Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026

Hon. Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kwanza nitumie fursa hii kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia hoja, nikushukuru wewe mwenyewe kwa fursa hii pamoja na Naibu Spika kwa kuendesha vizuri mjadala huu na niishukuru Kamati ya Bajeti chini ya Mwenyekiti wake Mheshimiwa Sillo Daniel Baran, Mbunge wa Babati Vijijini pamoja na wajumbe wake kwa michango waliyoitoa kwa ajili ya kuboresha utekelezaji wa mpango huu.

Mheshimiwa Spika, jumla ya Wabunge waliochangia ni 111 wakiwemo 94 waliochangia kwa kuongea na 17 waliochangia kwa kuandika. Na niseme michango ya Wabunge wote kwa kweli imekuwa ya Kibunge kwelikweli na ninaamini itatusaidia katika kutekeleza mpango huu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa ajili ya muda, kabla sijaenda kwenye hoja moja moja, nianze kwanza kwa kuisemea hoja ya jumla ile ambayo ilikuwa inahusisha kama wasiwasi kidogo hivi kuhusu utekelezaji wa mpango huu.

Mheshimiwa Spika, dira aliyoitoa Mheshimiwa Rais tangia ameapishwa na ambayo ameendelea kutoa katika maelekezo mbalimbali, katika matukio mbalimbali ya kitaifa ni dira tosha ambayo inatutosha kutupa uhakika wa utekelezaji wa mpango huu unaofuata, Mpango wa Tatu.

Mheshimiwa Spika, niwakumbushie tu Waheshimiwa Wabunge pamoja na Watanzania ni maelekezo yapi yale yanayotoa dira ambayo yanatosha kutupa matumaini makubwa kwamba mpango huu tunakwenda kuutekeleza ili wote tuyazingatie.

Mheshimiwa Spika, la kwanza, kauli moja tu ya kwanza Mheshimiwa Rais aliyoitoa ni ile iliyokuwa inahimiza mshikamano katika Taifa letu. Alisema huu ni wakati wa kushikamana kuliko wakati mwingine wowote ule, tukishikamana mtu mmoja mmoja, viongozi, Serikali, sekta binafsi, ni dhahiri kwamba tunakwenda kuutekeleza mpango hii kikamilifu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili, Mheshimiwa Rais alisema atasimama imara kwenye masuala ya mapato na matumizi. Na sisi viongozi tukiondoka na dira hiyo, sisi kwenye ngazi ya Wizara tumeshajipanga kwenda kuhakikisha kwamba tunatekeleza maelekezo hayo ya kusimama imara kwenye masuala ya mapato na matumizi. Tukisimama imara kwenye masuala ya mapato na matumizi ni dhahiri kwamba tunakwenda kutekeleza mpango huu kikamilifu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo Mheshimiwa Rais alisema atasimama imara, alisema atasimama imara kwenye masuala ya rushwa, zero tolerance on corruption. Jambo hili tukitembea nalo Watanzania wote kama dira ni dhahiri kwamba tunakwenda kuutekeleza mpango huu kikamilifu.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo Mheshimiwa Rais alilisema kwa nguvu kubwa, tena waziwazi, ni kwamba kodi za dhuluma, no! Akasema nendeni mkakusanye kodi kwa kutumia akili zaidi badala ya nguvu zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni nadra sana kusikia kauli za aina hiyo katika viongozi wengi sana wa Kiafrika. Dhamira ya aina hiyo ni jambo ambalo litafungua ushiriki wa hiari na wa kizalendo wa Watanzania wote kwenda kutekeleza mpango huu wa maendeleo. Na ni sifa moja ambayo naamini itatusaidia pia kwenda kuhakikisha kwamba tunatekeleza mpango huu kwa uhakika.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine, alisema Mkaguzi Mkuu (CAG) usiwe na kigugumizi. Maana yake ni nini; maana yake anachofanya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ni kujenga taasisi katika utendaji wa kazi. Ameelekeza hilo na maana yake kila sekta na kila taasisi ziwajibike katika kufanya kazi ipasavyo.

Mheshimiwa Spika, lingine ambalo na Mawaziri wengine wamelisemea ni miradi mikubwa yakielelezo yote iendelee. Na tumeona hatua ambazo zinaendelea.

