Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja

Hon. Ummy Ally Mwalimu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Tanga Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi nakushukuru, lakini nianze na kukishukuru Chama changu cha Mapinduzi na Wanawake wa UWT wa Mkoa wa Tanga kwa kunipa heshima hii ya kurudi tena katika Bunge hili.
Pia kwa heshima na unyenyekevu mkubwa, namshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa imani yake kubwa sana kwangu, namwahidi tutachapa kazi, kama kauli mbiu ya Serikali inavyosema.
Mheshimiwa Naibu Spika, tumesikiliza michango, maoni na ushauri wa Waheshimiwa Wabunge na tunawashukuru wote ambao wamechangia katika eneo hili. Lengo ni kutaka kuboresha utoaji wa huduma za afya, lakini pia kuhakikisha tunajenga jamii ya Watanzania inayojali na kuheshimu usawa wa jinsia, haki za wanawake, haki za watoto na haki za wazee. Nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge na niwathibitishie katika hatua hii kwamba tutafanyia kazi maoni yenu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu ya muda, nitajikita katika masuala makuu mawili ambayo yameongelewa sana na Waheshimiwa Wabunge wote. Kama walivyosema wenzangu, wakati wa kuchangia Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano na Mpango wa Maendeleo wa 2016/2017 tutatoa mwelekeo wa vipaumbele vyetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala kubwa ambalo limechangiwa na Waheshimiwa Wabunge, lakini pia limejitokeza kwa sauti kubwa wakati wa Hotuba ya Mheshimiwa Rais ni suala la upatikanaji wa dawa katika vituo vya umma vya kutolea huduma za afya katika Zahanati, Vituo vya Afya, Hospitali za Wilaya na Hospitali za Rufaa za Mikoa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia Bunge lako nataka kuwathibitishia Waheshimiwa Wabunge na Watanzania kwamba tumedhamiria kuhakikisha tunapunguza tatizo la ukosefu wa dawa katika hospitali zetu. Tayari tumeshaanza kuchukua hatua na kwa sasa hivi uwezo wetu wa kutoa dawa ni asilimia 70 na tunakusudia tufikie asilimia 95. Hii tutawezaje? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza dawa ambazo zinafika kwa wananchi, nyingi zinapotea mtaani katika mikono ambayo siyo salama. Kwa hiyo, kubwa ambalo tumelifanya na tutaendelea kulifanya ni kudhibiti upotevu wa dawa za Serikali na vifaa tiba. Sasa hivi tumeshaweka nembo katika dawa zote za Serikali ambazo ni muhimu. Asilimia 80 ya dawa za Serikali sasa hivi tayari zina nembo.
Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge, tuendelee kuhamasisha wananchi wetu, watakapoona dawa ya Serikali ambayo ipo katika duka la dawa ambalo halistahili, watujulishe na wachukue hatua. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili ambalo tumelifanya ni kuimarisha mfumo wa usambazaji, ununuzi na uhifadhi wa dawa. Hili ambalo tumelifanya tumeshaagiza MSD kuhakikisha dawa hazishushwi katika kituo chohote cha afya cha Umma bila kuwepo kwa Kamati ya Afya ya Kituo husika.
Waheshimiwa Wabunge, sisi sote ni Madiwani, tuhakikishe Kamati za Afya za Zahanati, za Vitua vya Afya za Wilaya zinatimiza wajibu wao wa kuhakikisha tunadhibiti dawa na vifaa tiba vya Serikali.
Jambo lingine ambalo ningependa kulisisitiza, mpango wetu wa muda mrefu ni kuhakikisha tunanunua dawa kutoka kwa wazalishaji, badala ya kununua dawa kutoka kwa wafanyabiashara na hili linawezekana sana. Kauli mbiu ya Serikali ya Awamu ya Tano ni kwamba tunabana matumizi. Kwa hiyo, tunaamini tutakaponunua dawa kutoka kwa wazalishaji, tutaweza kupata dawa nyingi, lakini pia kwa bei nafuu na hivyo kuweza kutatua tatizo kubwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hili, tutaongeza bajeti ya kununua dawa, vifaa na vifaa tiba. Waheshimiwa Wabunge, wameongelea suala la ukosefu wa X-Ray, Ultra-Sound, CT-Scan na MRI. Tayari tumeshachukua hatua, sasa hivi Muhimbili hamna shida tena katika vifaa hivyo vikubwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunao mpango pale Wizarani wa kuhakikisha katika kila Hospitali ya Rufaa ya Mkoa tunaiwezesha katika eneo zima la uchunguzi, maana yake, ni vifaa vyote ambavyo vinahitajika katika kufanya uchunguzi. Tayari tumeshapeleka mapendekezo yetu kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu, tuone ni jinsi gani tutaweza kusonga mbele.
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa
muda wa Mzungumzaji)
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, duh!
Meshimiwa Naibu Spika, la mwisho ni suala la miundombinu. Nikuhakikishie kwamba tutafanya kazi na wenzetu wa TAMISEMI kuhakikisha kwamba tunajenga zahanati katika kila kijiji, vituo vya afya katika kila Kata na Hospitali za Wilaya. Niwaambie Waheshimiwa Wabunge, hili kwa kweli, sisi la kwetu itakuwa tu ni kuweka vibali. Kwa hiyo, wale Wabunge wote ambao wamejenga vituo vya afya...
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Ummy, tafadhali weka nukta!
WAZIRI WA AFYA MAENDELEO YA JAMII JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, nimalize kwa kusema, kama mwanamke, afya ya mama na mtoto ni kipaumbele cha Serikali ya Awamu ya Tano. Tutahakikisha tunapunguza vifo vya wanawake wajawazito na watoto chini ya miaka mitano. Hilo ni la kipaumbele, tutaongea kwenye Mpango wa Maendeleo. (Makofi)