Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala Za Mikoa Na Serikali Za Mitaa

Hon. Dr. Amandus Julius Chinguile

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nachingwea

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala Za Mikoa Na Serikali Za Mitaa

MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi nichangie kwenye Wizara hii Ofisi ya Rais TAMISEMI. Awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya lakini pia nichukue nafasi hii kumpongeza pia dada yangu Waziri Mheshimiwa Ummy na Naibu Mawaziri kwa kuaminiwa na Mheshimiwa Rais kuongoza Wizara hizo. Natambua kazi nzuri inayofanywa na Wizara hii ya TAMISEMI kwenye sehemu ya elimu, afya mmefanya kazi kweli kweli tunawapongeza sana.

Mheshimiwa Spika, lakini hata hivyo, wacha nizungumzie kidogo suala la TARURA. Ukiona mtu mzima analia kwakweli kuna jambo. Kwenye suala la TARURA Waheshimiwa Wabunge wengi kila anayesimama analia kuhusu TARURA, TARURA shida, changamoto.

Katika hili niiombe sana Serikali waone namna watakavyokuja na muarobaini kuhusu TARURA. Lakini TARURA hii nitaizungumzia kwenye maeneo mawili, la kwanza kwenye muundo wenyewe wa TARURA. Yuko mtu anaitwa mratibu anakaa pale Mkoani, yeye ndiyo anafanya kila kitu, tender anatoa yeye na kila kitu. Sasa tumemuacha huyu meneja ambaye yuko Jimboni, wilayani ambaye anajua sasa barabara gani ni kipaumbele, yuko hana shughuli yoyote na hata tukizungumzia kwamba anashauri kule mkoani bado anayeshauriwa ana mambo mawili, kukubali au kukataa huo ushauri. Siku ya siku bado mkoani ndiyo wenye mamlaka ya kuongeza wapi kipaumbele. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo jingine ukosefu wa hii bajeti. Kwa kweli mimi niiombe sana Serikali, dada yangu Ummy najua ni mchapakazi sana. Mheshimiwa hebu njoo na muarobaini kuhusu TARURA ni namna gani tunaweza tukaongeza mapato yatakayotuwezesha kufanya kazi kwenye sehemu hii ya TARURA, nikuombe sana na naamini hili kwa uchapakazi wenu kwa uzuri kama mlivyofanya vizuri kwenye maeneo mengine ambayo nimewapongeza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nizungumzie pia kuhusu watumishi hasa watumishi wa afya na walimu. Huko nako ni shida, sisi tunaotoka pembezoni mwa nchi, hawa watumishi huwa wanaomba maombi ya moja kwa moja kwenda kwenye maeneo yale kwa ajili ya kupata cheque number tu lakini baada ya hapo wote wanaomba kuondoka kwenye maeneo yale.

Mheshimiwa Spika, niiombe sana Wizara, hebu tuwe na mpango maksudi wa kuhakikisha kwamba hao wanaoomba kwenye maeneo yale kwakweli wanakwenda wakiwa na ari ya kufanya kazi na sio tu kwenda kwenye maeneo yale kwa ajili ya kuchukua cheque number. Hapo hapo niendelee pia kushauri Wizara kwamba basi tuwape kipaumbele, wako vijana ambao wametoka na wana-apply kutoka kwenye maeneo yale wameshayazoea. Hebu tuwape kipaumbele, sizungumzii kwamba wale wengine wasipate nafasi, la hasha lakini basi tuone mpango ambao utatuwezesha na sisi tulioko pembezoni mwa nchi kuweza kupata watumishi ambao kwa kweli watakuwa na ari ya kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo jingine nizungumzie kwenye maboma. Maboma haya yako maboma ya zahanati lakini pia maboma ya shule za msingi na sekondari. Hebu tuuone huu mpango mkakati, kabla ya kuendelea na vipaumbele vipya tuone mpango mahsusi wa kwenda kumalizia haya maboma. Lakini tukifanya hivyo twende sambamba sasa na kuhakikisha vituo vyetu, shule zetu zinakwenda sasa kupata watumishi wa kutosha na hapo niende kule kwangu kwenye jimbo langu la Nachingwea, kuna kituo chetu cha afya Kilimarondo. Mheshimiwa Waziri ikikupendeza, ukipata nafasi twende utembelee eneo lile. Daktari yupo lakini pia na watumishi wengi wapo lakini hawatoshelezi. Eneo lile ni mbali kabisa kutoka Makao Makuu ya wilaya. Tuone namna maeneo yale tunavyoweza kuyapa kipaumbele ili basi waweze kupata watumishi watakaokidhi kwenye maeneo yale. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niendelee kuzungumzia pia suala la Posi, zile mashine za kukusanyia mapato. Huko nako iko shida. Wataalam wetu walio wengi haawana ufahamu wa kutosha na hasa kwenye zile kata. Tujikite kutoa elimu namna gani ya kutumia zile mashine kwa ajili ya kukusanya mapato.

Mheshimiwa Spika, kinachotokea, kwa sababu maeneo mengine wako waliopata shoti kwa namna hii mashine ile hawezi kuitumia vizuri. Badala yake sasa wakati wa kutoa ripoti anakuta anachotakiwa kuwasilisha ni kikubwa kuliko alichonacho. Kinachotokea sasa wanafunika zile posi, anaiweka pembeni anaendelea. Sasa tuwe na mpango huo wa kutoa elimu kwa hawa wataalam wetu kule chini, tunajua wengine hawana taaluma hiyo ya uhasibu. Basi tuwape walau zile kozi ambazo zitawawezesha kupata ujuzi huo. Lakini pia kuhakikisha tunafuatilia kadri inavyowezekana, kadri tunavyopata muda ili mapato yanakusanywa kisawasawa. Kuna mapato mengi yanapotea na nina hakika tukiimarisha kwenye eneo hilo kwa kweli tutafanya vizuri kweli kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wako vijana wengi ambao kwa kweli wanalia. Nikionesha hapa message za simu za kila Mbunge hakuna atakayekuwa anasema mimi sina message ya kijana kutoka kwenye Jimbo langu hana ajira. Mheshimiwa Waziri nikuombe sana, tunajua kwamba kipato chetu tunachokusanya ndicho kinachokwenda kuajiri vijana au ajira mpya. Tuone namna ya kuongeza ajira, vijana wetu wako wasomi, wako huko mashambani, vijijini wanao ujuzi wa kutosha. Tuone namna ya kuwatumia hawa kwa ajili ya maendeleo ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bado niendelee kuzungumzia tena wale walimu au watumishi wanaotoka kutoka maeneo mengine kuhitaji kuhamia maeneo mengine hebu tujaribu namna ya kuyaona hapa. Mheshimiwa Waziri wako watumishi ambao wanataka kutoka Tanga kwenda Nachingwea mahali ambapo tuna shida ya watumishi sasa process zile zinazotumika ili huyu mfanyakazi kurudi kule ambako moyo wake unatamani ni shida.

SPIKA: Ahsante Mheshimia Chinguile.

MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. Nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)