Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Samweli Xaday Hhayuma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kuniona na kunipa nafasi hii awali ya yote nichukue nafasi hii, kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ametupa uzima na tunaendelea na shughuli zetu. Nimpongeze Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa uwasilishaji mzuri wa bajeti yake. Lakini niipongeze kazi nzuri inayofanywa na Serikali yangu, Serikali ya Chama Cha Mapinduzi, ukiangalia kazi iliyofanywa na Awamu ya Tano chini ya uongozi wa Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwanga tunauona, miradi ni mingi imetekelezwa na Awamu ya Sita sera yetu kazi inaendelea, maana yake tunaenda kukamilisha miradi ile yote. Na sisi tuna Imani na Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan kwamba, tutaenda kwa kasi zaidi kwani alikuwepo kwenye maandalizi yote na ile awamu ya tano kazi walifanya vizuri pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa naomba nijielekeze kwenye eneo la ajira. Hasa suala la ajira kwa vijana, vijana wetu wengi wamemaliza shule wako mtaani hawana kazi na tumekuwa na mjadala mkubwa kwenye eneo la elimu, kama elimu yetu kweli inaendana na mazingira ya kwetu.

Mheshimiwa Spika, lakini, vijana wengi kuanzia wale ambao hawajakanyaga darasani na wengine wana masters wanafanya kazi ya bodaboda. Ninachoomba Serikali yangu sikivu ya Chama Cha Mapinduzi kundi hili limekuwa kubwa, lina watu wa aina mbalimbali tujielekeze. Ile mifuko ya maendeleo ya vijana iangalie kundi hili muhimu na vijana hawa wa bodaboda ambao ni kundi kubwa kwa sasa, tuwatengenezee utaratibu maalum wa kuwatoa kwenye kazi ile ya bodaboda na hatimaye nao wapate uchumi kupitia kazi wanayoifanya.

Mheshimiwa Spika, tuwajenge ili waielewe kwamba kazi ya bodaboda ni sehemu ya ajira, lakini wanahitaji kuendelezwa kutoka hapo. Kwenye zile asilimia 4 za vijana zilizoko kwenye halmashauri, tuwaangalie hao ambao tayari wameshaanza kujishughulisha. Fungu lile la mfuko wa vijana ambao uko chini ya ofisi ya Waziri Mkuu, tuangalie hili kundi ambalo limeshaanza kujishughulisha, ili hatimaye waweze kupata shughuli zilizo imara ambazo zinaweza zikawaingizia kipato. Kwani kwa sasa, kundi lile linaonekana kama kundi la watu ambao hawana nidhamu kihivyo katika uendeshaji wa shughuli zao.

Mheshimiwa Spika, hawafuati sheria, wakati mwingine nao wana hasira na jamii nyingine. Ukiona kijana wa bodaboda ukimgusa tu, wanakusanyika utafikiri ni vita kwasababu, watu wamekosa amani. Sasa, tutengeneze mfumo ambao unaweza kuwatoa kwenye kazi ile wanayoifanya. Kazi ya bodaboda ukiifanya miaka miwili kifua hakifai kwasababu, wanavyoendesha hawafuati sheria. Hawachukui tahadhari, hawajilindi na pia wanakimbizana na polisi sana. Sasa badala ya kukimbizana na vijana hao tuwatengenezee utaratibu mahsusi wa namna ya kuwafundisha kufata sheria na zile shughuli zao ziweze kutambulika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema suala la vijana hasa na kwa eneo la kuwawezesha lakini pia tunalo eneo la ardhi. Ardhi imekuwa changamoto kubwa na sababu kubwa ni kwamba, ardhi tuliyonayo haiongezeki na sisi tunaongezeka. Na ukiangalia wengi ambao wana ardhi zilizo kubwa yawezekana ni wazee wetu ambao hawakwenda shule sana, au wakati mwingine hawajapata bahati na hizo ardhi wamepata kwa njia zile za asili. Sasa hivi watu wanaohitaji ardhi kidogo wameanza kuwa na elimu elimu kwasababu, ardhi yetu haijapimwa yote kumekuwa na dhuluma sana kwenye eneo la ardhi. Ninachoomba Serikali yangu sikivu ya Chama Cha Mapinduzi tujielekeze kwenye eneo la ardhi. Tuhakikishe watu tunawamilikisha ardhi zao kwa mujibu wa sheria, ili kuondoa migogoro mingi iliyojaa kwenye ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye ofisi za Wabunge nina uhakika wenzangu pia mnapata tatizo kama mimi, kuna malalamiko mengi ya wazee wetu kudhulumiwa ardhi zao. Na ukifuatilia, mzee utakuta hana nyaraka atakuambia mwaka sabini na ngapi aligawiwa ardhi hiyo, sasa mtu amechukua na kwasababu anajua jua kidogo taratibu, inakuwa ngumu sasa kubatilisha kwamba hajaipata kisheria. Na ardhi ni chanzo kizuri cha mapato, tukiipima ni imani yangu malalamiko ambayo tunayo kwenye upande wa TARURA tutapata fedha hapa. Kwani watu wataanza kulipa kodi za ardhi. Ninachoomba eneo hili tuliangalie kwa umakini mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niseme kidogo eneo la miundombinu kwasababu ni changamoto ya kila sehemu. Tumeongea sana namna ya kupata fedha ili angalau TARURA iweze…

SPIKA: Ahsante sana

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana naunga mkono hoja. (Makofi)