Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026

Hon. Asia Abdulkarim Halamga

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026

MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia Mpango huu wa Tatu wa Maendeleo.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kumpongeza Waziri kwa uwasilishaji mzuri. Baada ya kumpongeza niombe nijikite katika sehemu mbili, moja ikiwa sehemu ya viwanda na ya pili ikiwa sehemu ya miundombinu.

Mheshimiwa Spika, naomba nianze na miundombinu. Awamu ya Nne ya Serikali yetu iliyopita ilifanikiwa sana katika kuhakikisha kwamba inaunganisha barabara katika kila mkoa ili kuhakikisha kwamba huduma za maendeleo zinapatikana kwa wananchi, lakini pia kupunguza gharama za maisha kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Spika, Serikali ile ya Awamu ya Nne iliamua kujiwekeza katika chombo kinachoitwa TANROADS. Katika kujielekeza katika chombo cha TANROADS tuliweza kufanikiwa kuunganisha mikoa mingi, na wote ni mashahidi, mikoa mingi sasa inafikika kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Spika, ili kukuza uchumi wetu ni lazima sasa Serikali ione kwa namna gani ambavyo TANROADS wanapata asilimia 70 ya fedha lakini tuna chombo kingine ambacho tumeamua sasa kuboresha kwa maana ya barabara za vijijini, chombo kinachoitwa TARURA.

Mheshimiwa Spika, na tukiweza kufanikiwa kuiboresha TARURA tutafanikiwa kufungua barabara zetu za vijijini na tutarahisisha huduma. Huduma ya kwanza tutakayoweza kurahisisha ni huduma ya pembejeo na kuwasaidia wakulima wetu kwasababu tunalenga uchumi wa kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuombe sasa kwa kuwa TANROADS sasa hivi wamebaki kuunganisha maeneo machache lakini pia maeneo yao makubwa ni kuangalia marekebisho pale ambapo panaharibika. Kwa maana hiyo kazi kubwa TANROADS imeshaifanya. Basi tuombe sasa Serikali iamue kuwekeza nguvu katika chombo chetu cha TARURA na kuongezewa fedha ili tuweze kufanikiwa kuleta maendeleo kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kuchangia hapo kwenye chombo cha TARURA kuongezewa fedha ili kuweza kukuza uchumi, niombe sasa nijielekeze katika kilimo cha alizeti, hasa kwa upande wa Kanda ya Kati. Serikali ilikuja na mpango mzuri na maono bora ya kuhakikisha kwamba kunaanzishwa kwa viwanda mbalimbali kulingana na jiografia ya maeneo yetu.

Mheshimiwa Spika, kuna zao la alizeti ambalo kwa kiasi kikubwa linalimwa katika Ukanda huu wa Kati. Tuombe sasa kuanzishwa kwa kiwanda kikubwa cha mafuta ya alizeti ili kukuza zao la alizeti katika kanda hii ya kati. Na namna ya kuanzishwa kwa kiwanda hicho kikubwa maana yake ni kwamba kitabeba viwanda vidogovidogo, kitarahisisha wakulima kuongeza bidhaa na kuwa na soko la ndani la uhakika kwa maana tutakuwa tuna kiwanda kikubwa lakini kile kiwanda kikubwa kitakuwa kimebeba nembo ya Tanzania, ambapo baada ya kupata soko la ndani la uhakika tutatoka kwenye soko la nje, litakalokuwa limebeba brand ya Tanzania na kuhakikisha kwamba tunapata soko la uhakika la huko duniani huku ndani tukiwa tumeshakidhi vigezo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika kuhakikisha kwamba zao hilohilo la alizeti pamoja na kuanzishwa kwa kiwanda kikubwa kitakachowasaidia wakulima wetu wa wafanyabiashara, tuhakikishe pia tunatoa mbegu iliyo bora kwa muda na wakati kwa wakulima wetu ili kuweza kufanikisha dhana tuliyoamini, dhana ya viwanda.

Mheshimiwa Spika, naomba nimalizie kwa Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Ajira na Vijana. Tunao vijana wenzetu kwenye makampuni na mashirika mbalimbali ambao wameweza kupata ajira zinazoweza kuwasaidia.

Mheshimiwa Spika, lakini tunaomba Wizara iende ikaangalie, vijana wengi wanafanya kazi lakini hakuna mikataba inayowalinda. Hivyo, tukiweza kusaidia vijana wakapewa mikataba na ajira za kudumu ama mikataba inayoeleweka, itaongeza mapato kwasababu wataweza kupata sehemu ya kulipa kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa siku ya leo mchango wangu ulikuwa ni huo, naomba nikushukuru kwa kunipa nafasi. (Makofi)