Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026

Hon. Mashimba Mashauri Ndaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi hii kukushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kutoa mchango wangu kwenye Mpango wetu wa tatu kwenye mipango ya miaka mitano ya nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, sekta yetu ya mifugo na uvuvi ni sekta ya uzalishaji, na Waheshimiwa Wabunge wamejikita sana kuchangia michango mingi inayohusiana na sekta hii ilikuwa inalenga changamoto ambazo zinakabili sekta yetu ya mifugo na uvuvi. Kwahiyo Waheshimiwa Wabunge mimi nichukue nafasi hii kuwashukuru sana kwasababu mmeelezea changamoto ambazo zinakabili sekta ya mifugo na uvuvi ili isiweze kuzalisha sana kama ambavyo inategemewa; lakini pia mmeshauri kwa namna gani sekta hii iendeshe mambo yake ili iweze kuwa na tija kubwa kwa Taifa na iweze kuchangia kwa sehemu kubwa kwenye uzalishaji kwa Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, sasa changamoto nyingi zilizoelezewa na Waheshimiwa Wabunge, Waheshimiwa Wabunge kama wanane hivi wamechangia kwenye sekta hii; moja ya changamoto waliyochangia Waheshimiwa Wabunge ni changamoto ya miundombinu hasa inayohusiana na mifugo ndio michango mingi imetoka hapo. Miundombinu inayohusiana na mifugo juu ya afya ya mifugo lakini pia juu ya miundombinu wezeshi ili kufanyabiashara ya mifugo iwe rahisi. Pia juu ya afya ya wanyama au afya ya mifugo yako masuala ya majosho, yako masuala ya malambo, visima, yako masuala ya kliniki za mifugo ndio hayo ambayo yanakwaza na yametajwa kwa sehemu kubwa na Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Spika, nipende tu kulihakikishia Bunge lako kwamba sisi pia Wizara ya Mifugo na Uvuvi tumewasikia na tutajitahidi kwa kadri itakavyowezekana kwa kadri ambayo tutakuwa tukipata fedha kwa kadri ambavyo tutakuwa tukipata rasilimali fedha kutoka kwa Serikali au kutoka kwa wadau wengine, tutajitahidi sana kumaliza au kupunguza matatizo ya miundombinu kwenye sekta hii ya mifugo.

Mheshimiwa Spika, kwenye bajeti ya mwaka ujao ambayo Waheshimiwa Wabunge mtatupitishia, tumeweka ujenzi wa majosho, malambo, kliniki na visima ili kuhakikisha kwamba afya ya mifugo yetu inakuwa bora ili mifugo yetu nayo iwe bora kuwezesha kutupa nyama bora na fedha nyingi ukilinganisha na leo. Tuondokane na ule usemi ambao hata Mheshimiwa Rais aliusema: “Mfugaji anakonda na ng’ombe mwenyewe au mfugo wenyewe nao unakonda”

Mheshimiwa Spika, sasa angalau mwakani tumeweka bajeti ya majosho 129, tutaomba Waheshimiwa Wabunge mtusaidie kutupitishia. Pia tumeweka bajeti ya malambo na visima kadhaa; tumeweka bajeti ya clinic kadhaa, tunaomba Waheshimiwa Wabunge mtusaidie ili angalau tuweze kusukuma mbele uzalishaji katika Sekta ya Mifugo na Uvuvi uweze kuongezeka.

Mheshimiwa Spika, suala lingine ambalo linakwaza uzalishaji ambao limetajwa na Waheshimiwa Wabunge hasa upande wa uvuvi ni juu ya Sheria yetu ya Uvuvi ya mwaka 2003. Napenda kuliambia Bunge lako sheria hii ya mwaka 2003 ilifanyiwa marekebisho mwaka 2009, lakini ikatengenezewa pia Kanuni zake mwaka 2009. Mwaka 2020, Kanuni zinazoongoza utekelezaji wa sheria hii zilifanyiwa tena marekebisho. Kwa hiyo, tumeendelea kufanya marekebisho ya Kanuni zetu ili kuwarahisishia wavuvi waweze kuvua samaki wale ambao wanatakiwa na wale ambao wao pia wavuvi wetu watajipatia fedha au kipato.

Mheshimiwa Spika, lakini tumeendelea pia kufanya mapitio ya Kanuni zetu, mwaka huu tulikutana na baadhi ya Wabunge na nikawaeleza kwamba tunafanya tena mapitio ya hizi Kanuni tujaribu kuona baada ya kuzitumia wavuvi wamesema ni Kanuni ipi ambayo bado inaendelea kukwaza. Kwa hiyo, tunaendelea kupitia tena Kanuni zetu na nimewaagiza TAFIRI waanze kufanya utafiti na walishaanza kufanya ili watuletee ni Kanuni zipi ambazo zinakwaza uvuvi kwenye bahari, maziwa na hata sehemu nyingine ili tuzifanyie marekebisho kusudi tu uzalishaji kutoka kwenye sekta ya uvuvi uweze kuongezeka. Niseme tu kwamba marekebisho haya yanaendelea na lengo lake ni kuboresha ili kwamba uzalishaji kwenye sekta ya uvuvi uweze kuongezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wakati watu wetu wanapita kule na kujaribu kuangalia vipimo au kupima nyavu zetu zinazotumika ili pengine kuangalia ni nyavu zipi zinatumika kwenye uvuvi haramu, kulikuwa na kipimo kinaitwa match gauge na kingine ni vernier caliper. Match gauge ilikuwa inawapunja wavuvi wetu, wavuvi wakalalamika na wakaja Ofisini kwangu tukarekebisha hiyo hali. Sasa tunatumia vernier caliper badala ya match gauge ili kupima nyavu ipi inafaa kwa ajili ya uvuvi. Kwa hiyo, utagundua malalamiko mengi yanayohusiana na kukamatwakamatwa wavuvi wetu yamepungua sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)