Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika Mpango huu wa Tatu wa Miaka Mitano wa Maendeleo wa mwaka 2021/2022 – 2025/2026. Nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango pamoja na Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti kwa wasilisho zuri sana walilotoa hapo jana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mpango wa Maendeleo ambao Waziri aliwasilisha jana, una vipengele vitano ambavyo wanalenga kuvitekeleza. Nami nitajikita kwenye eneo la tano katika ule mpango na eneo hili ni lile linalozungumzia kuendeleza rasilimali watu ambapo Serikali inategemea kuanzisha Program za kuendeleza maarifa na ujuzi kwa kuwasaidia vijana wetu kuanzia ngazi ya Elimu ya Awali mpaka Vyuo Vikuu. Kuna tatizo hapo. Kwa hiyo, nitalenga kwenye hili na nitaangalia mchango wa vijana kwenye kuchangia pato la Taifa, kwenye Sekta za Kilimo, Mifugo na Uvuvi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni ukweli usiojificha kwamba kilimo ni kitu muhimu sana; mifugo na uvuvi ni sekta muhimu katika maendeleo ya nchi yetu na karibia kila Mbunge aliyesimama hapa leo hii amelisema hilo. Nafasi ya vijana kwenye kilimo sasa hivi siyo nzuri sana, vijana wengi hawashiriki kwenye kilimo. Wanaoshiriki kwenye Sekta ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi ni wazee ambao wameshachoka na hawajaacha urithi mzuri kwa vijana wetu kushiriki katika hizi sekta. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, program hii ya Serikali nilitaka nishauri kwamba ni program muhimu sana kama tutashirikisha vijana na kama tutasaidia vijana, tuwafunze vizuri ili waweze kushiriki kikamilifu kwenye kuboresha Sekta ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi waweze kuchangia kikamilifu katika pato la Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, vijana wanaomaliza Darasa la Saba, Kidato cha Nne, sekondari Kitado cha Sita, Vyuo vya Kati na Vyuo vya Juu, wengi wao pamoja na kwamba ni watoto wa wakulima, wafugaji na wavuvi wakimaliza masomo hawaendi kwenye kilimo. Wanakimbilia mijini, wanakwenda kuendesha bodaboda, wanakwenda kuwa machinga, wanakwenda kuajiriwa. Kwa nini wanafanya hivyo? Wanafikiria kabisa kwamba kilimo, ufugaji na uvuvi ni kazi duni kitu ambacho sio sawa kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama Serikali itawekeza na kufuata ushauri ambao nitatoa leo hii hapa, nina hakika tunaweza kuwahusisha vijana wetu katika hizi sekta ambazo nimezitaja na watatoa mchango mkubwa sana katika kukuza uchumi wa nchi yetu. Sasa nitoe ushauri kwa Wizara ya Elimu na TAMISEMI ikiwezekana.

Mheshimiwa Naibu Spika, Rais alivyokuwa anawaapisha Makatibu Wakuu na Viongozi wa Taasisi za Serikali alielekeza tubadilishe mitaala. Alisema mitaala ibadilishwe, tuwafundishe vijana wetu, tuwape stadi ambazo watakwenda wakitoka pale wajiajiri, wafanye vitu vinavyoonekana, yaani mtu akimaliza Darasa la Saba awe na skills za kumsaidia kwenda kuzalisha. Akimaliza Form Four iwe hivyo hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba niishauri Wizara ya Elimu ibadilishe mitaala ifanye kilimo; kikijumuisha, kilimo, mifugo na uvuvi; liwe ni somo la lazima kuanzia Darasa la Kwanza mpaka Kidato cha Nne. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tukifanya hivi tutawafundisha hawa vijana kwa vitendo, tutaweka components nyingi. Nimesema kwenye hiki kilimo kitakuwa na hivyo vitu ambavyo nimevitaja, tutawafundisha ujasiriamali na ubunifu wa miradi ya kilimo kwa vitendo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ni mtaalam wa kilimo. Ni kwa nini nilienda kilimo? Hiki kitu nilikipata Shule ya Msingi. Kuna siku tulikwenda kwenye study tour, kwenye Kituo kimoja cha Utafiti wa Kahawa kule Lyamungo, nikaona walivyopanda kahawa kwenye mistari, mahindi kwenye mistari, maharage kwenye mistari, nikasema hapa hapa, mimi nakwenda kusoma kilimo. Leo hii nami ni mtaalam wa kilimo na nimeshatoa mchango mkubwa sana kwenye nchi hii, kwenye hiyo sekta. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kama tutabadilisha mitaala yetu tuhakikishe kuanzia Elimu za Awali, hii program ya Serikali ambayo Mheshimiwa Waziri ame- present hapa; kuanzia zile programs za awali tunafundisha vijana wetu kilimo, nakuhakikishia watakapotoka pale watakwenda kujiajiri na watafanya vizuri, watachukua urithi wa wazee ambao sasa hivi wengi wamechoka na hawawezi kulima tena. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye kilimo masoko yapo. Mahali pa kuanzia; kijana akijiingiza kwenye kilimo, akilima mahindi, mboga, mpunga, akazalisha mchele, Fuso huwa zinakwenda mpaka kijijini kuchukua haya mazao kule. Kwa hiyo, mahali pa kuuza kwa kuanzia sidhani kama ni shida kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ni ushauri wangu kwa Wizara ya Elimu mlizingatie hili, tuwafundishe vijana wetu kilimo, ambapo nimeshasema kinabeba vitu vingi tu, ili waweze kujiajiri watakapomaliza Darasa la Saba na waachane na yale mambo ya kwenda kufanya umachinga, kuendesha bodaboda ama kuajiriwa kwa watu wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hilo, nafikiri ni wakati sasa wa Serikali kuanzisha program maalum kila Wilaya kwa ajili ya vijana wetu na hizi Wilaya zitenge maeneo ya kutosha kwa ajili ya vijana. Haya maeneo yatatumika kama block farm zile ambazo Mheshimiwa Bashe amekuwa anasema, tuwapatie maeneo ya kulima, kufuga, maeneo ya kuanzisha visima vya kufugia Samaki. Kwa kufanya hivyo, watakuwa wamejiajiri baada ya kupata study hizi kule Shule ya Msingi na Sekondari. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tukishatengeneza hizi block farms, kwa mfano tukienda kule Kilimanjaro, wale wazee wangu kule kuna mashamba mengi yametaifinishwa, mashamba ya ushirika, nawashauri ikiwezekana yale mashamba badala ya kupiga kelele wanayatumia vibaya tuwape vijana walime kwenye hizi block farms, vijana walime kwenye haya mashamba ili wazalishe na waweze kuondokana na umaskini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye hizi block farms zitakuwa, tukishakuwa nazo itakuwa ni rahisi kuweka miundombinu ya umwagiliaji, kitakuwa ni kitu kirahisi sana, tutaweka miundombinu ya umwagiliaji na vijana wanaweza wakavuna mara mbili hadi tatu kwa mwaka. Nitatoa mfano kidogo tu, kijana akilima mboga ekari moja, tuseme amelima nyanya ana uhakika wa kupata milioni 22 kama amewekeza. Nisikilizeni vizuri jamani, ekari moja ya nyanya unaweza ukapata milioni 22 na hapo ukitoa milioni moja ya kununua pembejeo, mbegu na vitu vingine unabaki na milioni 21. Kuna kijana atakayekwenda kuwa Mmachinga kweli, huo ni msimu mmoja na ukilima misimu miwili, ni pesa nyingi zimekaa, zimelala ambazo naomba tusaidiane ili vijana wetu wajiingize kwenye hii miradi ya kilimo na waweze kujipatia pesa ili waoe. Vijana wengi sasa hivi ukimwambia aoe anakwambia hapana maisha magumu bwana, nioe nitampa nini, lakini pesa zipo kwenye kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile wakiwa kwenye hizi block farms wanaweza wakapatiwa huduma za ugani, watafundishwa namna ya kuzalisha vizuri, wanaweza wakapatiwa mitaji na mikopo itakuwa ni rahisi sana kuwasaidia hawa vijana wapatiwe mitaji na mikopo. Nitatoa mfano tu, kuna maeneo mengi ambayo yana pesa ambazo vijana wanaweza wakazi-access na wakafanikiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna ule Mfuko wa Halmashauri, asilimia nne ambazo huwa zinatolewa, vijana wanaweza wakazipata. Kuna Benki ya Kilimo ya Taifa inaweza ikawasaidia hawa vijana, kuna mfuko wa kutoa mikopo kwa wajasiriamali wadogo, unaitwa SELF Microfinance Fund, kuna Mfuko wa Pembejeo wa Taifa, wenzangu wameshausemea hapa, kuna Mfuko wa Taifa wa Kuendeleza Wajasiriamali, kuna Mfuko wa Maendeleo ya Vijana (Youth Development Fund), kuna Mfuko wa Mheshimiwa Rais wa Kujitegemea (Presidential Trust Fund). Tukiweza kuwaunganisha vijana wetu na hii Mifuko, tukiwapa maeneo Mungu atupe nini? Nina hakika vijana watazalisha kwa hakika na tutawatoa kutoka hatua moja waende hatua nyingine, haya mambo ya kwenda kuwa Wamachinga, bodaboda yatakuwa ni historia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tukishafanikisha hilo, pia ni rahisi kuwaunganisha na masoko ya ndani. Tumeshaona jitihada za Wizara ya Kilimo kwenye kutafuta masoko kwa mfano sasa hivi wanaotaka kulima soya soko lipo China, wanaotaka kulima mihogo Serikali imeshatafuta soko China. Kwa hiyo sidhani kama kutakuwa na shida kubwa sana ya soko na wakishaanza kuzalisha ni rahisi kuwaelekeza pia wafungue viwanda vidogo vidogo, waongeze thamani kwenye mazao watakayolima pale, kwa mfano wanaolima mpunga, wakishakoboa mchele badala ya kuuza raw rice wanaweza wakafanya packaging; wanaolima mahindi wanaweza wakasaga wakapaki; wanaolima nyanya wanaweza wakasaga wakakausha wakapaki, wakawa wameongeza thamani; TBS ikawasaidia vijana watakuwa wameanzisha viwanda vidogo vidogo kwa kusaidiana na SIDO na tutachangia kikamilifu kwenye uchumi wa Taifa hili.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa, kengele ya pili imeshagonga.

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)