Mheshimiwa Spika, mengine ni masuala ya haki. Amesema kesi za uonevu zote zifutwe, zile ambazo hazina base, zile ambazo hazina msingi, zifutwe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini hakuishia hapo, akasema wananchi hawana fedha mifukoni, madeni yalipwe na vitu vingine ambavyo vinaweza kuchochea mzunguko wa fedha kwenye uchumi, na punde mzunguko wa fedha unapokuwa mkubwa maana yake tutakuwa na makusanyo na tunapopata makusanyo maana yake tunakwenda kutekeleza miradi hii ambayo tumeiainisha katika Mpango huu wa Maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge pamoja na Watanzania, kwa hiyo dira ya aina hii sote tunatakiwa tuiunge mkono, tumuunge mkono Mheshimiwa Rais ili tuweze kutekeleza mpango huu. Na naamini ni jambo ambalo litaleta tija.

Mheshimiwa Spika, tuache chachandu chachandu zingine. Maana yake kauli zenye dira zimetolewa halafu kunatoa vimaneno vimaneno vingine; tuache chachandu chachandu zingine, kauli aliyoitoa Mheshimiwa Rais na maelekezo aliyoyatoa yanatutosha kutupeleka kutupeleka mbele, yanatosha kutupeleka mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wengine wanasema tumesikia kauli lakini hatuna imani, tunataka tuone vitendo. Kazi ya Urais si kama tofali useme utamuona siku moja anabeba tofali hivi uone ndiyo kitendo kile pale amekifanya; haya maelekezo aliyoyatoa ndiyo yameshaanza kufanyiwa kazi na wengine wameshaanza kutoa ushahidi kwamba akaunti zimefunguliwa, wengine wameshatoa ushahidi kwamba kesi imefutwa, kati ya yale ambayo alikuwa ameyatolea maelekezo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na sisi wasaidizi wake tayari tunaendelea kuyafanyia kazi na kila taasisi ambayo inaguswa na maelekeo imeingia kazini kuyafanyia kazi. Mheshimiwa Askofu Gwajima yuko hapa angeweza kutuambia, walikuwepo wale waliokuwa na mashaka, wasaidizi wa Yohana, akawatuma, nendeni mkamuulize hivi yule ni yule tuliyekuwa tunamngojea au tuendelee kumngojea mwingine? Wala hakuwajibu kuwa ni mimi, akawaambia tu vipofu wanaona, viwete wanatembea, wakoma wanatakaswa na akasema heri mtu yule ambaye hana mashaka nami. Sasa na wale ambao wana mashaka tuwaambie ni huyu huyu, hakuna tunayemngojea. 2025 tunaweka comma tu lakini safari inaendelea, nukta ni mpaka 2030. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wengine wanadiriki kuruisha mishale mpaka kwa Hayati. Nilisikia mahali hivi wengine wanarusha mishale; mwacheni mzee apumzike. (Makofi)

(Hapa Waheshimiwa Wabunge walishangalia sana)

SPIKA: Nakuongezea Mheshimiwa Waziri wa Fedha; tena apumzike kwa amani. (Makofi)

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, nashukuru; tena apumzike kwa amani. Amemaliza kazi yake Serikalini, amemaliza kazi yake duniani, tuliosalia ndio tuna kazi, tuna wajibu sisi tunalifanyia nini Taifa letu. Si utaratibu wa Kiuchamungu kumrushia mishale mtu ambaye ametangulia mbele za haki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwa dira hii ambayo Mheshimiwa Rais ameitoa, nitoe rai na nirudie tena; twendeni, tuchape kazi, kazi iendelee na twendeni kila mmoja awajibike katika eneo lake ambalo anawajibika kufanya kazi ili tuweze kuutekeleza ipasavyo mpango wetu.

Mheshimiwa Spika, tukienda kwenye hoja moja moja; Kamati ilikuwa inapendekeza kwamba tuone umuhimu wa mikopo yote kuelekezwa katika kukamilisha miradi ya maendeleo, hasa ile ya kimkakati.

Mheshimiwa Spika, mapendekezo haya yamezingatiwa na yanakwenda sambamba kabisa na sheria, sura ya 5 kipengele Na. 5.7 na sehemu ya vipaumbele vya Mpango wa Tatu wa Maendeleo ya Taifa pamoja na kifungu cha tathmini na uhimilivu wa deni la Taifa katika Knauni ya 38 ya Sheria ya Mikopo, Dhamana pamoja na Misaada. Kwa hiyo, haya yamezingatiwa kwa Waheshimiwa Wabunge wote ambao walilisemea.

Mheshimiwa Spika, lingine ambalo kamati ilitolea maoni, iliona kuna umuhimu wa malengo kwenda sanjari na hatua stahiki zinazochukuliwa katika mpango wa utekelezaji ukiwa umekwenda sambamba na mikakati ya utekelezaji wa mpango, mkakati wa ugharamiaji wa mpango, mkakati wa ufuatiliaji pamoja na tathmini wa mpango pamoja na mapitio na mikakati ya mawasiliano ndani ya Wizara zetu.

