Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Michael Constantino Mwakamo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibaha Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Naibu Spika, kama Wabunge wenzangu niungane nao kwenye kuiunga mkono hoja ya Hotuba ya Bajeti ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maneno hayo naomba nijielekeze kwenye hotuba yake ukurasa wa hamsini ambapo amejaribu kuelezea kwa kina namna ya mafanikio ya miradi mikubwa ukiwemo mradi wa reli, lakini kwa masikitiko makubwa kwenye eneo hili nimeisoma kurasa hiyo nimeona ameizungumzia sana SGR lakini naomba nilikumbushe Bunge hili na ninaomba niikumbushe Serikali yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwamba tunayo lugha tunayoitumia waswahili kwamba cha kale dhahabu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunazo reli mbili kubwa, tunayo reli ya kati ambayo inasimamiwa na TRC na tunayo reli ya TAZARA hizi reli, ni reli ambazo zimeweza kutoa huduma katika nchi hii kwa muda mrefu na zilikuwa na zina faida kubwa sana kwenye maeneo ambayo yamekatiza. Nikumbushe tu na Wabunge wengi naamini wataungana nami mkono kwamba wengi kati ya tuliohapa tumefanya biashara kwenye reli hizo ambazo nazitamka kwenye vituo mbalimbali zilizokuwa zimepita. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, zimesaidia stesheni zile kuwa sehemu za masoko ya kuuzia biashara za wakulima mbalimbali waliokuwa kwenye maeneo hayo. Nikitoa mfano kwenye maeneo ya Jimbo langu kwenye Stesheni ya Ruvu, Kwala, Ngeta, Msua, Magindu watu walikuwa wanakwenda kuuza mahindi yao. Kwa hiyo, ni moja ya sehemu kama masoko yalikuwa yanawaingizia kipato wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niwaombe Serikali pamoja na nguvu kubwa waliyoiwekeza na namna ambavyo wanaendelea kuifanyia ukarabati reli hii niwaombe waendelee kuongeza nguvu ili reli hii itumike na ikiwezekana kwa sasa waongeze ratiba ya kutumika ya abiria kutumika katika reli hiyo. Kwani sasa hivi ukiangalia ratiba imeharibika inapita kwa wiki mara moja kwa hiyo, maeneo mengi ya vijijini ambapo watu wanaitumia reli hii wamekosa kufanya huduma hiyo ambayo walizoea kuifanya kwa siku nyingi. Kwa hiyo, ningewaomba sana tuweze kuongeza nguvu ya kuwekea utaratibu wa miundombinu mizuri ili tuweze kuendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambambana hilo lipo jambo moja linaendelea sasa hivi kwa kweli kwenye eneo lile na ningeomba Mheshimiwa Waziri Mkuu na wasaidizi wake walichukue hili. Kuna watumishi kwenye Shirika la Reli na hasa hili la TRC kwa kweli kumbukumbu zinaonyesha mwaka 2007 Shirika hili lilikabidhiwa kwa shirika moja linaitwa TRL mkataba ulikuwa watumishi wale kabla hawajaenda kufanya kazi kwenye maeneo kwenye Shirika la TRL walitakiwa wamalizane kabisa na Shirika la TRC. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa masikitiko makubwa sana Shirika hili watumishi wale mpaka leo wapo, waliachwa na hajalipwa mafao yao na wamepokewa tena shirika lingine na wanaendelea kufanya kazi. Ningewakumbusha Serikali ebu waende wakazungumze na watu wale na ikiwezekana wawasaidie kulipa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia mwaka 2009 hao TRL walishindwa kuliendesha shirika na walirudisha tena TRL bado matatizo yakawa ni yaleyale wale waliofanya nao kazi malipo hawakuwapatia na mpaka hivi navyozungumza malipo yao hawana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kikubwa kuliko vyote wanachochama ambacho wenyewe ndio kinawasimamia maslahi yao kinaitwa TRAU chama hiki kimefumiliwa, viongozi wake wanatishwa na wakionekana wanasimamia maslahi ya wenzao wanahamisha