Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge

Hon. Kilumbe Shabani Ng'enda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kigoma Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge

MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Nataka niseme kwamba sina kawaida sana ya kuzungumzia mambo hasa ninayoona yananitia uchungu kwa watu ninaowafahamu vizuri na hasa Wabunge wenzangu, lakini mnapofika mahala mnataka kutengeneza chombo ni lazima mkubali kwamba, kama yuko mtu anapasua mtumbwi ili mzame, basi bora azame yeye lakini chombo kiendelee kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sisi Wabunge tuliomo humu tumeletwa na vyama vyetu kupitia kura za wananchi, vyama vyetu vina katiba na miongozo, chama kikongwe kama CCM kina mpaka Kanuni za Maadili na Uongozi, zinazoonyesha miiko, zinazoweka makatazo na utaratibu. Kwa bahati mbaya, niseme kwa mfano Shahidi Mbunge mwenzetu Mheshimiwa Gwajima, labda muda wake wa kuwepo kwenye CCM umekuwa ni mfupi sana, labda mambo haya hajapata nafasi nzuri ya kuyasoma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, si hilo tu, tukishachaguliwa tukifika hapa, hatuanzi kazi mpaka tubebe Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na tuape kuitii, kuitetea kwa mujibu wa sheria. Katiba hiyo inayo mambo ambayo yanatutaka lazima tuyafanye kwa sababu tumeapa, unashangaa na unajiuliza na unapata shaka, hivi hawa wenzangu wanapata nafasi ya kupita hii miongozo. Kama wangefahamu vizuri nadhani tusingefika huku tulipofika. Alipoanza Mbunge mwenzetu Mheshimiwa Gwajima, alianza kama anatoa ushauri hivi, akaeleza kuhusu hizo chanjo na nini, halikuwa jambo baya na wakati huo Rais wetu mpendwa alikuwa ameunda Kamati ya Wataalam kumshauri kuona namna ya kuliendea jambo la kupambana na COVID. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata kama unaamua kumshauri Rais, Katiba ulioapa nayo Ibara ya 37 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, inayoeleza majukumu ya Rais, inaonyesha kwamba Rais yuko huru katika kazi yake, halazimiki kufuata ushauri, ukimpa anaweza akauchukua au asiuchukue na atatimiza wajibu wake. Kama Rais alikua ameshaunda Kamati ya Wataalam hana lazima ya kusikiliza ushauri wa Askofu, maana jambo lenyewe la ugonjwa ni la kitaalam.

Mheshimiwa Spika, tuache Katiba na miongozo ya chama, ndugu yetu huyu ni mtumishi wa Mungu, Askofu, imeshafika mahali jambo liko kwenye mamlaka ya Rais analishughulikia, unawezaje kufika mahali ukaanza tena kuhoji, kwenda mbele kuchochea watu, hasomi hata Biblia yenyewe inasemaje? Kwamba mtii mamlaka maana hakuna mamlaka isiyotoka kwa Mungu (Makofi)

Mheshimiwa Spika, haya ya Kanuni, ya Katiba yamempita na ya Biblia yamempita? Si hilo tu hata sisi tunaoamini katika Uislamu imeandikwa atwiu-Allah, waatwiu rasuli wauli-l-amri minkum, kwamba tumtii Mwenyezi Mungu, tumtii Mtume na tuwatii wenye mamlaka miongoni mwetu. Huu aliouonesha mwenzetu siyo utii kwa mamlaka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa bahati mbaya, tunapokuwa hapa ni vizuri tujue viwango vyetu, umeingia siasa jana, Ubunge una miezi sijui sita au tisa, lakini hata huko kwenye Biblia, si tuyaishi maneno ya Bwana Yesu. Ukialikwa kwenye harusi usikae viti vya mbele, maana mwenye harusi anaweza akaja na watu muhimu akakupeleka nyuma, kaa viti vya nyuma ili kama yeye atakuona wa muhimu akulete mbele maana ajikwezae hushushwa na ajishushae hupandishwa na haya maneno hayajui? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa amekuja hapa Mheshimiwa Gwajima amekaa viti vya mbele, hata sisi tuliokaa siku nyingi humu kwenye chama hiki tunamwangalia, lakini basi umefika mahali umekaa viti vya mbele, unaanza tena kupiga mawe kiti cha bwana harusi na sisi tukuangalie tu haiwezekani. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wabunge karibu wengi ambao tumekutana huko nje tunazungumza juu la tukio hili la mwenzetu, kila mmoja anasema kwa kweli huyu bwana kafanya vibaya. Sasa ukiwauliza mbona hamkemei, wanasema hapana tunaogopa, atapanda madhabahuni kwenda kutuchapa pale kutukashfu. Mheshimiwa Gwajima, Mbunge mwenzangu, mimi nimejitoa kama dhabihu, nipeleke kwenye madhabahu siku ya jumapili, nichape ujuavyo, lakini mwachie Mama Samia na Serikali yake wafanye kazi. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, narudia tena nimejitoa, nikwambie kwa nia ya kukurekebisha kama Mbunge mwenzetu, twende pamoja, ukiamua kwenda kutumia jukwaa la Mungu badala ya kuongoza kondoo kuanza kuwasema watu, endelea hivyo ila ujuwe Mungu anakupa muda. (Makofi)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Kilumbe Ng’enda.

MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Spika, naomba dakika moja.

SPIKA: Haya malizia.

MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Spika, mimi nimechukulia wito wa mama yetu na juhudi alizozifanya Mheshimiwa Rais wetu, tena nimenukuu maisha ya Nabii Nuhu, alipoona watu wake wanatenda makosa mengi kwa Mungu na Mungu akamletea ufunuo kwamba, mimi nataka kugharikisha, alikwenda akawasihi watu wote, jamani tutengeneze safina tupande, Mungu analeta gharika kutokana na makosa tuliyofanya, sasa tujisalimishe tukae kwenye safina. Wako baadhi ya watu mpaka ya wa familia yake walimpinga. Kilichotokea gharika ilikuja na wote waliompinga waliangamia. Mama ametutaka tuchanje na akatuomba kwa hiari anayetaka achanje, asiyetaka aache, sisi tulioamua kuchanja tunasubiri safina iwe tayari, wale ambao wamekataa litakapotokea gharika ya Mungu shauri yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivi kweli angekuwa Mheshimiwa hayati Magufuli ndiyo Rais leo, Mheshimiwa Gwajima angeweza kusema hayo aliyoyasema? Wakati wa mwalimu Julius Kambarage Nyerere, mwaka wa 1979, alikuwepo Mjumbe mmoja wa Halmashauri tena Mjumbe wa Kamati Kuu na alikuwa Mkuu wa Idara ya Organization, namkumbuka alikuwa mtu wa kwetu, mzee wetu, ameshatangulia mbele ya haki, Mungu amuweke mahali pema, alikua anaitwa Tuwakali Karangwe. Iliwekwa karantini ya kipindupindu alipokwenda kule Kigoma akakuta ma- barrier watu wanazuiwa wasiende huku kwa imani tu ya kutaka watu wala sio kwa kiburi, akawaambia fungueni watu waende wakapate huduma, kipindupindu kikaathiri watu wakafa, alilazimika kujiuzulu nafasi zake zote za uongozi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mtu anachochea watu wasichanjwe na kushambulia wale wanaohamasisha na wanaoleta chanjo, katika CCM hii ninayoijua adhabu bado.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja, nakitaka chama kiangalie vizuri adhabu hii. Ahsante sana. (Makofi)