Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge

Hon. Agnes Elias Hokororo

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge

MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Kwanza kwa kuwa nami ni Mjumbe wa Kamati, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.

Mheshimiwa Spika, nianze kwanza na hoja ambazo pengine watu wamekuwa wakijiuliza, maana ukisikiliza nje ya sisi Wabunge, wapo baadhi ya wananchi katika makundi mbalimbali wanahoji pia kwamba kwa nini Waheshimiwa Wabunge hawa wawili ambao ni mashahidi walitokea mbele ya Kamati ama waliitwa kwenye Kamati yako ya Bunge?

Mheshimiwa Spika, naomba niliweke wazi hili kwa sababu pengine hawajui kwamba mashauri haya yote mawili yameshughulikiwa chini ya Sheria ya Haki, Kinga na Madaraka ya Bunge Sura ya 296. Kwa hiyo, siyo suala tu kwamba labda mhimili huu wa Bunge uliamua tu wenyewe bila kufuata sheria; ni kwamba ni suala la kisheria. Pia niwaambie wale ambao pengine wamepata mashaka kwamba masuala haya yote mawili yameshughulikiwa kwa mujibu wa Kanuni za Bunge. Bunge lako Tukufu linaendesha shughuli zake kwa kufuata Kanuni za Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilikuwa naomba nilieleze hili kwa sababu baadhi huko ukisilikiliza wanasema wameonewa, mtu kwa nini ameitwa? Kwa nini hakwenda huku? Kwa nini huku? Pengine wanadhani ni shinikizo la mtu mmoja, lakini kumbe huu ni utaratibu wa kibunge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mashauri haya yote mawili kama ambavyo Mwenyekiti wa Kamati amewasilisha mbele ya Bunge lako Tukufu, yote yameangukia katika Kanuni ya 85 - Utovu wa Nidhamu Uliokithiri.

Mheshimwia Spika, hapa pia naomba nianze na shauri lile la kwanza la Msheshimiwa Josephat Gwajima. Sote tunatambua kwamba Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imetoa uhuru wa kuabudu, lakini uhuru huo wa kuabudu tunaopewa Watanzania na watu kuanzisha taasisi za kidini hupaswi kuvunja masharti ambayo Katiba hiyo imeweka na sheria nyingine za nchi yetu. Tunajua sote kwamba hakuna uhuru usio na mipaka; yaani haiwezekani mimi leo; na kwa sababu kuanzisha Kanisa au taasisi ya kidini mtu yeyote anaruhusiwa; haiwezekani leo nikatoa maneno ambayo yanavunja sheria nyingine za nchi tu kwa kisingizio cha uhuru wa kuabudu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwa maneno ambayo yalisemwa na shahidi hayana shaka. Naomba niungane na Wabunge ambao wametangulia kwamba maneno yale yanaweza kuvunja amani na utulivu wa nchi yetu. Sasa tukiachia hiyo tukasema sasa kila mtu aamke tu, sidhani kama tunaweza tukaendelea kufurahia nchi yetu katika uwanda huu mpana wa utulivu ambao unamwezesha kila Mtanzania kufanya shughuli zake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge King hapo amesema, ukiacha ile mifano ya Kibwetere, tuliona pia kwenye maeneo mbalimbali; nakumbuka kama sikosei kule Kagera kuna mchungaji alitokea Kanisani akasema ameoteshwa aoe mke wa mwingine Kanisani, lakini tuliona Serikali pia ambaye ni Mkuu wa Wilaya alienda akachukua hatua kuhusiana na lile. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia yapo maeneo mengine. Kwa hiyo, kwa ufupi tu tuseme kwamba hili pia ambalo limefanywa na Mheshimiwa Gwajima kwa kisingizio kwamba alikuwa anasema yale maneno akiwa anahubiri waumini wake kwenye nchi 142; na kwa kuwa alikiri Tanzania ni miongoni mwa hizo nchi 142; kwa kufanya hivyo kwa kweli sioni kama kuna shaka kwamba alikuwa anajaribu kuizua Serikali kutekeleza wajibu wake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niwasihi Wabunge kuliunga mkono Azimio hili la Bunge ili kuendelea kuulinda utulivu wa nchi yetu, kuilinda amani ya nchi yetu na pia kuleta ustawi wa jamii zetu. Hii chanjo ambayo pengine watu wanahimizwa wasiende kuchanja, tuliambiwa wote ni kwa hiari, lakini pia mashaka yale mengine ambayo yametolewa na mzungumzaji yanaendelea kuwachanganya wananchi. Kwa sababu akisema daktari yeyote atakayebisha amepewa pesa, sasa tunaendelea kuwachanga wananchi. Kwamba hawa hawa Wabunge wanasema hii chanjo isichanjwe kwa sababu hakuna nafasi ambapo Mbunge anapofanya shughuli nyingine nje ya Bunge utasema sasa mimi Agness Hokororo sio Mbunge, nafanya kazi zangu kama mwananchi wa kawaida kwa sababu wote tumekula kiapo kwa mujibu wa Katiba.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana, ahsante Mheshimiwa.

MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naunga mkono hoja.