Mheshimiwa Spika, Kamati pia ilitoa maoni kuhusu wakandarasi wa ndani, jambo hili pia limezingatiwa na matumizi mbalimbali ya fursa pamoja na ugharamiaji wa mpango; jambo hili pia limezingatiwa. Jambo lingine ambalo limeongelewa na Wabunge wengi kuhusu tathimini pamoja na ufuatiliaji, jambo hili tumezingatia taratibu ambazo zinatumika katika nchi nyingi, lakini pia zinazotumia utaratibu wa tathimini ambao wametungua sheria na zile ambazo wanatumia utaratibu wa ufuatiliaji wa ndani ya taasisi husika. Kwa msingi huo na kwa kutambua umuhimu wa kuwa na nyenzo za ufuatiliaji na tathimini Serikali imechukua hatua ya kuandaa mwongozo na ufuatilaji wa tathimini ili kukabiliana na changamoto mbalimbali ambazo zinajitokeza kuhusiana na masuala haya ya ufuatiliaji.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo Waheshimiwa Wabunge wamelisemea kwa kiwango kikubwa ni lile lililokuwa linasema bajeti za maendeleo zitekelezwe kama ambavyo zilikuwa zimepangwa na kupitishwa na Bunge; jambo hili linazingatiwa. Jambo lingine ni uwepo wa uwajibikaji wa kina katika matumizi ya fedha; jambo hili litazingatiwa na Mheshimiwa Rais tayari alishalitolea kauli na kauli hiyo ni mwongozo kwa taasisi zote, Wizara pamoja na idara zote huku Serikalini.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo lilitolewa maoni na Wabunge wengi ni kuongeza wigo wa kodi na mahsusi ilikuwa Serikali ipunguze kiwango cha kodi ya makampuni ili kuvutia uwekezaji wa ndani na kampuni za nje ili kuongeza multiplier effect katika kuimarisha ukuaji wa uchumi.

Mheshimiwa Spika, jambo hili limekuwa likifanyiwa kazi. Ukiangalia katika mwaka wa fedha 2018/2019 Serikali ilipunguza kiwango cha kodi hiyo kutoka asilimia 30 hadi 20 kwa miaka mitano kuanzia mwaka 2018/2019 hadi 2022/2023 kwa wawekezaji wapya wa viwanda vya madawa ya binadamu pamoja na viwanda vinavyotengeneza bidhaa za ngozi. Sambamba na hilo mwaka 2019/2020 Serikali ilipunguza kiwango cha kodi ya mapato ya kampuni kutoka asilimia 30 hadi asilimia 25 kwa kipindi cha miaka miwili kuanzia mwaka 2019/2020 hadi 2020/2021 kwa wawekezaji wapya wanaotengeneza taulo za kike.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo makampuni mapya yaliyosajiliwa na Soko la Hisa la Dar es Salaam yalitozwa kodi ya mapato ya kampuni ya asilimia 25 kwa kipindi miaka mitatu mfululizo kuanzia tarehe iliposajiliwa. Kwa maana hiyo Serikali itaendelea kuyaangalia masuala ya haya ambayo yalitolewa hoja na Waheshimiwa Wabunge kama ambavyo nimesema. Yale masuala mengine ambayo yametolewa na Wabunge yanayoashiria, ambayo yamebeba maudhui ya kikodi tutayaelezea kwa kina tutakapokuja kwenye Bajeti Kuu pamoja na Muswada ule wa sheria, yaani Finance Bill. Yale mengine ambayo yanawahusu sekta, sekta zinazohusika zitaendelea kuyaelezea punde tu tutakapokuwa tunaenda kwenye mawasilisho yale ya kisekta.

Mheshimiwa Spika, concern nyingine ya Wabunge wengi ilikuwa Mpango wa Tatu wa Taifa wa Maendeleo pamoja na kutekeleza masuala mengine. Ni vyema ukaweka viwango vya maisha tofauti ikiwa ni busara mpango huu uweze…

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana nitalisemea hili kwa kuwa naelekea dakika za mwisho za wasilisho.

Kwa kuhitimisha nirudie tena kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia hoja ya mapendekezo wa Mpango huu wa Taifa. Nichukue fursa hii kuzitakia Wizara, Idara zinazojitegemea Taasisi na Wakala za Serikali, Sekretarieti za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kutekeleza ipasavyo falsala yetu ya kazi iendelee, na hivyo wajielekeze katika kusimamia utekelezaji wa mpango huu ili tuweze kufikia azma yetu ya kujenga uchumi shindani na viwanda kwa maendeleo ya watu.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo hayo naomba sasa kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naafiki.