Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Amina Nassoro Makilagi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nikushukuru wewe na nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kutoa mchango wangu katika hoja hii muhimu kwa ustawi wa Taifa ya makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri Profesa Joyce Lazaro Ndalichako na timu yake yote kwa kuandaa na kuwasilisha vizuri sana hotuba ya makadirio ya mapato na matumizi ya fedha kwa mwaka 2016/2017. Pia natoa pole kwa Naibu Waziri Mheshimiwa Engineer Stella Manyanya kwa kuondokewa na mzazi wake mpendwa. Naomba Mwenyezi Mungu ampe moyo wa uvumilivu katika kipindi hiki kigumu cha maombolezo na roho ya marehemu iwekwe mahali pema peponi. Amina.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba kutoa mchango wangu kwenye makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya elimu, sayansi, teknolojia na ufundi kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ubora wa vitabu vinavyotumika kufundisha mashuleni, wakati soko huria la utengenezaji na usambazaji wa vitabu likilenga kupunguza uhaba wa vitabu Serikali idhibiti ubora wa vitabu ili kuhakikisha vitabu vinavyotumika shuleni vinakuwa na ubora ili kuzalisha wasomi wazuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wa nini kifanyike kwenye mtaala wa elimu, Serikali kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu itengeneze mfumo ambao vijana wengi watakwenda kwenye Vyuo vya Ufundi na hivyo kuwa na wazalishaji wengi ambao wataweza kuunda vitu mbalimbali na sio kuwa na kundi kubwa la wasomi wa vyuo vikuu ambao watakuwa wanatafuta kazi baada ya kutunukiwa shahada zao. Ni muhimu sana Serikali ipitie upya mfumo wetu wa elimu ambao kwa kiasi kikubwa unawaandaa wasomi wetu kuwa waajiriwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano kwa mujibu wa hotuba ya bajeti ya mwaka 2014/2015, idadi ya vyuo iliongezeka kutoka 26 hadi 50 kati ya mwaka 2005 hadi 2014 na hivyo idadi imeongezeka kutoka wanafunzi 40,719 kwa mwaka 2005 hadi wanafunzi 200,986 kwa mwaka 2014. Wasomi wote hawa wanaandaliwa kuwa watawala ambao wataanza kutafuta ajira na hivyo kusababisha nchi kuwa na wasomi wengi ambao watahitaji kuajiriwa na siyo kuwa wazalishaji kutokana na mfumo wetu wa elimu kuwa na nadharia nyingi na siyo vitendo. Katika karne ya sasa ni muhimu Serikali kufanya marekebisho katika mfumo wetu wa elimu ili uwezeshe vijana wetu kuwa wazalishaji pindi tu wanapohitimu elimu ya vyuo vikuu na hivyo kuweza kujiajiri wenyewe badala ya kusubiria ajira za Serikali na mashirika binafsi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kwa kushirikiana na Wizara zake ielekeze pesa nyingi kwenye miradi ya maendeleo na sio kwenye matumizi ya kawaida. Mfano, kwa mujibu wa hotuba ya Wizara ya Maliasili na Utalii iliyosomwa Bungeni na Mheshimiwa Profesa Jumanne Maghembe, kwa mwaka 2015 sekta ya utalii peke yake ilitoa ajira rasmi kwa vijana 500 na ajira 1000 zisizo rasmi.
Aidha, kwa mwaka 2016/2017, Serikali iendelee kuboresha mazingira ya utalii kama vile kununua ndege, kujenga barabara na kujenga viwanja vya ndege ili sekta ya utalii ifanye vizuri ziaidi na hivyo kusaidia kupunguza tatizo la ajira ambalo kwa kiasi kikubwa linatokana na mfumo wetu wa elimu, kuzalisha wasomi wengi wenye shahada ambao wanategemea kuajiriwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika dunia ya sasa Serikali lazima itambue kuwa tatizo la ajira kwa wasomi wetu wa vyuo vikuu linazidi kuongezeka kila siku kutokana na mfumo wetu wa elimu kuwaandaa vijana wetu kuwa waajiriwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mwandishi wa kitabu cha Rich Dad Poor Dad Robert Kiyosaki anasema mifumo ya elimu yenye mtazamo wa go to school, study hard, get good grades and find a safe and secure job umepitwa na wakati.
Aidha, mwandishi huyu anashauri mifumo ya elimu ya sasa iwe na mtazamo wa go to school, study hard, get good grades, build your business and become a successful investor. Serikali itazame namna ya kuhakikisha vijana wengi wanapata elimu ya ufundi ambayo itawasaidia vijana wengi kuwa wazalishaji wa moja kwa moja na siyo kutegemea ajira. Katika nchi zilizoendelea kiteknolojia kama China na Japan vifaa vingi vidogo vidogo vinatengenezwa na vijana ambao kwa kiasi kikubwa wana elimu ya ufundi tu. Ingawa tuna vyuo vya ufundi stadi, bado idadi ya wanafunzi wanaojiunga katika vyuo hivi ni ndogo kama ilivyooneshwa katika kitabu cha hotuba ya bajeti ya Wizara ya Elimu, ukurasa wa 95.
