hatuna shaka na ana Manaibu Waziri wazuri lakini wenzetu hawa ni watumiaji wa bajeti kama sisi wengine tujipange vizuri kwenye kuishauri Serikali jinsi ya kupata fedha kwenye bajeti ya Wizara ya Fedha na bajeti kuu ya Taifa ili miundombinu ya Dar es Salaam iweze kuboreka, wananchi wale waendelee kuzalisha uchumi na mapato ya Taifa hili yazidi kuboreka kupitia miundombinu ya barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge katika kipindi cha kampeni na katika michango yetu mingi humu ndani tunasema kwamba Serikali imefanya kazi kubwa sana kwenye sekta ya afya, elimu na sekta nyingine zinazosimamiwa na Wizara ya TAMISEMI. Zimejengwa zahanati nyingi, vituo vya afya vingi, hospitali za wilaya, shule Kongwe zimekarabatiwa na kazi ya ujenzi wa miundombinu ya elimu na afya inaendelea. Naomba kusema jambo moja hasa katika nyakati hizi ambapo miradi yetu mingi hii inatekelezwa kwa force account, kazi hizi zimefanywa na Wakurugenzi na watendaji wa halmashauri zetu nchi nzima. Sikatai, yawezekana wako watendaji wachache wenye upungufu lakini wako watendaji wengi wanaofanya kazi nzuri ya ujenzi wa Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge na Serikali, nawaomba; Waheshimiwa Wabunge ni Wajumbe wa Kamati za Fedha na Utawala kwenye Halmashauri zetu; na kamati hizi ndiyo Mamlaka ya Nidhamu kwa watumishi wote ndani ya Halmashauri. Nawaomba sana, mnyonge mnyongeni, haki yake mpeni. Wale watumishi wenye upungufu tuwachukulie hatua kwa mujibu wa Kanuni za Utumishi wa Umma na Sheria ya Utumishi wa Umma; na wale wanaofanya vizuri tuwapongeze. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tusimbebeshe Waziri wa TAMISEMI mzigo wa kuwa disciplinary authoriry ya mpaka Mtendaji wa Kata majukumu ambayo ni ya kwetu kule Halmashauri. Tusigueze Bunge hili ikawa ni sehemu ya kuja kusulubu watu ambao bahati mbaya wengine hawana uwezo wa kuja kujitetea.

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali iendelee kusimamia nidhamu ya watumishi, lakini na sisi tuwaangalie tuwaangalie wenzetu amabo ni wadau wenzetu…

MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

T A A R I F A

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Jerry Silaa kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Mussa Azzan Zungu.

MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumpa taarifa msemaji, lakini kwanza nampongeza kwa alivyoanza. Ila naomba amalizie kwa kusema Dar es Salaam isiwe mamlaka, iwe na Wizara ya kuiendesha Dar es Salaam. (Kicheko/Makofi)

NAIBU SPIKA: Sasa unaipokea hiyo taarifa ambayo imekuja kwa namna ya wazo jipya! (Kicheko)

MHE. JERRY W. SILAA Mheshimiwa Naibu Spika, naipokea kwa mikono miwili; na ametujenga, ndiyo maana nikasema iko Miji ilichukua mbinu tofauti hili Serikali iangalie maeneo haya, kwa maana ya Wizara, kama ni Dar es Salaam Metropolitan Authority ili tupate mamlaka nzuri ya kusimamia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naomba kuwasilisha, naunga mkono hoja. (Makofi)