Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kupata fursa hii ya kuchangia bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Kwa kuanzia kabisa naomba kwa kipekee nianze kwanza kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu mama Samia Hassan Suluhu kwa kushika nafasi ya Urais. Ameanza vizuri na wote tumeona. Pia napenda kumpongeza Mheshimiwa Mpango naye kwa kuteuliwa na kushika nafasi ya Makamu wa Rais. Naye kwa kweli tumeona ameanza vizuri sana na kweli timu imekamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile napenda nimpongeze Waziri Mkuu. Kwa kweli Waziri Mkuu amefanya kazi kubwa sana. Ofisi yake inafanya kazi ya coordination ya Wizara zote, kwa hiyo mafanikio ambayo tumeyapata katika Serikali yetu ya Awamu ya Tano na yanayoendelea mpaka sasa hivi yote ni juhudi ya ofisi yake ambayo imeweza kuzi- coordinate Wizara zote na Serikali kwa ujumla. Wote ni mashuhuda wa mikakati ambayo tunayo mpaka sasa hivi ambayo ni endelevu. Pamoja na mafanikio yaliyoko kwenye miradi ya mkakati, lakini hata huko chini kwenye Halmashauri zetu tumeona mafanikio makubwa mno. Kwenye maji, kwenye umeme hata kwenye miundombinu tumeona mafanikio makubwa mno.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye jimbo langu tumeona mafanikio makubwa ya ujenzi wa hospitali, vituo vya afya vitatu ambavyo ni vya kihistoria na sasa hivi tunakamilisha tu ili viweze kuanza kufanya kazi vizuri. Kwenye miundombinu vile vile kwa mara ya kwanza kwenye historia tumeona barabara za kiwango cha lami zikianza kujengwa vijijini kwa ajili ya kwenda maeneo mahsusi ya wakulima wetu ili kuweza kufanya miundombinu ya vijijini iwe rahisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye umeme nako tumefanya vizuri sana. Kwenye Halmashauri yangu tulikuwa na vijiji vingi sana, vijiji karibu 200 lakini sasa hivi ndiyo Serikali inamalizia vijiji 40 vya mwisho ili tuweze kufikia asilimia mia moja ya vijiji vyote kuwa na umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na mafanikio hayo hapawezi kukosa changamoto, lakini changamoto zetu tulizonazo naona suluhisho lipo na tunategemea sana Serikali ya mama yetu Samia Suluhu Hassan. Ataweza kuzikabili hizo changamoto, sio kubwa kiasi hicho, ni ndogo na ukiangalia mpango wetu ambao tumeupitisha sasa hivi ni mpango ambao ni mzuri, unaangalia Taifa letu la Tanzania ni namna gani litakuwa shindani kwenye ukanda wetu lakini vile vile na kidunia. Kwa hiyo, kikubwa hapo ni kuangalia miundombinu ambayo itatufanya sisi tuwe washindani, tuweze kufanya vizuri ukitulinganisha na wenzetu huko duniani.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto ambazo tunaziona hasa kwa sisi tunaotoka majimbo ya vijijini ni miundombinu ya barabara. Barabara za vijijini ambazo zinahudumiwa na TARURA kwa kweli kwa asilimia kubwa zina hali mbaya sana. Tukiongelea kilimo bila ya kuwa na miundombinu mizuri ya barabara hatuwezi kufanikiwa kwa sababu gharama ya pembejeo itakuwa kubwa, tutashindwa kushindana. Lakini mazao yetu yatashindwa kwenda sokoni. Kwenye halmashauri yangu nina kilometa zaidi ya 1,000 ambazo zinahudumiwa na TARURA, lakini leo hii zaidi ya asilimia 90 hazipitiki. Wakulima wanashindwa kupeleka mazao yao sokoni.

Mheshimiwa Naibu Spika, sio hilo tu, vile vile hata halmashauri haiwezi kukusanya kwa sababu halmashauri yetu ambayo inakusanya karibu bilioni tatu kwa mwaka kutokana na mazao ya kilimo kwa miezi yote ambayo mvua zinanyesha wameshindwa kukusanya ambao ni karibu nusu mwaka. Sasa hii inaweza kutupeleka mahali pabaya sana. Tunakuja na bajeti zetu, ambazo ni nzuri kiasi hicho, lakini tunashindwa kutekeleza yale malengo.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile kulikuwa na ahadi ya Mheshimiwa Rais, hata Mheshimiwa Rais Samia naye aliahidi pale kwetu Mbeya. Kuna barabara yetu, kipande cha barabara ambacho kinasababisha sana ajali, Mlima Iwambi pale Mbalizi na wewe ni shuhuda, hatuna barabara nyingine zaidi ya hiyo, ukiachilia mbali msongamano wa pale Mbeya Mjini lakini ile barabara imeua wananchi wetu wengi. Mwaka 2018, Mheshimiwa Hayati Dkt. Magufuli aliahidi ijengwe haraka kwa kiwango cha lami. Nina Imani hata Viongozi Wakuu wengine waliwajibika kwa ajili ya hilo. Alikuja mama, wakati huo akiwa Makamu wa Rais naye akaahidi ijengwe haraka. Mpaka leo hakuna chochote kinachofanyika, sasa ukiangalia ile barabara ndiyo inabeba mzigo wote ambao ni karibu asilimia 75 ya mizigo yote inayotoka bandarini kwa ajili ya majirani zetu na hiyo barabara inapita katikati ya Jiji. Kunapita na ma-tanker ya mafuta pale ambayo ni hatari kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Waziri wa Ujenzi atuambie ni nini kinakwamisha hilo kwa sababu tuliambiwa mwanzoni kwamba hata wadau wetu wa maendeleo walikuwa tayari kuijenga hiyo barabara ya Mlima Nyoka sehemu za Uyole kwenda Songwe, lakini mpaka leo hakuna kinachoendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna barabara zingine pia ambazo ni za kimkakati; barabara ya Isyonje – Kikondo kwenda mpaka Makete ambayo tunategemea iweze kubeba mazao mengi sana, matunda matunda pamoja na sasa hivi kuna utalii kwa jirani zetu wale wa Makete. Hiyo barabara nayo pamoja na kuwekwa kwenye bajeti hatuoni kinachoendelea. Kuna barabara nyingine ambayo nayo ni ya kimkakati; barabara ya Mbalizi – Galula – Makongolosi ambayo inatokea mpaka kwa majirani zetu wa Mikoa ya Tabora na Singida. Hiyo barabara imekuwepo kwenye bajeti kwa miaka mingi, lakini mpaka leo na hivi juzi juzi ilikuwa haipitiki. Kuna barabara yetu nyingine ambayo ni ya kimkakati; barabara ya Mbalizi – Shigamba ambayo nayo inaenda mpaka Isongole karibu na mpaka wetu na Malawi, hii ni barabara ya kimkakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba hizi barabara zote zipewe kipaumbele ikiwemo na barabara zetu za vijijini, zina hali mbaya sana na ikiwezekana Waheshimiwa Wabunge tuangalie ni namna gani tuiwezeshe TARURA itusaidie ili wakulima wetu waweze kusafirisha mazao yao kutoka vijijini tuweze kupunguza gharama za mazao yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)