Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge la Kutambua na Kuenzi Mchango wa Rais wa Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, kwa Utumishi wake Uliotukuka Pamoja na Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Hon. Prof. Kitila Alexander Mkumbo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ubungo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Azimio la Bunge la Kutambua na Kuenzi Mchango wa Rais wa Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, kwa Utumishi wake Uliotukuka Pamoja na Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru na mimi kwa kunipa nafasi hii kuchangia maeneo haya mawili katika maazimio yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze mchango wangu kwenye hiba. Hiba ya Mheshimiwa Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, hiba ni urithi au waingereza wanasema legacy. Hili naamini wasomi wataandika kwa muda mrefu ujao kwaajili ya kuweka kumbukumbu sawasawa; mchango ambao Mheshimiwa Rais wetu wa Tano alitoa.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa duniani maisha yetu ni mafupi, na kifo cha Dkt. Magufuli kinatukumbusha kwamba hapa duniani Maisha yetu ni mafupi sana. Muhimu sana kwa kweli ni kwamba, sio kwamba tutakufa au la, kufa tutakufa, lakini tukifa tunapoondoka tutakumbukwa kwa lipi? Mwenzetu kwa kweli ameondoka akiwa ameacha alama kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa duniani tunaambiwa kuwa kuna mambo mawili, kuna kutoa na kupokea. Wengi wetu huwa tunapokea, lakini tunapata baraka kwa kutoa, mwenzetu ametoa, ametoa maisha yake, ametoa kupitia mchango mkubwa wa kazi zake ambazo tutaendelea kuziishi kwa muda mrefu bila kuorodhesha mambo mengi ambayo ameyafanya ambayo watu wengi wameyasema.

Mheshimiwa Naibu Spika, na uteuzi wa leo wa Makamu wa Rais ni jibu na ujumbe kwamba kazi inaendelea. Hilo ndilo jibu ambalo tunapewa kwamba, ni stability and continuity. Kwamba kitabu kinaendelea kuandikwa tunaendelea kwenye ukurasa mwingine. Tunashukuru sana kwa uteuzi ambao Mheshimiwa Rais ameufanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, kifo hiki kinatukumbusha miaka 20 iliyopita. Tarehe 4 Julai, 2001 nchi yetu ilikumbwa pia na msiba wa Makamu wa Rais Dkt. Omari Ali Juma. Mheshimiwa Mkapa alipomteua Dkt. Ali Mohamed Shein alitoa sababu kwa nini amemteua. Alitoa sababu sita ambazo kwa kweli ukizirejea, ndizo unazoziona leo kwa viongozi wetu wawili wakuu; kwa maana ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, lakini hata uteuzi wa leo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na kwa ruhusa yako naomba nizirejee hizo sifa sita ambazo zilimuongoza Mheshimiwa Mkapa kumteua Mheshimiwa Ali Mohamed Shein. Yeye alisema kwamba, Watanzania wanatarajia sifa zifuatazo kutoka kwa viongozi wao; na ameandika pia kwenye kitabu chake kwamba ndivyo kigezo cha viongozi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sifa ya kwanza ni utu na uadilifu. Yamesemwa hapa kuhusu utu na uadilifu wa Mama Samia lakini pia wa Mheshimiwa Dkt. Mpango. Upendo na heshima kwa watu wote. Kupenda kazi na kutumikia wananchi badala ya kupenda kutumikiwa na kukuzwa. Watu wengi wenye vyeo tuna shida moja. Ukiwa na cheo kuna mawili, unataka watu wakikuona wakuone nini? Wakimuona Kitila wamuone Kitila kwanza Waziri baadaye, ama Waziri kwanza Kitila baadaye? Watu wengi wanataka waonwe kwanza kwa vyeo vyao, halafu baadaye wao. Hapa Mheshimiwa Mkapa anasema, kiongozi mzuri ni yule ambaye anataka kwanza kabla ya cheo chake watu wamuone yeye, na hii ni sifa ya msingi ambayo viongozi wetu wawili wanayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini naiweka vile vile namba nne, kuweka mbele maslahi ya taifa na Watanzania badala ya maslahi binafsi, viongozi wetu tunawafahamu vizuri. Unyenyekevu, limezungumzwa sana hili, viongozi wetu wawili Mheshimiwa Rais tangu aanze kazi hii; na watu wanaomfahamu kabla tuliopata nafasi na bahati ya kufanya naye kazi kabla tunafahamu unyenyekevu wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mwisho ni kuzingatia misingi ya Taifa; na aliitaja misingi tisa; utu, haki, usawa, fursa sawa, amani, umoja, upendo, mshikamano na hii ya mwisho aliandika kwa herufi kubwa MUUNGANO. Kiongozi yeyote katika nchi hii lazima tukimuona, tukimuangalia, tukimsikia tuwe na hakika kwamba Muungano wetu upo salama. Hakuna shaka kwamba kwa viongozi wetu wawili hawa Muungano wetu upo salama sana. Na hilo ni jambo la msingi mno. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho ni ukuu wa Katiba yetu. Watu wamelizungumza hili na limezungumzwa sana lakini sidhani ni kwa uzito ambao tunapaswa kuuona. Marekani wameshafiwa na Marais nane, wakiwa madarakani tangu mwaka 1841 na juzi 1993; na muda wote walikuwa na changamoto ya namna ya kumuapisha Makamu wa Rais, wamehangaika wameweza kufanikiwa kufanya mabadiliko 25 mwaka 1967. Sisi walioandika Katiba Mungu awabariki. Katiba yetu ina ukuu wa pekee, tumepita katika kipindi kigumu wala tusijue kwasababu Katiba yetu na misingi ipo salama.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninamtakia Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan na Makamu wa Rais na viongozi wote neema na baraka na mafanikio tele katika uongozi wao. Mungu awabariki sana. Ahsante. (Makofi)