Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026

Hon. Joseph Zacharius Kamonga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ludewa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026

MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kutoa maoni yangu kwenye Mpango huu wa Tatu wa Maendeleo ya Taifa. Nianze kwanza kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwa wasilisho zuri la Mpango na hasa vipaumbele sita vya Taifa letu kwa ajili ya kuleta maendeleo. Wananchi wa Ludewa wanaipongeza sana Serikali ingawa wana mashaka bado sababu wakati wa awamu ya nne hii miradi ya Mchuchuma na Liganga walishaandaa hadi eneo kwa ajili ya uzinduzi. Mheshimiwa aliyekuwa Rais Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete alishaandaliwa kwa ajili ya kwenda kuzindua Miradi ya Mchuchuma na Liganga lakini bahati mbaya mpaka sasa muda mrefu umepita.

Mheshimiwa Naibu Spika, licha ya kuwa Serikali imeingiza miradi hiyo kwenye kipaumbele na imeweka mpango, lakini bado wananchi wana mashaka na hilo. Mimi kama kiongozi wao nimeendelea kuwapa moyo na kuwaaminisha kwamba Serikali ya sasa ni Serikali ya vitendo, kwa hiyo naomba Mheshimiwa Waziri tuwe pamoja kwenye hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo wananchi ambao wameathirika na Mradi wa Mchuchuma na Liganga nao wamesubiria fidia kwa muda mrefu sana takribani bilioni 11 ni pesa chache sana kwa Serikali iwapo dhamira ya kuwafuta machozi wananchi hawa ili waweze kuondoka kwenye maeneo haya wakafanye shughuli zao katika maeneo mengine. Toka miaka ya sabini wamezuiwa kabisa kuendeleza maeneo haya na fidia hawalipwi, kwa hiyo wananchi wanaona kama Serikali imekuwa katili kwao, hawa ni wananchi wa Nkomang’ombe na wananchi wa Mundindi na Amani ambao wanalinda mali hizi kwa muda mrefu sana. Kwa hiyo naomba hili la fidia litekelezwe, kwa sababu tunavyozidi kuchelewa thamani ya ardhi inazidi kupanda, tutaingia mgogoro mkubwa sana na wananchi iwapo hatutachukua hatua mapema. Kwa hiyo, hil ni muhimu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kwa kuwa Wilaya hii ina miradi mikubwa miundombinu yake bado ni changamoto kubwa. Barabara inayoanzia Itoni kwa Mheshimiwa Deo Mwanyika, Lusitu mpaka Ludewa na kwenda Manda takribani kilometa 211.44. Tunashukuru Serikali imetutengenezea lami kwa kiwango cha zege, lazima tuwe waungwana tukubali na tushukuru, kilometa hamsini ambapo thelathini zimekwisha kukamilika. Kwa hiyo tunaomba barabara hii ikamilike yote kwa sababu Serikali hii imetuletea meli kule Ziwa Nyasa ambazo zinatoa mchango mkubwa sana kuinua uchumi wa mwambao, lakini bahati mbaya meli zile zinakosa mzigo wa kutosha kwa sababu barabara hizi hazijaunganishwa. Kwa hiyo uchumi huu na miundombinu yake lazima viwe na mawasiliano kwa sababu sekta moja ya uchumi inaweza kutoa mchango kwenye sekta nyingine. Sambamba na hilo wananchi wa mwambao wanaomba kuwe na kituo cha meli kwenye Kata ya Makonde ili iweze kusaidia hali hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile Wabunge wengi hapa wamechangia kwamba wananchi wengi Watanzania ni maskini sana na wanaishi vijijini zaidi ya asilimia 75. Kwa hiyo tukijitahidi kutafuta masoko ya mazao kwa maeneo ya vijijini, tunavyosema uchumi jumuishi, uchumi shirikishi tutawagusa wananchi ambao wanaajiriwa kwenye sekta ya kilimo. Waheshimiwa Wabunge wengi ambao wanatoka maeneo vijijini kama mimi ambako kuna wakulima wengi, wamezungumzia mazao yanakosa masoko. Kwa mfano wilaya yangu wanaongoza kwa kulima mahindi, nitatoa takwimu chache, kwa mwaka 2019/2020 tani zilizozalishwa zilikuwa 110,800 lakini ambazo kwa makisio zinatosha kwa matumizi ya chakula ni tani 46,852, tani za ziada ni 63,239 na ambazo mnunuzi mkuu wa mahindi kwa kule ni hawa wanaitwa NFRA.

Mheshimiwa Naibu Spika, NFRA walikwenda wakanunua tani 709 tu. Kwa hiyo unakuta tani zaidi ya 62,000, mahindi ya wananchi yalioza kwa kukosa soko, kwa hiyo ni muhimu Serikali ikaona haja sasa ya kutafuta wawekezaji waweze kufungua viwanda kwa ajili ya kuzalisha vyakula vya mifugo, viwanda kwa ajili ya kusaga nafaka na kwenda kuuza katika maeneo mbalimbali ili kuweza kuongeza soko kwa wakulima.

