Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Maimuna Salum Mtanda

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Newala Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Awali ya yote, nampongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hotuba yake nzuri pamoja na wale wote waliosaidia kuandaa hotuba ile. Nimeipitia hotuba yake, lakini naomba nami nichangie baadhi ya maeneo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na suala la watumishi, ambao ni walimu. Nilipata kusikia kuhusu ajira mpya za walimu kwamba sasa hivi Wizara imeweka mpango kwamba anayeomba ajira ya walimu anataja sehemu ambako anatakiwa kwenda kufanya kazi. Yaani kwenye application, katika maombi yake anaandika, mimi nataka kwenda sehemu fulani.

Mheshimiwa Naibu Spika, wazo ni zuri, lakini linaweza kuwa na changamoto kwa upande mwingine kwamba kuna maeneo hali yetu, maeneo yetu tunayafahamu, kuna maeneo miundombinu ni hafifu kiasi kwamba hayatapata watu wa kuomba moja kwa moja. Katika mazingira hayo kuna maeneo yatanufaika, yatapata watu wengi na kuna maeneo yatakosa kabisa watu wa kuomba kutokana na hali ya kijografia. Kwa hiyo, naomba tuangalie upya, wazo ni zuri kwamba litapunguza ile hali ya mtu akishapangiwa eneo, anakwenda kuomba abadilishwe, lakini italeta athari kwa upande mwingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia nizungumzie suala la uhaba wa walimu katika maeneo yetu. Sasa hivi nchi yetu iko kwenye uchumi wa kati, lakini tunataka tutoke hapo. Katika hali hiyo ni lazima kujiimarisha kuwekeza katika elimu ili hivyo ambavyo tunavitarajia viweze kwenda vizuri. Kuna uhaba mkubwa sana wa walimu katika shule zetu hasa za msingi pamoja na sekondari. Maeneo mengi ambayo yameadhirika ni yale ambayo yapo remote sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, ukija kwenye Jimbo la Newala Vijiji, kutokana na umbali kati ya kijiji na Kijiji; na sera yetu ni kwamba kila kijiji kiwe na Shule ya Msingi, unakuta jumla ya wanafunzi katika Shule ya Msingi kwenye shule fulani iliyopo katika kijiji fulani haizidi 100. Hesabu zinazopangwa kwa ratio ya mwalimu na mwanafunzi ni mwalimu mmoja na wanafunzi 45. Kwa hiyo, unakuta shule hiyo; mathalani shule yenye wanafunzi 80 au 90 inakuwa na walimu wawili tu, lakini ina madarasa kuanzia awali mpaka la Darasa la Saba.

Mheshimiwa Naibu Spika, walimu hao wana mzigo mkubwa sana. Kwa hiyo, naomba tuangalie, sawa ratio ni hiyo, lakini naiomba Wizara na kuishauri iangalie upya maeneo yale ambayo yako mbali lakini yana uchache wa wanafunzi ili angalau walimu waweze kuongezwa kwenye maeneo hayo na watoto wapate stahiki yake ili Tanzania ya viwanda iweze kuendelea vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naiu Spika, ukienda kwenye afya, kuna uchache pia wa watumishi katika maeneo hayo. Unaenda kwenye Dispensary unakuta mtumishi ni mmoja, anahudumia watu wote; wajawazito awapime yeye, wagonjwa wa Malaria awatibu yeye, kila kitu ni yeye.

Mheshimiwa Naiu Spika, kama binadamu anachoka, wakati anapochoka, anakuja mgonjwa ambaye anatakiwa apatiwe huduma ya haraka, naye ana mlundikano mkubwa wa wagonjwa, anashindwa. Anaposhindwa, mgonjwa analalamika kwamba sijapata huduma ipasavyo; lakini siyo kwamba kwa matakwa ya yule ambaye yuko pale anatoa huduma, ni kwa sababu ya uchache wa watoa huduma katika eneo lile, wagonjwa hawapati matibabu stahiki.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba Wizara iangalie eneo hili ili wananchi wapate huduma ipasavyo. Ukienda kwenye Jimbo la Newala Vijijini hali ya Watumishi wa Huduma za Afya ni mbaya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni ukosefu wa bei za uhakika kwenye mazao mchanganyiko hasa Mbaazi, Njungu pamoja na Mihogo. Wananchi wanajitahidi sana kulima, lakini mazao hayo hayapati bei. Matokeo yake kule kwangu Newala vijijini wanaamua kuhama makazi yao, wanaenda mikoa ya jirani kulima ufuta angalau ambao una nafuu ya bei. Matokeo yake, maendeleo ya Newala Vijijini yanazidi kuzorota; na kwa sababu wazazi wamehama, wanaondoka na watoto wao na kwa hiyo, kunakuwa na utoro mkubwa wa wanafunzi na mimba zisizotarajiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba Wizara ya Kilimo iangalie suala la bei ya mazao mchanganyiko kwa jicho la kipekee ili wananchi watulie kwenye maeneo yao waweze kufanya shughuli za uzalishaji mali.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie na suala la TARURA ambalo jirani yangu Mheshimiwa Cecil ameliongea. Hali ya barabara zinazohudumiwa na TARURA kule kwetu siyo nzuri sana. Hatuwalaumu wao, lakini tatizo ni fedha chache ambazo zipo katika mfuko huo. Barabara nyingi hazipitiki. Wakulima ambao wanazalisha mazao yao pembeni au walioko pembeni mipakani mwa Newala na Wilaya jirani wakati mwingine wanashindwa kusafirisha hasa zao la Korosho kutoka kule wanakolima kuleta kwenye maeneo yao ili wauzie kwenye vyama vya msingi ambavyo viko kwenye maeneo yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, matokeo yake Jimbo la Newala Vijijini kwa sababu ya ukosefu wa miundombinu ya barabara nzuri, linajikuta linapoteza mapato kwa sababu wanalazimika kwenda kuuza mazao yao kwenye wilaya na vijiji vya jirani hatimaye tunakosa mapato. Hasa ukienda Kata ya Mikumbi; barabara ya Mikumbi - Mpanyani haipitiki, barabara Namdimba - Chiwata haipitiki, barabara Mkoma - Chikalule haipitiki na barabara nyinginezo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba sana suala la TARURA liongezewe mapato ili barabara ziboreshwe na Jimbo la Newala vijijini liweze kupata kile ambacho kinatarajiwa kutokana na mazoa yanayolimwa na wananchi wa jimbo hilo. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana. Mheshimiwa kengele ya pili imeshagonga.

MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Naunga mkono hoja. (Makofi)