Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Abdallah Dadi Chikota

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nanyamba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami nichangie hoja iliyoko mezani kwetu. Nami nianze kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa mawasilisho ya hotuba yake; pili, nimpongeze Rais wetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri aliyoianza, lakini na ahadi yake ya kuyaenzi maono ya Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano, Hayati Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitajielekeza katika Sekta ya Kilimo na nitaanza na kuchangia kuhusu zao la Korosho. Tangu mwaka 2004 - 2017 tumeshuhudia ongezeko la uzalishaji wa Korosho na hii ilitokana na uwekezaji mkubwa ambao Serikali iliweka kwenye zao la Korosho. Kwa sababu mwaka 2004 tulikuwa na tani 72,000 na mwaka 2017 tulifikisha tani 313,000 za Korosho. Kwa hiyo, kulikuwa na uwekezaji mkubwa na ndiyo maana tukafanikiwa kwa kiasi hicho. Kuanzia mwaka 2018 kuna kushuka kwa uzalishaji wa Korosho na hii ni kwa sababu tulipunguza fedha katika Sekta ya Korosho. Nachukua nafasi hii sasa kuipongeza Wizara ya Kilimo, hususan Waziri na ndugu yangu Mheshimiwa Bashe kwa jitihada ambazo wanazichukua sasa hivi kuhakikisha pembejeo za uhakika zinapatikana kwa wakulima ili uzalishaji uanze kuongezeka. Hongereni sana Wizara ya Kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile, nizungumzie kuhusu Soko la Korosho. Ukurasa wa 30 wa Hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, ameweka kinagaubaga kwamba ushirika utaendelezwa na vile vile mauzo kwa mazao ya kimkakati utaendelea kuwa chini ya minada chini ya mfumo wa Stakabadhi Ghalani. Naiomba Wizara kurekebisha dosari chache zilizopo. Mfumo huu umeleta mafanikio makubwa sana kwenye zao la Korosho, naomba tuulinde ili wakulima wetu wanufaike na Korosho ambazo wanazalisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, hilo suala la TMX kwa sasa hivi kwa sababu tumeona kuna upungufu ambao umeanza kujitokeza, ni kama alivyowasilisha Mheshimiwa Waziri Mkuu hapa, litumike katika kutafuta masoko ya nje, lakini soko la ndani tuendelee na mfumo wetu wa Stakabadhi Ghalani, kwa sababu TMX imeonekana bado ina changamoto ambazo hazijapatiwa ufumbuzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile nijielekeze kwenye suala la miundombinu. Ukurasa wa 30 unaelezea vile vile suala la miundombinu, nami nijielekeze katika matumizi ya Bandari yetu ya Mtwara. Kuna uwekezaji mkubwa sana umefanywa katika Bandari ya Mtwara, zaidi ya shlingi bilioni 57 zimewekwa pale; na sasa hivi Bandari yetu ya Mtwara ina uwezo wa kupokea tani milioni moja. Naomba ule mradi wa kujenga reli kutoka Mtwara Mbambabay sasa uanze kutekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia Mradi wa Mchuchuma na Liganga sasa uanze ili bandari hii iweze kutumika ipasavyo. Sasa hivi tunasema Bandari ya Mtwara haitumiki kwa sababu Mradi wa Mchuchuma na Liganga bado hatujautekeleza, lakini tukiutekeleza mradi huu Bandari yetu ya Mtwara itakuwa effective. Kwa hiyo, muda umefika sasa, tutekeleze Mradi wa Mchuchuma na Liganga na pia tujenge reli kutoka Mtwara kwenda Mbambabay. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala la maji. Juzi hapa niliuliza swali kuhusu Wizara au Serikali imejipangaje kutumia maji ya Mto Ruvuma kwa ajili ya kutatua changamoto za maji zilizopo katika Mikoa ya Mtwara? Kama tumeweza kuthubutu kutekeleza kutoa maji kutoka Ziwa Victoria mpaka sasa tunafikisha mpaka Nzega, ni matarajio yangu sasa tutaanza kutumia maji ya Mto Ruvuma ili kujenga miradi mikubwa kwa ajili ya Mtwara Mjini, Lindi, Masasi, Tunduru hadi Songea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni muda muafaka sasa wa kuhakikisha kwamba, maji haya ya Mto Ruvuma yanatumika kutatua changamoto za maji iliyopo katika miji yetu ya Kusini ili kuhakikisha tunatekeleza Ilani ya Chama chetu ambayo inasema ifikapo 2025, basi vijijini tuwe tumepeleka maji kwa asilimia 85. Kwa Mkoa wetu wa Mtwara hali bado ni tete kwa sababu tumefikisha asilimia 60 tu. Tutazipata asilimia 25 zilizobaki tukianza kutumia maji ya Mto Ruvuma.

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza Wizara ya Maji kwa sababu wameshatuhakikishia kwamba Bajeti ya mwaka huu wataanza kutumia maji ya Mto Ruvuma, kwa ajili ya kutatua changamoto za maji katika Mkoa wa Mtwara na maeneo ya jirani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie kwa suala la mabadiliko katika Sekta ya Elimu. Kuna mjadala mkubwa unaendelea sasa hivi kuhusu elimu yetu. Naiomba Wizara ya Elimu ikubali hicho kilio cha Watanzania. Kwa kweli elimu yetu sasa hivi inahitaji mabadiliko makubwa. Kuanzia elimu ya awali, msingi, sekondari na vyuo vikuu. Hakuna mtu ambaye anabisha sasa hivi, kwa sababu falsafa yetu ya elimu ni Elimu ya Kujitegemea.

Mheshimiwa Naibu Spika, huko zamani ilikuwa mtoto wa Shule ya Msingi akimaliza anaweza kutumia maarifa yale kuishi katika mazingira yake. Sasa hivi tumebadilisha Elimu yetu ya Msingi inamwandaa mtoto kuingia sekondari. Tumepotoka, tufanye kila kiwango cha elimu kuwa kinajitosheleza. Elimu ya msingi ijitosheleze, Elimu ya Sekondari ijitosheleze na Elimu ya Chuo Kikuu iwe kamili, ijitosheleze. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tukifanya hivyo, hakutakuwa na malalamiko kwamba graduates wetu wakifika mitaani, wakifika mahali pa kazi, wanapwaya, hawatakuwa na maarifa ambayo yanasaidia katika kuzalisha katika maeneo yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Naunga mkono hoja. (Makofi)