Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa fursa hii, kwanza kabisa nitumie fursa hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kunipa nafasi hii ya kutoa mchango wangu, lakini nitumie fursa hii vile vile kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Manaibu wake na watendaji kwa uwasilishwaji wao bila kusahau Kamati ya TAMISEMI.

Mheshimiwa Spika, nitakuwa na mchango kwenye maeneo kama mawili, kama muda utaruhusu basi nitaongeza eneo lingine moja. Eneo la kwanza ni juu ya flow ya pesa kwenye halmashauri zetu, dhamira ya uundwaji wa Serikali za Mitaa ni kurahisisha au kuhakikisha huduma za kijamii zinawafikia wananchi katika mazingira yaliyo mazuri na wapate huduma hizi katika mazingira yaliyo safi.

Mheshimiwa Spika, na pale ambapo halmashauri hizi zinaanzisha miradi, inatakiwa fedha ziende miradi ikamilike na iweze kuwa na tija ile thamani ya fedha iweze kuonekana. Bahati mbaya kumekuwa na shida kwa namna fulani kwenye flow ya pesa kwenda kwenye halmashauri zetu, matokeo yake ni kwamba miradi ama haikamili au wakati mwingine inakamilika lakini haiwezi kufikia thamani ile ambayo inakuwa imetarajiwa ili kuweza kuwasaidia wananchi wetu.

Mheshimiwa Spika, niki-cite kwa mfano taarifa ya CAG ya Mwaka 2019/2020 kwa mfano, utaona kwamba CAG katoa mfano kwenye mwaka huo kuna karibu bilioni 184 zilipelekwa kwa ajili ya miradi, miradi hii haijakamilika, matokeo yake nini, ni kwamba kile kilicho tarajiwa kwa ajili ya wananchi wale, ili huduma iweze kuwafikia haikuweza kuwafikia kwasababu miradi ile haijakamilika.

Mheshimiwa Spika, na hili linatokea kwasababu gani, inawezekana watumishi tulionao hawasimamii vizuri miradi ile ikaweza kukamilika, au fedha hazijaweza kwenda kama ambavyo ilitarajiwa ili thamani ile iweze kuonekana.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niombe tu kama ushauri, Serikali ihakikishe kwamba miradi inapokuwa inabuniwa kwenye halmashauri zetu basi Serikali ihakikishe fedha zinakwenda kama zilivyotarajiwa ili yale tuliyotarajia kama manufaa kwa wananchi wetu, yaweze kupatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kuna wakati mwingine miradi inakamilika lakini haitumiki, niki-cite kwenye taarifa ya CAG, vile vile, utaona kwamba CAG anasema kwenye Mwaka 2019/2020, kuna bilioni 18 zimepelekwa kwenye miradi ya maendeleo, miradi imekamilika lakini haitumiki.

Mheshimiwa Spika, tafsiri yake ni kwamba ama kuna shida kwenye ushirikishwaji wa wananchi, matokeo yake sasa miradi imebuniwa lakini siyo kwa manufaa ya wananchi na hili linatokea wakati mwingine ushirikishwaji unakuwa siyo mzuri kwasababu kuna tatizo kwenye uwakilishwi wetu.

Mheshimiwa Spika, asubuhi kuna mchangiaji mmoja ameonyesha umuhimu wa kuboreshwa kwa maslahi ya Madiwani, Wenyeviti wa Vijiji na Wenyeviti wa Vitongoji.

Mheshimiwa Spika, ni jambo la msingi sana, kwasababu miradi yetu inayotekelezwa kwenye halmashauri zetu wasimamizi wakuu ni Wenyeviti wa Vijiji, Wenyeviti wa Vitongoji na Waheshimiwa Madiwani, lakini maslahi yao ni duni sana! (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niiombe sana Serikali iliangalie jambo hili iweze kuboresha maslahi ya wawakilishi wetu hawa ili angalau waweze kusimamia shughuli hizi za maendeleo katika kiwango kilicho kizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini eneo la pili ambalo nilitaka nichangie ni kwenye eneo la TARURA, wengi wamesema juu ya TARURA na kupitia michango mbalimbali tumesema juu ya umuhimu wa kuboresha TARURA. TARURA mpaka inaanzishwa ilikuwa na umuhimu wake na ina majukumu mazito sana kwa ajili ya kuboresha miundombinu kwa ajili ya watu wetu kwasababu barabara zinazohudumiwa na TARURA nyingi ni zile barabara ambazo wananchi wetu kwa wingi wao wanatumia kwa ajili ya shughuli zao za maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ni muhimu sana TARURA ikaangaliwa kama ambavyo tulivyokuwa tunapendekeza, na kwangu mimi ningependekeza maeneo mawili ambayo ni muhimu sana yaangaliwe kwenye eneo la TARURA.