Mheshimiwa Mwenyekiti, umuhimu wa vyuo vya ufundi kila mkoa; umefika wakati sasa Serikali ianzishe vyuo vya ufundi kila mkoa ambavyo vitawasaidia vijana wetu kupata elimu ya kuwawezesha kujitegemea na siyo kutegemea kuajiriwa na Serikali. Aidha, vyuo hivi vitoe elimu kutokana na mazingira ya eneo husika. Mfano, vyuo vitakavyojengwa Mikoa ya Iringa, Njombe na Mbeya vitoe elimu ya ufundi juu ya matumizi ya mazao ya mbao na vile vitakavyojengwa katika Mikoa ya Kanda ya Ziwa vijengwe vyuo vya kutoa elimu ya ufundi na ujuzi na kusindika samaki. Kama Serikali itaweka mfumo ambao vijana wengi watakwenda kwenye vyuo vya ufundi wataweza kuzalisha samani nyingi ambazo Serikali pia inaweza kununua samani ambazo zitakuwa zinazalishwa na vijana wetu hapa hapa nchini kwa matumizi mbalimbali na hivyo kupunguza matumizi ya fedha za kigeni kutokana na kununua samani nje ya nchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuunga mkono jitihada za Mheshimiwa Rais za kujenga Tanzania ya viwanda, ni muhimu vijana wengi wawe na elimu ya ufundi ambao wataanzisha viwanda vidogo vidogo vingi ambavyo vitazalisha samani mbalimbali. Aidha, wasomi wetu wenye elimu ya ufundi wanaweza kuunda viwanda vikubwa ambavyo vitasaidia katika kuleta mapinduzi ya viwanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali kwa Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi 2016/2017, je, Serikali imejipangaje kwa mwaka 2016/2017 kutatua changamoto za upungufu wa madawati, upungufu wa nyumba za Walimu na madai ya Walimu ambayo ni muhimu hasa katika kuimarisha sekta ya elimu?
Mheshimiwa Mwenyekiti, nini kifanyike kwa mwaka 2016/2017, katika Wizara hii, baada ya Serikali ya Awamu ya Mheshimiwa John Pombe Magufuli imeanza kutoa elimu bure na hivyo watoto wengi wamejitokeza shuleni na hivyo kusababisha shule kufurika watoto wengi. Aidha, Serikali kwa kushirikiana na Wizara ya Maliasili, Wizara ya Elimu na wadau mbalimbali wa maendeleo waweke mpango mkakati wa kutatua changamoto hizi kama vile kushawishi wananchi, taasisi binafsi na Serikali katika kuchangia ununuzi wa madawati na ujenzi wa vyumba vya madarasa ili kuwezesha watoto wengi kupata elimu.
Aidha, kwa mwaka 2016/2017, Serikali iendelee kuboresha mazingira ya kazi na makazi ya Walimu hasa wale walioko vijijini. Walimu wapandishwe madaraja na kulipwa stahili zao bila kucheleweshewa, pia kwa mwaka 2016/2017, Serikali ianze kuwapa motisha ili kuwapa moyo na kuwahamasisha wengine kufanya kazi kwa bidii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sababu za kuunga mkono makadirio ya mapato na matumizi Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi 2016/2017 yapitishwe, katika bajeti ya mwaka 2016/2017, Wizara imeomba kupitishiwa jumla ya shilingi trilioni 1.396 huku matumizi ya kawaida yakiwa ni shilingi bilioni 499 sawa na 35.7% ya bajeti yote huku miradi ya maendeleo ikitengewa shilingi bilioni 897 sawa na 69.1%. Ili kuunga mkono jitihada za kuinua kiwango cha elimu kwa mwaka 2016/2017, Serikali imedhamiria kuinua kiwango cha elimu kwani kati ya shilingi bilioni 897, Serikali imetoa shilingi bilioni 620 sawa na 69.1%, ni fedha za ndani huku 30.9% ikiwa ni fedha za nje.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mwaka 2016/2017, Serikali ihakikishe kuwa fedha zilizotengwa kwa ajili ya Wizara ya Elimu zinapelekwa kwa wakati ili kuimarisha kiwango cha elimu nchini. Mfano wa mwaka 2015/2016 hadi tarehe 30 Aprili, 2016 Serikali ilipeleka shilingi bilioni 789 sawa na 72.12% ya bajeti yote. Kwa sababu Serikali ya Awamu ya Tano imejiimarisha katika ukusanyaji wa mapato yanayotokana na kodi ni vizuri kwa mwaka 2016/2017 Serikali ipeleke fedha za miradi ya maendeleo kwa wakati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuinua kiwango cha elimu, Serikali imeongeza kiwango cha bajeti kutoka shilingi trilioni 1.094 hadi shilingi trilioni 1.396 sawa na ongezeko la 21.6% kutoka mwaka 2015/2016 hadi 2016/2017.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja.