Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii adimu angalau dakika tano na mimi nichangie hotuba iliyo mbele yetu. Kwa sababu muda ni mchache basi mimi nitautumia muda huu kuongea mambo ya wapiga kura wangu walionituma kuwawakilisha hapa ndani.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunakwenda kukaa hapa zaidi ya miezi mitatu, tunachokifanya hapa ni kugawanya keki ya Taifa letu. Naomba nitoe ushauri kwa Serikali, tunapokwenda kuigawa keki hii lazima tujue jiografia ya nchi yetu inatofautiana sana, maendeleo ya kanda moja kwenda kanda nyingine inatofautiana sana, kutoka mkoa mmoja kwenda mkoa mwingine inatofautiana sana. Kwa hiyo, iwepo juhudi ya makusudi kuangalia ni namna gani ya kuisaidia ile mikoa au zile sehemu ambazo kimaendeleo zipo nyuma au kiuchumi zipo nyuma ili tuweze kwenda pamoja tusiwaache wenzetu. Natoa mfano hata Rais wa Awamu ya Nne aliamua kwa makusudi kuelekeza nguvu nyingi Kigoma, amejenga barabara nyingi sana kule,ili kwenda nao pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile tusisahau kuna element moja ilikuwepo tangu zamani kwamba Mikoa ya Kusini ilikuwa ni ya adhabu; miaka ya 80. Naomba niiambie Serikali ile element bado haijafutika, bado ipo pamoja na kwamba Serikali zote Awamu Tano zilizopita zimejitahidi sana kuipunguza lakini hiyo element bado ipo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi leo naongea zipo barabara kwenye nchi yetu zimepitiliza zaidi ya 20, life span ya barabara zetu ni miaka 20, tayari kwenye bajeti hii zipo barabara hizo zinakwenda kufanyiwa upembuzi yakinifu pengine kuondoa ile lami ili waweke nyingine kwa sababu life span yake imekwisha. Hata hivyo, mnapokwenda kufanya hayo mjue kwamba Nangurukuru - Liwale tangu tumepata Uhuru hatujaona lami. Mnapokwenda kufanya hayo mjue kuwa Mkoa wa Lindi hakuna wilaya hata moja ambayo inakwenda mkoani kwa barabara ya lami, ukiondoa Wilaya ya Kilwa na Wilaya ya Lindi Vijijini ambazo ziko kwenye hiyo barabara kubwa ya Kibiti-Lindi. Kwa hiyo, mnapokwenda kufanya hayo mjue kuna mikoa bado ipo nyuma inahitaji juhudi za makusudi kuisaidia ili twende pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe mfano mwingine, Wilaya ya Liwale ni Wilaya tangu mwaka 1975 leo tunazungumza ni miaka 46, lakini Wilaya ile mpaka leo Mkuu wa Wilaya, DED, OCD, Mganga Mkuu, Hakimu wa Wilaya na Polisi OCD hawana ofisi. Kwa mfano mzuri wale Mawaziri waliowahi kutembelea Wilaya ya Liwale wote tunawapokelea kwenye ile rest house ya Selous, vitabu vyote wanakuja kusainia pale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, asimame Waziri aniambie kama ameshawahi kuiona Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Liwale; Ofisi ya DED wa Liwale, asimame Waziri yeyote aseme ameshawahi kuona jengo la Polisi Wilaya ya Liwale. Wote tunakusanyika pale kwenye jengo la Selous. Tunaishukuru Selous, wametujengea rest house ambayo ndiyo inatumika mpaka leo. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, nawaomba sana…

MBUNGE FULANI: Aibu!

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ile wilaya ni ya mwaka 1975 na Mwalimu Nyerere alimpa Waziri wa Kwanza wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mzee Rashid Mfaume Kawawa Wilaya ile ya Liwale, lakini wilaya ile iko hoi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawaombeni sana, tunapokwenda kugawa keki hii, tuiangalie mikoa ile ambayo iko chini. Mkoa wa Lindi na Mkoa wa Mtwara ni mikoa ambayo iko nyuma kwa barabara, ndiyo maana tukaomba barabara yetu ile ya korosho inayotokea Mtwara inakwenda Newala – Tandahimba – Masasi – Nachingwea - Liwale mpaka Ruangwa, muikumbuke ili tuweze kuinua uchumi wa watu wa kusini.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)