Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Stella Simon Fiyao

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, najua wazi kabisa kwamba moja ya majukumu ya Ofisi ya Waziri Mkuu ni kuwa kiunganishi baina ya Serikali na vyama vya siasa, lakini ajabu ni kwamba, Ofisi ya Waziri Mkuu haijatekeleza jukumu hili la kuhakikisha inaviunganisha vyama vya siasa na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mahusiano kati ya Serikali na Vyama vya Siasa, hususan Vyama vya Upinzani yamekuwa na uhasama na uadui mkubwa kwa kipindi chote cha miaka mitano. Ndani ya miaka mitano tumeshuhudia mambo kadhaa yakiendelea kutokea ndani ya Taifa letu…

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Stella, pokea Taarifa. Mheshimiwa Waziri wa Nchi.

T A A R I F A

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Spika,
maneno yanayosemwa na Mheshimiwa Mbunge siyo sahihi. Kama Serikali na Vyama vya Siasa tungekuwa na uhasama mkubwa, usingeshuhudia Vyama vya Siasa vikienda kukagua miradi ya maendeleo inayotekelezwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Vimekuwa vikitoka hadharani na kuthibitisha kwamba kwa kweli, katika kujenga demokrasia na ujenzi wa ustawi wa Watanzania, kazi ya Serikali inaungwa mkono na Vyama vya Siasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vyama vya siasa vimekuwa vikitoka hadharani katika maadhimisho ya shughuli mbalimbali za Kitaifa na kuthibitishia Watanzania kwa umoja wao kama vyama vya siasa vinakubali kwamba Serikali imesimama na inatekeleza majukumu yake sawa sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hiyo, ni mifano michache ya kuonesha kwamba Serikali na vyama vya siasa vimekuwa na mahusiano ya karibu na mmekuwa mkishuhudia katika matukio mbalimbali Serikali iko na vyama vya siasa. (Makofi)

SPIKA: Ahsante. Mheshimiwa Stella Fiyao, Taarifa unayopewa ndiyo hiyo. Kwamba ushirikiano upo isipokuwa chama ambacho chenyewe hakitaki tu.

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Naendelea.

Mheshimiwa Spika, kwa kipindi cha miaka mitano tumeshuhudia mambo mengi katika Serikali yakiendelea, ikiwa ni pamoja na vyama vya siasa kuzuiliwa mikutano ya hadhara, jambo ambalo liko kikatiba na katika Sheria ya Vyama vya Siasa ya Mwaka 1992. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kipindi cha miaka mitano tumeshuhudia viongozi wa vyama vya siasa na wanachama, hususan wa vyama vya upinzani, wakikamatwa, wakishitakiwa na Serikali na kupewa kesi mbalimbali zikiwemo kesi za uhujumu uchumi, kesi za uchochezi na wakati mwingine kupewa hata fine kubwa ambazo haziko kisheria. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ndani ya miaka mitano…

SPIKA: Niliona taarifa, wapi? (Kicheko)

Aah, endelea Mheshimiwa Stella Fiyao. Aah, Mheshimiwa Waziri wa Fedha. (Kicheko)

T A A R I F A

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, katika nchi yetu na nchi nyingi ambazo hazijaendelea, tunaongea sana siasa badala ya uchumi. Hata tukiwa hapa kwetu nchini tunawatoa Watanzania wetu ku-concentrate kwenye masuala ya uchumi na kulenga zaidi siasa.

Mheshimiwa Spika, rai yangu kwa Mheshimiwa Mbunge, Mheshimiwa Rais ametoa kauli ambayo ni njema sana kwamba kesi zote ambazo hazina base zifutwe. Kwa kauli ya aina hiyo, ni nia ya dhati sana ya kiongozi wa kisiasa kusema.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ombi langu, kwa sababu tunajadili masuala ya kibajeti na tumetoka kujadili mpango, Waheshimiwa Wabunge, hebu tuchukue mwelekeo huo. Hata viongozi wa kisiasa ambao wako nje ya nchi, warudi tujenge nchi yetu, tujenge uchumi. Hata viongozi wa kisiasa ambao wako hapa wanajadili vitu ambavyo vinawatoa wananchi wetu kwenye umoja, tufuate kauli ya Mheshimiwa Rais ambayo ameonesha nia ya dhati. Tusimtoe kwenye dira hiyo ili tujenge uchumi.

Mheshimiwa Spika, tuna dola 1,080 tu, bado tuna deni la karibu dola 2,090 kufikia dola 3,000 ambayo ni lengo la uchumi wa kati wa kiwango cha juu ili tuweze kutafuta uchumi wa juu zaidi. Nawasilisha.