kwenye shirika hili na kuwapatia shughuli nyingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, niwaombe sana Serikali na hasa wasaidizi wa Mheshimiwa Waziri Mkuu waende wakazungumze na watumishi wale, wawasikilize wanamatizo mengi. Ninayezungumza natokea kwenye ukanda huo nimeishi kwenye maeneo hayo nawafahamu vizuri changamoto wanazozipata watumishi hawa. Zamani walikuwa wanapelekewa mpaka maji na treni kwenye maeneo wanayofanyia kazi, sasa hivi hawana hizo huduma. Kwa hiyo, ningeomba sana Serikali iende ikawaangalie watu hawa na waweze kuwasaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lipo jambo lingine ambalo ningependa kulizungumza katika eneo ambalo nataka nilizungumzie sasa hivi ni suala zima la miradi ambayo Serikali imeielezea miradi ya kimkakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye jimbo langu wakati anapita ambaye ni Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano leo kwenye kipindi cha kampeni alitoa ahadi na ahadi ile naomba niithibitishie Serikali yake kwamba tumetekeleza vile ambavyo ametuelekeza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, alitwambia kulikuwa pale na mradi wa kujenga soko mradi ule uliingiliwa na changamoto mbalimbali na Serikali inajua. Rais wetu alitueleza kwamba endapo tutakuwa tumerekebisha kasoro zilizopo basi atakuwa yuko tayari kutuletea zile fedha na tuendelee na kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi hii niseme changamoto ambazo zilikuwa zinataka zisumbue kwenye eneo lile tumezimaliza na eneo tunalo na tuko tayari kwenda kuendelea na ujenzi. Kwa hiyo, nimuombe sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kutumia Wizara ya TAMISEMI, Naibu Waziri kama itampendeza aende pamoja na mimi baada ya Bunge hili akaone zile changamoto ambazo tumezimaliza ili tuweze kuendelea na mradi ule ambao ni mradi muhimu kwetu kwani utaongeza pato la halmashauri katika eneo letu na kuongezea mapato ya Serikali nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo dogo lingine kwenye maeneo yetu tunao matajiri ambao wamemiliki mashamba makubwa sana, mashamba ambayo yanaleta mgogoro mkubwa sana wa kimaslahi kwa sasa, wananchi wameingia mle wako katika muda mrefu sana na yale maeneo hawajatumia kwa miaka mingi sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunalo shamba moja linaitwa la TAN CHOICE la hawa watu wanaitwa Trans- continental liko Kikongo. Yule bwana hafahamiki, hajulikani aliko anatumia vibaraka wake kuwatisha wananchi wanaendelea na shughuli zao mle ndani. Naomba Serikali ije imalize tatizo lile ili wananchi waliowekeza kwenye eneo lile waweze kuongeza kipato cha nchi hii kwasababu wanalima na wanalipa kodi mbalimbali na maeneo yale wengine wameshaweka visima mle ndani, wameshajenga majumba mazuri, na wanaendeleza maeneo yale, kwa hiyo ningeomba sana Serikali ifike sehemu iweze kuja kutusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo kuna eneo ambalo hata Mheshimiwa Marehemu Hayati Dkt. Magufuli alipita pale Soga. Kuna shamba la Mohamed Enterprise hii imekuwa kero ya muda mrefu Mheshimiwa Rais alisema jambo hili limalizwe lakini mpaka leo halijamalizwa. Na Wizara ya Ardhi wanalijua lakini sijui tatizo liko wapi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimuombe Mheshimiwa Waziri Mkuu kwamba Serikali iende kwenye maeneo yale itumalizie matatizo haya ili wananchi waishi kwa amani waendelee na shughuli zao. Kwasababu sasa hivi wanazidi kuendelea, wengine wanavunjiwa majumba yao na mambo mbalimbali yanaendelea kufanyika kwa hiyo, ningeomba wizara inayohusika tukamalize tatizo hili. Baada ya kusema maneno haya naunga mkono hoja. (Makofi)