Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Shamsia Aziz Mtamba

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Mtwara Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. SHAMSIA A. MTAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi ili nami niweze kuchangia hotuba hii ya Waziri Mkuu. Awali ya yote, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya nzuri na leo hii nimeweza kusimama katika Bunge hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, miongoni mwa matatizo makubwa yanayowakabili wananchi wa Jimbo langu la Mtwara Vijijini ni maji. Ifike wakati Serikali itoe fedha kwa ajili ya kusambaza maji kutoka Mto Ruvuma hadi kwa wananchi wangu. Sijui kwa nini suala hili limekuwa gumu wakati Serikali ilitenga fedha na wananchi walifanyiwa uthamini mwaka 2015 ili mradi huu uanze. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo langu la Mtwara Vijijini lina kata 21, lakini ndani ya kata hizi 21, zote zimekuwa na changamoto kubwa sana ya maji ikiwemo Kata ya Mango pacha nne. Kata hii tokea tumepata uhuru haijawai kabisa kufurahia huduma hii ya majisafi na salama. Nikija Kata ya Libwidi, nayo imekuwa na changamoto kubwa sana ya maji; halikadhalika na Kata za Naguruwe, Kata ya Mkutimango, Kata ya Mbalawa na Makome, Kata ya Naumbu na Pemba Pwani nazo zimekuwa na changamoto kubwa sana ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wa Mkoa wa Mtwara kiujumla tuna changamoto kubwa sana ya maji, ndiyo maana tunataka mradi huu wa Mto Ruvuma ufanye kazi. Mradi huu wa Mto Ruvuma utaleta manufaa kwa maeneo mengi. Sitafaidika mimi katika jimbo langu tu, wanaweza kunufaika kwa kaka yangu Mheshimiwa Chikota; kwa kaka yangu Mheshimiwa Katani; utakwenda Nanyumbu; watakwenda Songea na Namtumbo. Kwa hiyo, mradi huu wa Mto Ruvuma una faida sana na utanufaisha maeneo mengi wataweza kupungukiwa na kero hii ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wa Mtwara uchumi wetu mkubwa ni Korosho. Naomba katika Bajeti hii, zao hili la Korosho lisiyumbishwe yumbishwe, mwachie bodi ifanye kazi yake. Naiomba Serikali irudishe Mfuko wa Pembejeo. Mfuko huu ulikuwa ni mkombozi kwa mkulima wa Korosho. Kwa hiyo, wananchi na wakulima wa Korosho wa Mtwara wamenituma, ni lini Mfuko huu wa pembejeo utarudishwa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mara nyingi nikisimama ndani ya Bunge nimekuwa nikizungumzia sana masuala ya matibabu kwa wananchi hasa kwa wananchi wangu wa Mtwara Vijijini. Kusema kweli wamekuwa wakipata taabu sana wanapokwenda katika hospitali zetu hasa wale wenye magonjwa makubwa kama moyo pamoja na figo. Wapokwenda katika hospitali zetu wanakuta Madaktari Bingwa hakuna, wanaambiwa waende Muhimbili. Kutokana na uchumi wa watu wetu wanashindwa kwenda Muhimbili. Hivyo, naishauri Serikali iweke utaratibu angalau kwa miezi miwili au mmoja wawe wanatuletea Madaktari Bingwa katika mikoa yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Sekta ya Uvuvi iboreshwe hasa katika Jimbo langu la Mtwara Vijijini. Sekta hii napenda iboreshwe katika maeneo yafuatayo: wavuvi wapewe elimu ya kisasa, wapatiwe mikopo na vyombo vya kisasa vya uvuvi kama mashine za boti, nyavu, ndoana, pamoja na vifaa vingine. Pia wavuvi wapewe semina mbalimbali za kuwajengea uwezo ili kuhifadhi hifadhi ya bahari. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na doria mbalimbali katika bahari zetu. Jeshi la Polisi wamekuwa wakifanya doria mbalimbali, lakini wavuvi wamekuwa wakilalamika kupigwa pamoja na kuchomewa nyavu zao. Kwa hiyo, naomba wasitumie nguvu kubwa, watoe elimu ya kutosha kwa wavuvi. Wakikamilisha haya, Serikali na Halmashauri wataweza kupata mapato ya kutosha kutokana na uvuvi. Pia zitengwe bandari maalum kwa ajili ya uvuvi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)