SPIKA: Mheshimiwa Stella, taarifa hiyo unapewa kwamba siasa zote baada ya uchaguzi ni hapa mjengoni. Unapokea?

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Spika, tunasubiri utekelezaji wa hicho alichokisema Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Spika, katika kipindi hicho pia tumeshuhudia Miswada Miswada ya Sheria za Vyama Vya Siasa ikiletwa ndani ya Bunge. Miswada hiyo ilikuwa na masharti magumu kwa vyama vya siasa ikiwa ni pamoja na kuvidhibiti, lakini mbaya zaidi ni kuingilia chaguzi za ndani za vyama vya siasa. Vyama vya siasa vilipotoa wito kwa Serikali wa kufanya maridhiano ya kujenga umoja wa Kitaifa, Serikali ilinyamaza kimya, mpaka sasa haijasema chochote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa maana hiyo basi, kwa mara ya kwanza kabisa katika historia ya vyama vingi, tumetengeneza hofu kubwa sana kwa wananchi. Tumezalisha hofu kubwa, hasa kwa wafuasi wa vyama vya upinzani kwani, wafuasi wengi wa vyama upinzani sasa hivi hawana amani kwa kuwa tu wako vyama vya upinzani. Mfano mzuri ni katika Mkoa wa Songwe, Jimbo la Tunduma…

SPIKA: Mheshimiwa Fiyao subiri. Mheshimiwa Katambi ulikuwa umesimama, taarifa. (Kicheko)

T A A R I F A

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, (KAZI, VIJANA NA AJIRA): Mheshimiwa Spika, naomba nitoe taarifa kwa Mzungumzaji kwamba katika Katiba yetu, Ibara ya 107(a) inasema kwamba chombo pekee cha utoaji haki kitakuwa ni Mahakama. Kwa msingi huo, mpaka sasa ninavyozungumza, nimefanya mawasiliano na Mkurugenzi wa Tume ya Uchaguzi, amethibitisha kwamba hakuna electoral petition yoyote ambayo imepelekwa kwa maana ya kwamba wakati wa uchaguzi kama kuna mtu aliumizwa angeweza kutumia avenue ya kisheria. Katika hilo nimpe Taarifa pia, kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, watu wote wana usawa, kwa mujibu wa Ibara ya 13. Usawa huu mbele ya sheria, haiangalii chochote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa Taarifa ninayompa, katika kipindi chote, hata wakati fulani ambapo tulijaribu kwenda kuzurura hivi, kuna kesi ambazo wakishinda upande mwingine, wataona Mahakama imetenda haki; wakishindwa kesi hiyo, inaonekana kwamba Mahakama haziko huru. Vilevile kwenye uchaguzi, wakishinda uchaguzi kama alivyoshinda pale Nkasi, Tume ilikuwa huru, lakini wakishindwa uchaguzi, Tume haiko huru. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Jean-Jacques Rousseau na Montesqueus walitoa msingi wa separation of power kwamba kutakuwa na Bunge, Serikali na Mahakama. Katika hivi, kuna institutional separation na functionale separation na personale separation. Kwa msingi huo, maana yake vyombo hivi vinasimamiana na ndiyo maana leo Jamhuri ya Muungano wa Tanzania iko huru, chaguzi zinafanyika kwa uhuru na hakuna kesi yoyote iliyopelekwa Mahakamani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilipenda nimpe Mheshimiwa Mbunge taarifa hiyo. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Fiyao shule hiyo umeielewa kidogo?

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Spika, naomba kuendelea. Mfano mzuri ni kwa wananchi wa Mkoa wa Songwe, Jimbo la Tunduma ambao wanaishi mpakani. Leo hii wananchi asilimia kubwa wanakimbilia nchi jirani ya Zambia kutokana na hofu kubwa kwa kutishiwa na Madiwani ambao wamepita, wako madarakani, wameendelea kuwatisha wananchi wakiwapa kesi za kuwasingizia na zisizokuwa na dhamana. (Makofi)

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Spika, hata wakipewa kesi zenye dhamana Watendaji wa Kata na Mitaa wamekataa kutoa barua kwa kusingizia kwamba wanatishiwa na Wakuu wa Wilaya kutoa barua za dhamana.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Stella dakika zako zimeisha. (Kicheko)

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Spika, muda wangu ulikuwa bado.

SPIKA: Dakika zako zimeisha.