Mhehimiwa Naibu Spika, wananchi wengi wa Jimbo la Ludewa na maeneo mengine wanalalamikia sana changamoto ya vijana kuhitimu vyuo vikuu na kukosa ajira. Kwa hiyo, tunavyozungumzia katika Ilani ya Uchaguzi kuzalisha ajira 8,000,000 wanaona kama ni chache sana, kwa hiyo wanaamini sekta mbalimbali hizi kama zitaanzishwa za viwanda na mikopo ya vijana kama ambavyo Mheshimiwa Nyamoga amezungumzia, tunaweza tukafungua soko la ajira.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata kwenye utumishi wa umma kuna pengo kubwa sana katika ile Seniority, kwa hiyo unakuta wako Principal Officer lakini wale Juniors hakuna, kwa hiyo kuna kupindi fulani tutazalisha tatizo kwenye utumishi wa umma na tutalazimika wakati mwingine kutengua baadhi ya kanuni za utumishi wa umma na sheria. Kwa mfano inakwambia ili mtu awe Mkuu wa Idara lazima awe amefanya kazi miaka saba, sasa itafika kipindi tutawakosa hawa watu, kwa hiyo lazima tuangalie na athari ambazo zinaweza kutoka hapo mbele.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hili watumishi wa umma muda mrefu kidogo hawajapandishiwa mishahara yao. Bahati nzuri aliyekuwa Rais wetu Mheshimiwa Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli apumzike kwa amani huko aliko, wakati akiomba kura aliahidi kwamba awamu hii anakwenda kutatua tatizo la ajira. Kwa hiyo ili kumuenzi, tumsaidie mama yetu mama Samia Suluhu Hassan kuweza kuajiri vijana ambao wengi hawana kazi. Hapa kwa kwakweli tutakuwa tumeongeza tija. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile na hii hoja ya kupandisha mishahara, nayo Mheshimiwa Rais wetu alikuwa ameshaahidi kwamba safari hii atapandisha mishahara na hili ni kwa mujibu wa sheria za utumishi wa umma, Sheria ya mwaka 2002 inasema mtumishi wa umma atapanda daraja kila baada ya miaka minne wengine, wengine miaka mitatu, kwa hiyo kupuuza sheria wakati ipo wakati mwingine sio hekima sana, ni heri kuifuta. Kwa hiyo tuangalie hiyo, tuweze kuangalia watumishi wa umma kama ambavyo alama za Chama Cha Mapinduzi ni jembe na nyundo; jembe ni wakulima na nyundo ni wafanyakazi. Kwa hiyo tuwaenzi kwa sababu hata kwenye alama ya Chama cha Mapinduzi watumishi wa umma wamo na hawa wafanyakazi wamo.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile hata wafanyabiashara kero zao bahati nzuri mama ameanza kuzishughulikia…

(Hapa kengele ya kwanza ililia)

MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Naibu Spika, sijui ni kengele ya pili, au ya kwanza?

NAIBU SPIKA: Ya kwanza, malizia mchango wako.

MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, asubuhi nimshukuru Mheshimiwa Waziri William Lukuvi na Mama Mabula, walezi wangu hawa, wamenilea vizuri na nawaheshimu sana, walitoa ufafanuzi kwa swali alilouliza jirani yangu Mbunge wa Nyasa, Mheshimiwa Stella Manyanya kuhusiana na ile capital gain tax.

Mheshimiwa Naibu Spika, bahati nzuri na wewe ni Mwalimu wangu pale Law School, sheria inayoanzisha kodi hii ni Sheria ya Kodi ya mwaka 2004, Sura 332 na kuna sheria nyingine ambazo zinasimamia ambayo ni Sheria ya Ardhi Na. 4 ya mwaka 1999 na Sheria ya Usajili wa Ardhi, Sura ya 334, rejeo la mwaka 2002.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto ambazo zipo kwenye kodi hizi ni kwamba ili mwananchi aweze kuhamisha umiliki wa ardhi yake ambayo amenunua au amepewa kama zawadi, anakwenda Ofisi zaidi ya moja, Ofisi za Ardhi zinahusika katika kufanya uthamini, TRA wanakwenda kukadiria kodi. Kwa hiyo ile ya mwananchi nenda hapa, nenda hapa imekuwa kama usumbufu, kwa hiyo kama wangeachiwa Wizara ya Ardhi kwa sababu Serikali ni moja, hii kodi wangeweza kuisimamia vizuri, nina imani sana na Mheshimiwa Lukuvi na Mama Mabula.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile Kamishna wa TRA amepewa mamlaka makubwa sana kwenye hii kodi, kwa hiyo hii nayo inachanganya sana wananchi. Pia ina mlolongo mrefu na kupoteza muda wa mlipakodi, ile nenda sijui kafanye valuation, kwa hiyo wananchi wengi wanabaki na nyaraka wanajenga bila kubadilisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika maeneo ambayo hayajapimwa vile vile kodi hii haitozwi, kwa hiyo kuna maeneo mengine katika miji mikubwa ambayo hayajapimwa transaction kubwa zinafanyika, lakini watu hawalipi kodi. Kwa hiyo kuna maeneo ya kuangalia na hata asilimia yenyewe kumi ni asilimia kubwa sana. Mtu ameuza nyumba milioni 100, asilimia kubwa, akiambia asilimia 10 anaondoka anaenda nyumbani na nyaraka. Kwa hiyo hapa tunaweza tukaangalia kuna mambo ambayo yanaweza yakarekebishwa ikiwa ni pamoja na elimu kwa mlipa kodi na vilevile kuboresha namna ya ukusanyaji. Mwananchi asisumbuliwe kuambiwa nenda hapa, nenda hapa, nenda pale, kuwe na mtu mmoja anasimamia kama ni wa Wizara ya Ardhi, afanye uthamini yeye kwa sababu ana watalaam, akusanye yeye kodi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono pia Waheshimiwa Wabunge waliozungumzia ile kodi ya majengo (Proper tax) ile wangerejeshewa halmashauri ili kuweza kuongeza mapato. Kwa sababu wana wataalam wa GIS wanaweza wakaweka vizuri mifumo ya ukusanyaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)