Mheshimiwa Spika, la kwanza ni muundo wake, ilivyo hivi sasa TARURA menejiment ya TARURA na hasa kwenye eneo la bajeti linasimamiwa zaidi na uongozi wa mkoa, lakini huku wilayani ambako kuna watu ambao wanajuwa kwa uhalisia matatizo na changamoto za barabara zilizoko kwenye maeneo yao, hawana nguvu yoyote ya kibajeti, kiasi kwamba wanashindwa kushughulikia matatizo madogo madogo yaliyoko kwenye maeneo yao ambayo yangewasababisha sasa waweze kuondoa hizi changamoto za barabara na hatimaye ziweze kuwasaidia watu wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niombe Serikali iangalie marekebisho ya muundo, ili angalau Mameneja wa TARURA kwenye wilaya nao wawe na nguvu ya kibajeti, jambo ambalo litawasaidia angalau kuweza kushughulikia matatizo madogo madogo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vile vile, suala lingine ni ambalo tumelizungumza mara kwa mara kusaidia uwezeshaji kwa TARURA, fedha wanazozipata kimsingi ni ndogo sana, haziwezi kuwapa uwezo wa kushughulikia matatizo ya barabara zilizoko kwenye maeneo yetu. Kwa hiyo, ile fomula kama itaweza kubadilishwa, itasaidia sana barabara zetu ziweze kuwa bora. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye eneo la Ukerewe kuna changamoto kadhaa na niombe Mheshimiwa Waziri, tumeleta mara kadhaa karibu miaka mitatu mfululizo tunaleta ombi kwenu, mtusaidie hasa hapa pale Ukerewe, angalau mtupe kilometa moja mbili za lami ili tuweze kuchochea mzunguko wa kiuchumi kwa wananchi wa Ukerewe, jambo ambalo litatusaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini vile vile kwenye eneo la Ukerewe, kuna eneo moja linaitwa Namakwekwe, kuna eneo ambalo kuna mto ambao nyakati za mvua watu hawapiti na inasimamisha hata shughuli za kiuchumi na hata watoto hawawezi kwenda shule, kwenda upande wa pili eneo la Mibungu. Mtusaidie Mheshimiwa Waziri, angalau tuweze kujengewa daraja pale kuweza kuunganisha eneo hili ili wananchi waweze kufanya shughuli zao vizuri.

Mheshimiwa Spika, lakini Mheshimiwa Waziri nikumbushe tu ahadi wakati Mheshimiwa Waziri Mkuu alivyokuja Ukerewe, aliahidi kupitia maelezo tuliotoa lakini na changamoto alizoziona kutujengea kituo Kituo cha Afya kwenye Kisiwa Ilungwa, lakini vile vile kutujengea zahanati kwenye Kisiwa cha Ghana, mtusaidie sana ili anghalau visiwa hivi viweze kupata huduma nzuri za kiafya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini sambamba na hilo, kuna mradi wa barabara mradi wa Tanzania Strategic Cities Projects, ambao ulikuwa unahudumia barabara kwenye miji, mradi huu sasa umekwisha kamilika na tumeanza mradi mwingine wa Tanzania Cities Transforming Infrastructure Competitiveness yaani TAIC ambao utasaidia miji 40 kujengewa barabara za mawe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niiombe Serikali, kupitia mradi huu na barabara hizi za mawe zikianza kujengwa, maeneo mengi kama Ukerewe tuna fursa ya kutumia mawe kwa ajili ya ujenzi wa barabara hizi, lakini bahati mbaya na barabara hizi kwasababu zinafadhiliwa na Benki ya Dunia, kuna kikwazo kimoja ambacho kinafanya kama zinafanyika, basi watu wetu hawapati fursa ya kunufaika na barabara hizi. Sasa niombe Serikali, kwasababu kuna ile Sera ya Ujenzi ya Mwaka 2003, hebu Serikali muone kama mnaweza kuifanyia mabadiliko ili angalau kiwekwe kipengele kinachoweza kuruhusu matumizi ya nguvu kazi (labour based), hili litasaidia sana watu wetu angalau kuweza kunufaika na barabara hizi kwa kupata ajira, kwa sababu shughuli hizi za kuponda mawe kufanya nini, kupanga yale mawe barabarani itasaidia sana kuchochea uchumi wa watu wetu. Kwasababu likifanyika hili ni jambo jema sana na watu wetu ndiyo watakao nufaika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na hizi barabara ni nzuri ukilinganisha na lami kwa mfano kwa tathimini, ujenzi wa barabara za mawe gharama yake ni karibu robo ya barabara kilomita moja ya barabara ya mawe, ni karibu robo ya barabara ya lami. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini sambamba na hilo, angalau ikifanyika kama nilivyopendekeza, itasaidia sana kuchochea uchumi wa watu wetu kwasababu watu wetu angalau hasa vijana wataweza kunufaifa kwa kupata ajira ndogo ndogo katika kufanya shughuli kwenye maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine la mwisho ambalo nilitaka nichangie ni juu ya upungufu wa watumishi kwenye halmashauri zetu. Wamesema wachangiaji waliotangulia, kwenye maeneo tunayotoka hasa maeneo ya pembezoni kama ilivyo visiwa vya Ukerewe kwasababu ya jiografia yetu mara nyingi watumishi wanapopangwa kwenda kwenye maeneo yale, wanafika wanaripoti na kuondoka! Niombe wizara, kwa changamoto kama hizi, tuone namna ambayo tunaweza tukatoa hata posho ya mazingira magumu. Ili angalau watumishi wetu wanapopangiwa kwenye maeneo haya, waweze basi kukaa na kuwahudumia wananchi wetu, angalau wananchi waweze kufaidika na Serikali yao kupata huduma zile zinazostahili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kwenye maeneo kwa mfano Ukerewe mwaka juzi tumepambana sana kuhamasisha wananchi tukajenga madarasa zaidi ya 400; tumejenga maboma kwa ajili ya zahanati yote haya yamekamilika tunahitaji msaada angalau muweze kutushika mkono tumalizie kazi hizi. Pamoja na fedha mlizozitoa kwenye bajeti hii kwa ajili ya kusaidia ukamilishaji wa maboma Ukerewe kama specific area tunaomba mtusaidie angalau haya maboma tuliyoyajenga kwa kushirikikana na wananchi zaidi ya 400 tuweze kuyaezeka. Jambo hili litasaidia wananchi wetu kupata moyo na kuona Serikali inawajali na wakati mwingine hata ukiwahitaji waweze kushiriki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, nashukuru sana kwa fursa hii, naunga mkono hoja. (Makofi)