Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge la Kutambua na Kuenzi Mchango wa Rais wa Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, kwa Utumishi wake Uliotukuka Pamoja na Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Hon. Timotheo Paul Mnzava

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Korogwe Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Azimio la Bunge la Kutambua na Kuenzi Mchango wa Rais wa Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, kwa Utumishi wake Uliotukuka Pamoja na Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami nipate fursa ya kuchangia maazimio haya mawili yaliyoletwa mbele yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee kabisa nami niungane na wenzangu kutoa pole kwa Mheshimiwa Rais na Watanzania kwa ujumla kwa msiba mzito ambao ulitufika kama taifa wa kuondokewa na mpendwa wetu Dkt. John Pombe Magufuli aliyekuwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, maazimio haya yamekuja kwa wakati sahihi na ni jambo sahihi na ni jambo muhimu na kubwa sana kufanywa na Bunge lako Tukufu. Katika miaka sita ambayo Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli amehudumu kama Rais wa nchi hii amefanya mambo makubwa, amefanya mabadiliko makubwa sana kwenye taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukisema tuanze kueleza kazi nzuri na njema alizofanya Dkt. Magufuli, hata muda huu haunitoshi kusema yote mazuri aliyoyafanya. Lakini kama Mbunge na kama Mbunge kijana, nianze kabisa kwa kutambua mchango na thamani kubwa ambayo Dkt. Magufuli aliitoa kwa vijana wa taifa hili kwa kuwateua kwenye nafasi mbalimbali za uongozi ndani ya nchi yetu. Mheshimiwa Dkt. Magufuli aliwaamini sana vijana, aliwapa nafasi za kufanya kazi na kuitumikia nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika,inawezekana yako maeneo tumemuangusha kidogo lakini kwa sehemu kubwa vijana aliowateua walifanya kazi nzuri ya kumsaidia na kuleta uongozi kwenye taifa letu. Sisi kama vijana tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais Dkt. Magufuli kwa imani hiyo kubwa kwa vijana. Amewatengeneza watu wengi kuwa viongozi na kuweza kutoa mchango kwenye taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine kubwa zaidi alilofanya Dkt. Magufuli ni kutusaidia kukamilisha ndoto kubwa tulizokuwa nazo kama taifa kwa miaka mingi. Kwa muda mrefu tumekuwa na ndoto ya kuifanya Dodoma kuwa Makao Makuu ya nchi yetu lakini tulikuwa tukisuasua kwenye utekelezaji wa jambo hili. Dkt. Magufuli kwenye kipindi chake amesimama imara jambo hili limefanikiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, hakuishia kuhamishia tu makao makuu, alihakikisha kwamba Wizara za Serikali zinapata majengo mazuri na ya kudumu kwenye eneo la Dodoma ili Serikali iweze kufanya shughuli zake vizuri hapa Dodoma. Ni muhimu sana kuendelea kuenzi mchango huu. Pia amefanya kazi kubwa kwenye kusimamia rasilimali za taifa letu. Tulibadilisha sheria kwenye usimamizi wa madini na nchi yetu imeongeza thamani na imeongeza mapato kutoka kwenye rasilimali tulizokuwa nazo kama taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kazi nzuri alizofanya Dkt. Magufuli, lakini kwa mara ya kwanza kama kijana wa Kitanzania nimeona na kusuhudia kitu cha tofauti. Nimeona na kushuhudia baadhi ya watu wakifurahia kifo na kusema maneno yasiyokuwa mazuri. Kwa umri wangu mdogo, kwa nilivyolelewa kwa utamaduni wetu si jambo zuri sana kufurahia kifo cha mtu mwingine. Lakini pia si jambo zuri kukosoakosoa mtu akiwa ameshatangulia mbele ya haki. Ninawaomba Watanzania, Dkt. Magufuli ameifanya kazi yake vizuri, ameimaliza safari yake, amefunga kitabu chake. Tumpe heshima anayostahili, tuendelee kumuomba Mwenyezi Mungu amhifadhi mahali pema peponi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuondoka kwa Dkt. Magufuli tumempata mama yetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, kipekee kabla ya kumpongeza Mheshimiwa Samia ni lazima Watanzania tujipongeze kama taifa. Tumepita kwenye kipindi ambacho pengine kuna watu walikuwa wanatuangalia kama tutavuka salama au hatutavuka salama. Lakini leo tunapozungumza kwa uimara wa Katiba iliyotengenezwa na waasisi wa taifa letu, kwa uimara wa sisi Watanzania na kupendana kwetu, kwa uimara wa vyombo vyetu vya ulinzi na usalama, kama taifa tunavuka salama na tunavuka vizuri. Tunayo sababu ya kujipongeza na kujivunia Watanzania, ni jambo kubwa ambalo tunaweza tukaliona kama ni jambo la kawaida, lakini ni jambo kubwa sana kuvuka kwenye kipindi kama hiki tukiwa salama na tukiwa tumeendelea kushikamana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi hii kuendelea kumpongeza sana Mheshimiwa Samia kwa kupata nafasi ya kuwa Rais wa Nchi yetu. Mheshimiwa Samia ana uzoefu mkubwa kama ilivyosemwa na aliyewasilisha hoja ya Azimio la Kumpongeza. Ana uzoefu mkubwa kwenye kuongoza Serikali ya nchi yetu, ana uzoefu mkubwa kwa uongozi wa Serikali kwa pande zote mbili za Muungano, na hili ni jambo la kipekee na muhimu sana. Tunampongeza kwa kupata nafasi ya Urais. Tuna matumaini kwamba ataifanya kazi hii vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Samia ni mchapakazi. Kama wako watu ambao wanafikiri baada ya kuondoka kwa Dkt. Magufuli mambo yatalegalega, wanafikiri watapata nafasi ya kuja kuiibia na kuifisadi nchi yetu, kwa mama Samia nafasi hiyo haipo. Ni mama mwadilifu anayependa taifa lake, mama mzalendo anayeichukua rushwa na mchapakazi wa kweli.

Mheshimiwa Naibu Spika, tarehe 15 ya mwezi Februari tulikuwa Korogwe kwenye ziara na Mheshimiwa mama Samia akiwa Makamu wa Rais. Tulikuwa na daraja linasumbua akiwa mama kwa muda mrefu, tulipomueleza akatoka palepale akafanya mawasiliano na Wizara na TARURA wakasema hawana fedha. Akawaambia hata kama hakuna fedha jengeni kivuko ambacho akina mama wanaokwenda kupata huduma za afya hawatateseka. Leo ninapozungumza mkandarasi yuko site ameshashusha vifaa na kazi inafanyika; ni ufuatiliaji wa mama Samia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie kwa kusema kwamba mama Samia Suluhu Hassan si mtenda miujiza. Kama ambavyo tumetoa ushirikiano kwa Dkt. Magufuli, nawaomba Watanzania tumuunge mkono Mheshimiwa Rais, nawaomba tumuombee, nawaomba tushirikiane naye ili mama huyu aweze kuifanya kazi vizuri aende mbali zaidi kuanzia pale alipotuacha Dkt. John Pombe Magufuli.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na ninaunga mkono maazimio yote mawili. (Makofi)